Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuchangia. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara; kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kuandaa bajeti hii. Nawapongeza sana Wabunge wa CCM kwa kutimiza wajibu wao waliotumwa na wananchi wao kwa kutimiza sababu yao ya kuchaguliwa kwa kuingia Bungeni kufanya kazi waliyotumwa na wananchi na kueleza shida za wananchi wao mbele ya Serikali, nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo kadhaa ambayo ningependa kuyazungumzia, la kwanza ni suala la VAT kwa Zanzibar na Bara. Kuna upotoshaji mkubwa sana kwamba hatua iliyochukuliwa na Serikali, hatua nzuri kabisa ya kuhakikisha kwamba bidhaa zinazozalishwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar VAT inakusanywa Zanzibar; na bidhaa zinazozalishwa Zanzibar na kuletwa Tanzania Bara VAT inakusanywa Tanzania Bara. Kuna upotoshwaji mkubwa sana unaofanywa na wenzetu kule Zanzibar kwamba hatua hiyo inaiumiza Zanzibar, si kweli, ni kunyume chake. Hatua hii inainufaisha Zanzibar, hatua hii itawaumiza wale wadanganyifu wachache, waliokuwa wanatumia utaratibu huu kujipatia kipato ambacho sio halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ambalo ningependa kulizungumzia ni ahadi ya Chama cha Mapinduzi kwenye Ilani yetu kwamba kila kijiji kitapatiwa shilingi milioni 50 kwa ajili ya uwezeshaji, ukopeshaji wa wajasiliamali. Ahadi hii ya CCM ni hatua kubwa ya kimapinduzi ya kumuondoa Mtanzania katika lindi la umaskini. Mzunguko wa shilingi milioni 50 katika kijiji ni pesa nyingi sana zitakazoleta chachu ya maendeleo pale kijijini. Serikali katika mwaka huu wa fedha kama ambavyo mmeona, imetenga shilingi bilioni 59 kama kianzio, lakini zaidi ya hapo Serikali imeunda jopo la wataalam ambalo linatengeneza utaratibu madhubuti kabisa. Utaratibu utakaozingatia uzoefu wetu huko nyuma wa mifuko mbalimbali na mafanikio ya mifuko hiyo ili tuwe na utaratibu mzuri utakaohakikisha fedha hizi zinatumika kama zilivyopangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni jambo kubwa linabidi lifanyike kwa umakini na umahiri mkubwa ili tusipoteze fursa hii adhimu katika kuwaokoa watu wetu. kwa hiyo utaratibu mzuri unaotengenezwa na Serikali utaletwa hapa Bungeni ili kabla ya kutumika na ninyi Waheshimiwa Wabunge muwe na mchango wenu katika aina ya utaratibu ambao Serikali itautumia na ikiwezekana kabisa aidha ni kwa kuleta Sheria mpya au kufanya mabadiliko ya Sheria katika Sheria ya Uwezeshaji sasa hivi. Ili fedha hizi ziwe katika msingi wa kisheria na ziweze kutumika vizuri kuliko mifuko mingine yote huko nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli kwamba zimetengwa shilingi bilioni 59, haina maana kwamba tutashindwa ndani ya miaka mitano kufanya vijiji vyote; tumeweka hizi ili tuanze na tujifunze na kadri tutakavyokuwa na utaratibu mzuri, kasi ya kupanga fedha nyingi zaidi ili tutimize ahadi hii kwa miaka mitano inakuwepo. Kwa hiyo napenda kuwahakikishiwa Waheshimiwa Wabunge na watanzania, kwamba hii ni ahadi ya CCM, hii ni ahadi ya Rais na itatimia bila shaka yoyote.
Naomba niseme kidogo jambo moja muhimu. Sisi Chama cha Mapinduzi tulipomteua Dkt. John Pombe Magufuli kuwa mgombea wetu, tulitoa statement duniani kwamba tunahitaji aina mpya ya nchi kutokana na aina ya kiongozi huyo. Kwetu sisi kumteua yeye tulitoa kauli duniani kwamba tunataka mabadiliko ya kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya kweli hayawezi kuletwa kwa hatua ndogo ndogo, mabadiliko ya kweli yanaletwa hatua kubwa na yanaletwa na uthubutu na uthubutu huo umeanza kujidhihirisha katika bajeti ya mwaka huu, tumethubutu kwamba tunaweza kukusanya shilingi trilioni 29.5; tumethubutu kwamba tunaweza kutenga asilimia 40 kati ya hizo kwa maendeleo. Unapothubutu jambo kubwa kuna watu watatia shaka, sisi wana CCM Serikali hii ni ya kwetu, Bunge hili ndio wengi, ilani ni ya kwetu, tusitetereke katika uthubutu wetu wa kukusanya shilingi bilioni 59 tumsaidie Rais tuisaidie nchi yetu kufikia malengo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa suala la hatua za kikodi hapo mbalimbali imetokea malalamiko kwamba kodi ni kubwa, kodi ni nyingi zitadhohofisha uwekezaji. Jambo hilo si la kweli kwa sababu utafiti unaonyesha mimi hapa ninayo ripoti inaitwa Tax incentive in a global perspective inasema kwamba; survey analysis shows that host country taxation and international investment incentives generally play only a limited role in determining the international pattern of FDI. Factors like market characteristics, relative production costs and resource availability explain most of the cross-country variation in FDI inflows. Transparency, simplicity, stability and certainty in the application of the tax law and in tax administration are often ranked by investors ahead of special tax incentives.
Suala siyo kiwango cha kodi, suala ni mfumo wa kodi. Kwa hiyo, miaka yote tumeaminishwa kwamba ukiweka kodi ndogo wanakuja, ukiweka kodi kubwa hawaji, dhana hiyo si ya kweli. Ukitengeneza mambo mengine vizuri zaidi ndiyo wanakuja ikiwemo uhakika wa mfumo wa kodi. Kwa hiyo, tusiwatishe wananchi na tusitishane hapa kwamba kiwango cha kodi tulichoweka kitafukuza wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ngoja nimalize kwa kusema kwamba Rais Magufuli tumempa usukani wa kuiongoza nchi yetu, lakini nchi hii ni yetu sote na sisi tunawajibu wa kumsaidia ili tufanikiwe. Rais Magufuli akifanikiwa, nchi yetu imefanikiwa sisi tusiwe kama watazamaji kwamba ngoja tumuone atafanyaje, sisi tuko naye kwenye basi hili tumsaidie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua tunazochukua nchi yetu ni sawasawa na gari nzuri aina ya benzi iliyoingia kwenye matope tunataka kuirudisha kwenye lami, hatua ya kuirudisha kwenye lami itakuwa na misukosuko, kuna wengine wataamua kushuka lakini tuendelee kuwa ndani ya gari hilo mpaka likae kwenye lami lifike safari. Maendeleo yanahitaji sacrifice, katika bajeti hii Wabunge sisi tume-sacrifice, tume-sacrifice kwa kukubali kukatwa kodi, kila mtu lazima a-sacrifice, wafanyabiashara, waendesha bodaboda, kila mmoja lazima a-sacrifice ili nchi yetu iende mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema mwaka 1961 wakati Rais Kennedy wa Marekani anaapishwa aliwaambia wa Marekani kwamba ask not what your country can do for you, but what you can do for your country. Ni wakati sasa kwa Watanzania wote kutokaa siku zote na kujiuliza nchi hii itanifanyia nini bali sisi tutaifanyia nini nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.