Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Kwa kweli kazi uliyoifanya umeliletea heshima Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nieleze tu eneo moja dogo. Kwa kawaida wenzetu wa upande wa pili wanapochangia, hata wakisema maneno mabaya kiasi gani upande huu wanakaa kimya. Tunapochangia sisi wanaanza kutuzomea hata michango yetu haisikiki. Naomba na hili nalo tulidhibiti. Tukilidhibiti hilo Bunge hili litakuwa zuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Dkt. Philip Mpango kwa mipango yake kabambe na hasa katika miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujibu maswali machache ambayo Waheshimiwa Wabunge wamechangia. Moja, kuhusiana na bandari bubu. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Serikali imejipanga kudhibiti bandari bubu. Kama mtakumbuka hivi karibuni nilijibu swali moja la Mheshimiwa Mbunge wa Mtwara; kwamba tuna vikao vinavyoshirikisha Serikali za Mwambao pamoja na Zanzibar kuhakikisha tunazitambua bandari zote bubu na hatimaye kudhibiti mapato yanayopotea kupitia hizo bandari bubu. Tutaendeleza na katika Maziwa Makuu. Kazi hiyo tutaifanya kwa kasi, mwaka huu ujao wa fedha hiyo kazi lazima ikamilike.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee TTCL. TTCL naomba niwaote wasiwasi. Tulivyojipanga Wizarani na ndani ya Serikali TTCL mnayoiona sasa, TTCL mliyoizoea kuanzia mwezi wa Tisa itakuwa ni TTCL tofauti kabisa. TTCL hii itaingia kwenye kusambaza teknolojia za simu na mitandao ya 2G, 3G na 4G kuanzia Dar es Salaam na mikoa mingine tisa mpaka mwezi Desemba mwaka huu na miaka inayofuata tutasambaza Tanzania nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hilo, na kwa sababu Mkongo wa Taifa uko chini yetu hatutakuwa na mshindani. Tutashindana kibiashara na sisi tutaingia katika mashindano ya kutoa vifurushi, kwa sasa hatujaanza kutoa. Nawahakikishia TTCL hii itakuwa tofauti kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Fedha alivyoniahidi, madeni yote ya TTCL yatalipwa na baada ya hapo tunaiwezesha TTCL si kwa mtaji, kwa namna tulivyojipanga sasa wala hawahitaji mtaji tena, wanaingia kwenye biashara za ushindani na tuna makamanda pale. Baadhi tutawaondoa ili tuhakikishe kile tunachokikusudia katika TTCL kinapatikana katika muda mfupi na hatimaye Serikali nzima itatumia huduma za TTCL.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee TEMESA nayo. Nayo tuna mipango kabambe ya kuibadilisha. Zile tabia za ajabu ajabu za kudhani TEMESA haina mwenyewe zitakwisha. Masuala ya kuvuruga vuruga, mtu analeta gari zima linatoka bovu mwisho wao ni mwaka huu, baada ya mwaka huu hali itabadilika na Serikali itapunguza matumizi kwa kutumia huduma za TEMESA.
Mheshimiwa Naibu Spika, TRL na RAHCO. Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea kuhusu kuunganisha TRL na RAHCO. Wametoa maelezo marefu, Serikali imeyachukua. Lakini, upande wa pili hawauongelei sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa tuna mpango wa kujenga reli kutoka Tanga hadi Musoma, tuna mpango wa kujenga reli kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay, tuna reli ya TAZARA, tuna reli ya Kati na matawi yake yote. Hapa ni wajibu wa Serikali na ushauri wenu tutauchukua, kuamua je miundombinu hiyo ya reli zote isimamiwe na TRL peke yake? Kuna faida lakini vile vile kuna hasara zake.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia upande wa hasara, ujenzi wa miundombinu unahitaji fedha nyingi sana na fedha hizo sehemu kubwa tutazipata kupitia mikopo. Mikopo hii ikikaa TRL kazi yao ya kutoa huduma inaweza ikakwamishwa kutokana na ukubwa wa madeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunadhani TRL ifanye kazi ya kutoa huduma halafu RAHCO kiwe ndicho chombo cha Serikali cha kuwekeza na tutakopa mikopo yote itaingia RAHCO ili TRL iweze ku-operate kibiashara. Kama nilivyosema, kupanga ni kuchagua, tumesikia maoni yenu, tutayajadili ndani ya Serikali na hatimaye uamuzi utatoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, ATCL. Kuna baadhi walichangia kuhusu ATCL. Tutafanya kazi ya kuirekebisha ATCL, tutafanya kazi ya kuibadilisha ATCL. Tatizo kubwa la ATCL liko kwenye mindset. Tutafanya kazi ya kuondoa matatizo ya kwenye mindset ili tuwapate watu ambao wana fikra za kibiashara waweze kutusaidia tuweze kuinua na kuisimamisha ATCL iweze kutoa huduma za usafiri. Kwa kweli, ndege nyingi zinatumia sana fedha za Serikali na fedha za Serikali zinakwenda nje na tunalazimisha kulipa hela nyingi sana kwa gharama za usafiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiweza kuimarisha ATCL kwanza tutatoa ushindani kwa nchi, lakini vile vile tuta-save fedha nyingi sana zinazopotea sasa kutokana na gharama ambazo hawa wenzetu wachache wanajipangia kwa namna wanavyotaka wao. Naomba tushirikiane tuifanye kazi ya kuibadilisha ATCL iweze kutusaidia kwa namna ambavyo tunataka.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda nirudi tena kwenye TTCL. TTCL mnafahamu kwamba tulikuwa na partnership na Bharti Airtel. Hivi sasa tunaongelea tutaanza mwezi wa Tisa kwa sababu kwanza tunalitatua hili tatizo la Bharti Airtel na tuna uhakika itakapofika mwezi wa Saba tatizo hili litakuwa limekwisha, TTCL itamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, ndipo tutakapoanza kuingiza hiyo mitaji na mitaji haitoki Serikalini, inatoka kama mkopo, TIB anafanya Syndication na makampuni yanayotoa Service kama vile Alcatel, ZT ya Japani pamoja na Huawei. Watu wa TIB wanatusaidia kufanya Syndication na ndiyo mtaji tutakauotumia kuibadilisha TTCL.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na hayo machache na nakuomba sana tena sana utusaidie kulirekebisha Bunge hili. Uwezo unao, umeanza vizuri na naamini hili eneo dogo lililobakia tukilikamilisha kulirekebisha, Bunge hili litakuwa na heshima inayostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja na ahsante sana kwa kunipa fursa.