Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa dhati kabisa nianze kwa kukupongeza wewe mwenyewe kwa umahiri mkubwa na umakini mkubwa unaoonesha katika kusimamia shughuli za Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli umejipambanua kama ni mtaalam na mwanamke unayeweza kuhimili mikiki ndani ya Bunge, lakini unao weledi wa hali ya juu wa kuhakikisha kwamba Bunge hili linaongozwa kwa kufuata Kanuni ambazo zimewekwa na sisi Wabunge wenyewe. Naomba nikutie moyo, katika safari yoyote kuna magumu, lakini yastahimili kwa sababu Umma wa Watanzania unaamini kabisa kwamba unao uwezo wa kutusaidia kuliongoza Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi ya pekee pia kuwapongeza sana Wabunge wa Chama cha Mapinduzi. Nawapongeza sana!
Mheshimiwa Naibu Spika, watu wengi walikuwa wanadhani kwamba Wabunge hawa wa Chama cha Mapinduzi uwezo wao katika kuyachambua mambo, kuchangia michango yenye kuwawakilisha Watanzania ni mdogo, lakini katika Bunge la Bajeti la mwaka huu, Wabunge wa Chama cha Mapinduzi wameonesha wanao uwezo mkubwa sana wa kujenga hoja; wa kuwakilisha matatizo mbalimbali na mahitaji ya wananchi waliowachagua na kuamua kuwaweka wawakilishe katika maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge hawa wa Chama cha Mapinduzi wamefanya kazi kubwa ya kihistoria katika Bunge hili kwa mwaka huu na katika bajeti ya mwaka huu. Kwa hiyo, kwa kweli, naomba niwapongeze. Wameishauri Serikali, wametoa michango ambayo Serikali ikiifanyia kazi, inaweza ikatimiza vizuri Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2015. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameshiriki kikamilifu katika mchango wa Hotuba ya Bajeti ya kwamba michango yao ambayo wameotoa, kwanza kupitia Kamati za Bunge, lakini na michango ambayo wameitoa na ushauri walioutoa kupitia Kamati ya Bajeti, sisi kama Serikali tutaichukua na kuifanyia kazi ipasavyo. Nasema hivyo kwa sababu gani?
Katika bajeti ambayo tumekuwa tukiijadili ili tuipitishe leo, ingawa watu wengi wanasema kwamba Wabunge wa Chama cha Mapinduzi wamejiandaa kutokupitisha bajeti yao, jambo ambalo siyo kweli na leo watashuhudia tutakapopitisha bajeti hii! Nasema hayo kwa sababu sitaki Wabunge wa Chama cha Mapinduzi wachonganishwe na Rais wao na Serikali yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Bajeti hii ni ya kwetu sisi kama Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi na inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na tunaamini kabisa kama Serikali, haya ambayo yamechangiwa, tena na Waheshimiwa Wabunge wa Chama cha Mapinduzi, ndiyo wananchi waliyotutuma kuyafanya ndani ya Bunge la Hamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli wa jambo hili unajidhirisha katika Kanuni yako ya 94 ya Kanuni za Bunge. Kanuni hiyo ya 94 kwa faida ya Watanzania nitaisoma tu kidogo. Kanuni ya 94 inasema, “Katika Mkutano wake wa Mwezi Oktoba na Novemba kwa kila mwaka Bunge kwa siku zisizopungua tano litakaa kama Kamati ya Mipango, ili kukidhi matakwa ya Ibara ya 63(3)(c) ya Katiba kwa kujadili na kuishauri Serikali kuhusu mapendekezo ya Utekelezaji wa Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali katika mwaka wa fedha unaofuata.” (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kanuni hiyo ya 94, kazi ya Mkutano huo, Mkutano ambao ni Mkutano wa Kuishauri Serikali, itapokea na kujadili na kutoa maoni na ushauri kuhusu Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali.
Kwa hiyo, sisi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tuna miaka mitano ya kuishauri Serikali yetu na kuhakikisha tunatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatuna shaka na tutayafanya hayo yote bila wasiwasi wowote na Serikali yetu itaendelea kutekeleza matakwa ya Watanzania, bajeti moja hadi nyingine kwa kipindi chote cha miaka mitano na Watanzania wawe na amani Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tuko imara na Serikali iko imara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji wengi wamezungumza matatizo ya Sekta ya wafanyakazi na hasa katika sekta binafsi. Kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa Sheria za Kazi, kumekuwa na tatizo kubwa la wageni kufanya kazi bila vibali katika nchi yetu ya Tanzania, lakini vilevile kumekuwa na wageni ambao wanatumia ujanja ujanja tu katika kupata ajira katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote, yako marekebisho ya Kisheria tutayaleta hapa katika Bunge hili yataipa meno Serikali kupambana na waajiri wote wanaokiuka Sheria za Kazi katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Wabunge wamechangia sana kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii kwa maana ya Social Protection. Tunajua, tunajipanga kupitia upya Sheria zetu zinazosimamia mifuko ya hifadhi ya jamii ili kero ambazo zinawapata Watanzania katika sekta hiyo ziweze kushughulikiwa inavyotakiwa, lakini kubwa zaidi ni kuhakikisha tunaongeza wigo wa kuwafanya Watanzania wengi wafikiwe na suala zima la hifadhi ya jamii katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Munde na Wabunge wengine wameomba sana tuongeze fao la bodaboda katika mafao ambayo yatakuwa yanatolewa katika sekta hii ya hifadhi ya jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshakubaliana na mifuko yote kuona ni namna gani sekta binafsi, hawa vijana wetu wa bodaboda nao waingizwe katika suala zima la social protection ili waweze kupata faida ya mafao yanayotolewa na mifuko.
Mhshimiwa Naibu Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, mimi na Naibu Waziri wangu, Mheshimiwa Mavunde, tumejipanga na tutapita katika Mkoa mmoja baada ya mwingine ili kuona namna gani tunashirikiana na nyie katika suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mengine tutayajibu kimaandishi, lakini naunga mkono bajeti hii na ninampongeza sana Waziri wa Fedha na Naibu wake. Ahsante sana.