Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba nichangie machache katika mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka kuiomba Serikali kuwa, mipango inayotuletea kwa kweli ni mizuri sana na imepangwa kwa utaratibu mzuri sana wa kimkakati, lakini nafikiri katika mapendekezo mengi na maoni mengi yanayotolewa na Wabunge ni dhahiri kuwa, tuna tatizo la utekelezaji kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi hasa ile ya kimkakati imekuwa katika majadiliano kwa muda mrefu, tungetegemea sasa tuanze kuwa tumeweka mpango wa kuanza kuitekeleza. Tunajua kuwa mengine hatua ambayo imefikiwa ni nzuri, lakini kuna mambo machache tu ambayo yanatakiwa yakamilishwe ili miradi hii ianze kufanya kazi na ianze kutuletea faida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie miradi mikubwa ya kielelezo ambayo tumeipitisha hapa na imeonekana kuwa ingesaidia sana nchi yetu hasa katika wakati huu ambao tunalenga kuingia katika uchumi wa viwanda. Nataka nitaje mradi kwa mfano wa Mchuchuma na Liganga. Huu ni mradi ambao kwa kweli ungeanza kutekelezwa ilivyoandikwa au ilivyopangwa ni mradi ambao ungeiondoa nchi yetu katika uzalishaji wa chini na kutuingiza katika viwanda kwa haraka zaidi, maana ingetuletea malighafi muhimu sana kwa ajili ya viwanda vingine, lakini nasikitika kuwa mpaka sasa hivi bado haujakamilishwa na tunaambiwa kuwa pengine ni masuala machache tu yaliyobakia kujadiliwa. Je, kwa nini Serikali isiharakishe majadiliano hayo ili sasa huu mradi uanze kufanya kazi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunapozungumzia mradi huu wa Liganga na Mchuchuma, huu mradi utashughulikia makaa ya mawe, tunajua ni bidhaa ambayo ni kubwa, nzito na kwa vyovyote vile inahitaji miundombinu muhimu ya kusafirishia. Kulikuwa kuna mpango wa kujenga reli kwa ajili ya kupitisha makaa ya mawe kutoka katika maeneo ya mradi hadi bandarini, tungependa kujua fedha imeshawekwa kwa ajili ya kufanyia kazi hiyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo kwa kweli linawagusa wananchi moja kwa moja. Wenzangu wengine wamegusia ni suala la kilimo, ni suala la maji, ni suala la afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kukaa hapa tunazungumzia uchumi, tunazungumzia kilimo chenye tija bila kuzungumzia maji kwa maana ya umwagiliaji kwa maana ya maji salama yatakayotumiwa na wananchi, vilevile maji ya kusindika mazao ya kilimo na mazao ya mifugo. Kwa hiyo, tungependa sana kuona mkakati unawekwa kuhakikisha kuwa fedha ya kutosha inawekwa katika maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia kilimo, wananchi wengi wangependa kulima kisasa, mashamba makubwa kwa tija, lakini hawawezi kupata mikopo. Kwanza Benki ya Kilimo haina mtaji wa kutosha, pili mashamba yao hayajapimwa. Kwa hiyo, hata kama Benki ya Kilimo ingeweza kuwakopesha, hawatakopeshwa kwa sababu mashamba yao hayajapimwa, hivyo, tunajikuta bado tuna tatizo, tunazunguka palepale, tunazungumzia kilimo lakini hatuwezeshi kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa Serikali ije sasa ituambie kuhusiana na suala hili la kilimo ambalo ndilo linaloajiri wananchi wengi na ambalo linge-absorb vijana wetu wengi, wangelima kwa tija na kibiashara tusingekuwa tunalia kuwa vijana wengi hawana ajira. Vijana wengi wangefuga, vijana wengi wangekuwa wanauza na kusindika na tungekuwa hatuna shida na uchumi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji kama nilivyozungumzia, kuna mikakati iliwekwa hapa na Serikali, tukaipitisha Bungeni juu ya kuweka tozo maalum kwa ajili ya kuhakikisha kuwa Mfuko wa Maji unaundwa na unafanya kazi. Hatujui lile limefikia wapi, lakini tungependa Serikali iangalie uwezekano hata wa kuongeza ile tozo ili miradi ya maji yote itosheleze, bila maji ndugu zangu tutaongea mambo yote hapa lakini tunafanya kazi bure.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna suala vilevile la vituo vya afya na zahanati nchi nzima. Ndugu zangu tunapokuwa tuna matatizo ya maji ni rahisi sana wananchi kupata maradhi, wananchi wakipata maradhi tunazungumzia sasa kwenda hospitali ambako tena hakuna vifaa au huduma muhimu. Kwa hiyo, tunajikuta tunazunguka katika mzunguko wa umaskini na inefficiency ambayo kwa kweli hatuikubali kama Wabunge, maana sisi ndiyo tuko na wananchi kule tunasumbukanao sana juu ya masuala haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tuliomba, mwaka huu wakati wa bajeti tuliyoipitisha ya mwaka huu na mwaka wa kesho tuliomba tuongezewe fungu fulani kwa ajili ya kujenga zahanati na vituo vya afya ili vikamilike na vingi wananchi tayari walishajitolea, vipo. Tunaomba Serikali itusaidie kwa hilo, ile miradi muhimu ambayo ni kichocheo cha uchumi, cha uzalishaji kwa wananchi, ifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuisisitiza hii kwa sababu hiyo ndiyo miradi ambayo inawagusa wanawake wengi. Wanawake wengi ndio wazalishaji vijijini, wanawake wengi ndio wanaohangaika na maji, wanawake wengi ndio wanaohangaika na watoto wagonjwa na wao wenyewe wakiugua, lakini huduma zote ambazo zinawagusa akinamama ndio hizo ambazo tunazipigia kelele sasa. Tunaomba Serikali wakati mnaangalia mambo makubwa lakini na haya madogo msiyape kisogo kwa sababu yana umuhimu mkubwa sana kwa uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala ya miradi ya mikakati ya kielelezo, kwa mfano, General Tyre. Hakuna asiyejua umuhimu wa General Tyre ilipokuwa ikifanya kazi na tunaambiwa kabisa kuwa ilikuwa tayari ianze kufanya kazi. Tunajiuliza kimekwama nini sasa kwa General Tyre kuanza kazi? Tungependa kujua General Tyre kwa nini haijaanzishwa mpaka sasa hivi wakati kila kitu kilikuwa kiko tayari kuendelea?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka vilevile kuzungumzia NDC - Shirika la Taifa la Maendeleo. Hili ni shirika ambalo limepewa majukumu maalum kusimamia au kuibua miradi ya maendeleo na limekuwa likifanya hivyo, lakini fedha linayopata ni kidogo mno kiasi kwamba unashindwa kuelewa watafanyaje kazi. Mradi huu tunaozungumza wa Liganga na Mchuchuma ni mradi ambao upo chini ya NDC, mradi wa magadi soda upo chini ya NDC na miradi mingine mingi ambayo tunategemea NDC waisimamie lakini bila kuwa na bajeti ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tungependa sasa hivi kusikia kutoka Serikalini mipango mikakati yao ya kuhakikisha kuwa hii miradi sasa inaanza kufanya kazi. Tumekuwa tukiizungumza na imekuwa katika vitabu vyetu kwa miaka mingi sana sasa, tungependa tujue Serikali imeshatenga fedha ya kutosha kwa ajili hiyo? Lakini kama wao wenyewe hawana fedha tulishakubaliana kuwa tuna mpango wa PPP jamani siyo kila kitu lazima Serikali yetu yenyewe ifanye na uwezo huo bado hatuna. Kwa nini tusiachie huu mpango wa PPP sasa ufanye kazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa na nitafurahi sana kusikia Serikali ikisema kuwa kuanzia mwaka huu wa fedha tunaouendea tutakuwa na miradi kadhaa hata kama ni mitatu tu mikubwa ambayo inaendeshwa kwa mpango wa PPP ili kuipunguzia Serikali adha ya kuhakikisha inatafuta fedha yenyewe. Nchi nyingi zinazoendelea au zilizoendelea zilitumia mfumo huo kupunguza ule mzigo kwa Serikali kwa ajili ya bajeti yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nizungumzie masuala ya Economic Processing Zones na Special Economic Zones. Nchi nyingi kama China kwa mfano waliendelea haraka sana kiuchumi walipojiingiza katika mfumo huu wa maeneo maalum ya kiuchumi. Sisi tumeainisha maeneo mengi mengine tumeshalipa mpaka hata fidia, lakini hatufanyi chochote wakati huko ndio ambako tungehakikisha kuwa uwekezaji mkubwa unafanywa na sekta binafsi kwa ajili ya kuhakikisha kuwa tunaendeleza viwanda vyetu hasa vile vidogo na vya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vichache ambavyo tayari vimeshaanzishwa kwa mfano pale Dar es Salaam tunaona kabisa jinsi ambavyo vinazalisha na vimezalisha ajira nyingi sana, imagine kila mkoa ambako kulikuwa kumeainishwa maeneo hayo ingekuwa yanafanya kazi sasa hivi tungekuwa tunalalamikia ajira wapi? Kwa hiyo, nataka kusikia EPZ na Special Economic Zones sasa hivi Serikali inakwenda kufanya nini kwa maana ya utekelezaji, kwa maana ya nadharia na mipango tunayo tunaijua muda mrefu. Tunaomba sasa ikafanyiwe kazi japo tuone mradi hata mmoja unaanza katika hii miradi mikubwa ambayo imewekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la bandari; tumekuwa na mipango mizuri tuliyoiweka kwa ajili ya kupanua bandari zetu, magati yale ili kuhakikisha kuwa meli zinakuja kuweka nanga na kutoa mizigo na kuchukua mizigo, lakini yamekuwa ni mazungumzo ya muda mrefu. Mpaka wenzetu sasa wamestuka wao sasa wameshaendeleza bandari zao na tupo kwenye ushindani mkali sana. Nataka kusema hivi, haya mambo ya kusema ooh! wawekezaji wanatupenda jamani tuachane na hizo ndoto, anakupenda kwa sababu kuna kitu atakuja kunufaika na wewe, hakupendi kwa sababu wewe ni Mtanzania au kwa sababu sijui una sura nzuri au kwa sababu una amani. Naomba ndugu zetu Serikalini mtambue kuwa biashara ni mashindano, Kenya wakimaliza bandari zao, Kenya wakimaliza reli zao hao mnaowaita marafiki zenu hamtawaona na tukishapoteza wateja siyo rahisi kuwarudisha jamani yaani hiyo ni economic sense ya kawaida kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali yangu sikivu, hebu sikieni hili for the last time, hebu fanyeni hivi vitu sasa hivi viwe reality. Tunashindwa hata jinsi ya kuvitetea kwa wananchi kwa sababu ni kila mwaka wanaviona, vyote vipo vimeainishwa katika Ilani yetu lakini utekelezaji lini sasa? Na kama hatuna fedha viko vyanzo sasa through sekta binafsi ambavyo vinaweza vikafanya. Rahisisheni masharti kwa sekta binafsi wa-engage wasikilizeni sekta binafsi wana mawazo mazuri, wale ni wafanyabiashara na wanajua jinsi ya kuendesha biashara kwa faida na faida hiyo itapatikana kwa wote; ninyi Serikali na wao sekta binafsi. Ningependa sana kusisitiza kuwa hayo ni mambo ambayo lazima sasa hivi tuyawekee mikakati ya kufanya, yapo kwenye vitabu, yapo kwenye Ilani lakini sasa tuanze utekelezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la wajasiriamali wadogo na wa kati, bila kuwawezesha hawa hata hao wakubwa ambao tunataka kufanya nao biashara itakuwa ni kazi bure, hawa wadogo ndio watakaosaidiana na wakubwa, watakuwa na mahusiano yanayoshabihiana. Wakubwa watakuwa ndio wanunuzi wa huduma za hawa wadogo na wadogo ndiyo watakuwa wanapata ujuzi kutoka kwa wakubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tukawa tuna sekta ya chini kabisa na ya juu kabisa katikati hapa hakuna kitu, hakuna kitu kama hicho! Kwa hiyo, lazima wajasiriamali wadogo na wa kati wawe na mkakati maalum wa kuwasaidia kwa maana ujuzi, urasimishaji, lakini vilevile tuhakikishe kuwa kodi wanazotozwa jamani wanakuwa discouraged na kodi. Wanaanza tu hivi tayari wana mzigo wa kodi, haitawezekana kama tunataka kuwawezesha tuwape muda wafike mahali ambapo wataweza sasa kusimama ndiyo tuanze sasa kuwatoza kodi. Lazima tuwalee, mbona tunalea wakubwa, hawa wadogo kwa nini tunashindwa kuwalea na ni wazalendo na ndio watu wetu? Huko ndiyo vijana wetu watakapoponea katika masuala ya kiuchumi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala lingine la mabenki. Yamezungumzwa mambo mengi sana kuhusiana na mabenki kuwa yamekosa mitaji sasa yatakosa kukopesha, nataka kusema mabenki yetu yalikuwa yamelemaa, yalilemazwa na Serikali kwa ajili yalikuwa yanapata pesa za bure. Asilimia 20 ya Watanzania ndio ambao wanatumia mabenki, hawa wengine wote pesa zao ziko wapi? Mabenki yaanze kutoka sasa maofisini waende vijijini huko wakatafute wateja wakaweke kama ni agency, kama ni branches, chochote kile lakini wahakikishe kuwa wanazitafuta, fedha zipo, siyo za Serikali tu ndiyo fedha zao, wao watafute vyanzo vingine vya deposits.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naunga mkono hoja.