Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwamba Bunge lako Tukufu liridhie mkataba wa Kimataifa wa kudhibiti matumizi ya dawa na mbinu za kuongeza nguvu michezoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumechelewa sana kama nchi na kwa kweli nchi yetu ya Tanzania kulinganisha na nchi ambazo zimetajwa kwenye hiyo orodha ya nchi saba ni kama aibu. Naomba sana leo hii turidhie na tuingie kwenye zile nchi ambazo zipo makini kwenye hili suala. Wanamichezo wengi wa Tanzania inawezekana wameathirika kutokana na matumizi ya hizi dawa. Ingawa mkataba huu una udhaifu wa kutokutoa viwango sawa vya udhibiti wa dawa kiasi ambacho kuna baadhi ya nchi wanaruhusu matumizi ya bangi, wanaona ni sawasawa tu, lakini kwa kweli tukiingia sisi inabidi tuwe na orodha ndefu zaidi kuliko ile orodha ambayo ipo kwenye huu mkataba ili kusudi Watanzania wote wanaoshiriki michezo na Watanzania ambao wako mitaani waweze kuishi wakiwa na afya njema; tuwalinde wote siyo tuwalinde wana michezo peke yao, Kwa sababu hata waliopo mitaani kesho wanaweza wakawa wanamichezo tukiwahamasisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, ziko faida nyingi ambazo tutazipata kutokana na kutekeleza huu mkataba. Kwanza tutapata elimu; elimu ambayo kwa wana michezo na makocha wa michezo kuhusu makosa ya kutumia dawa hizo na madhara yake itasaidia sana kuweza kuokoa kundi na hasa la vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tutapunguza, tutazuia usafirishaji wa biashara ya vifaa na dawa ambazo zimezuiliwa, pia tutadhibiti matumizi kwa kuboresha njia mbalimbali za uchunguzi na vipimo kwenye maabara na inawezekana na sisi tukapata maabara yenye ithibati ya Kimataifa ya kuchunguza na kupima matumizi kama hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Kamati ambayo Mheshimiwa Hafidh ameipendekeza iwe inatoa adhabu kali sana kwa watakaogundulika kutumia hizo dawa, kwa sababu bila adhabu kali matumizi ya dawa hizo yataendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, ni wajibu wa Serikali na wadau kufadhili na kusimamia mfumo wa ufuatiliaji na tathmini ambao utahakikisha utekelezaji sahihi wa kanuni zilizopo kwenye mkataba huo ili kuhakikisha kwamba matumizi ya dawa zote zilizoainishwa na ambazo sisi kama Taifa tutaziongeza yanadhibitiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili la Bunge linaweza kusaidia nchi yetu kupata mafanikio kimichezo na kuondokana na sifa ya kuwa kichwa cha mwendawazimu, kwa sababu baadhi ya dawa kama bangi na mirungi na hata dawa za kusisimua misuli kwa wale ambao wanapenda sana kucheza michezo ile mingine ya usiku, nadhani zinaweza kusababisha afya kuathirika na nguvu zao kimichezo kupungua na viwango vyao vya michezo kupungua. Kwa hiyo, inabidi tuchukue hatua kali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nimalizie mchango wangu kwa kusema kwamba, kama nchi hizi hatua kali ambazo tutazichukua lazima ziandikwe kwenye sheria, kama hazijaandikwa kwenye sheria zikabaki tu kwenye kanuni ndogo ndogo sijui za Vyama vya Michezo tutakosa nguvu ya kuweza kutekeleza. Kwa hiyo, inatakiwa ziingie kwenye sheria zetu kama nchi, Mheshimiwa Waziri wa Sheria ashiriki kuhakikisha kwamba sheria inatungwa ambayo itatoa udhibiti na makosa ya matumizi ya hizo dawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini nasema hivyo? Wapo wachezaji wengi sana wamecheza mpira kwa muda mfupi na wakaathirika; wamecheza mpira mwaka mmoja mtu anakuwa nyoronyoro kabisa. Nasikia pale Kariakoo kuna matatizo makubwa sana ndiyo maana wachezaji wengi wa Yanga huwa wanacheza kwa muda mfupi mpira, sasa hiyo inatakiwa ifuataliwe, siyo wote ni baadhi yao na hata wachezaji wa Simba!
Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta mchezaji mzuri anatoka mkoani akifika pale mjini mwaka mmoja, miwili tayari amepoteza kiwango chake, angalau wale ambao huwa wanatoka katika nchi za nje kidogo wanajua mantiki ya hizo dawa; huwa wanacheza kwa muda mrefu sana, kwa mfano yule Mkongo, anaitwa nani yule, yule wa Yanga ana umri wa miaka karibu 40 lakini anacheza mpira mpaka sasa hivi. Mwenzangu ameonesha wasiwasi kwamba huenda inawezekana labda anatumia lakini naamini yule hatumii ndiyo maana amecheza mpira kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mifano ya wachezaji kama Joseph Kaniki ambaye alikamatwa na dawa za kulevya kule Ethiopia na wachezaji ngumi ambao walisafirishwa na marehemu Shaban Mwintanga ambao walikamatwa kule Mauritius ni mifano ya aibu ambayo hatutegemei tuendelee kuipata katika nchi yetu ili kusudi hata sisi tujenge jina kwenye nchi nyingine kwamba sisi ni nchi ambayo ipo makini. Ni lazima uchunguzi wa kina uwe unafanywa kwa mfano kama timu inasafiri kwenda nje ya nchi, kabla hawajatoka nje ya nchi uchunguzi ufanywe wa kina kwamba hawana dawa na wanaporudi vile vile uchunguzi ufanyike wa kina kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii. Ahsante sana.