Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mussa Azzan Zungu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ilala

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi, lakini kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Vilevile nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya, nitoe pongezi kwa Mawaziri wake kwa kazi nzuri sasa wanayoifanya na kuwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Ilala kwa kunirudisha tena kwenye Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la ujangili likiendelea litapunguza mapato kwenye Taifa letu. Mimi nilikuwa naomba kutoa ushauri and I stand to be corrected.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa majangili ambao wako katika mbunga hizi, wanajichanganya na wawindaji halali, hivi Serikali ikipiga marufuku uwindaji kwa kipindi cha miezi mitatu, hakuna mtu yoyote kuingia na silaha kwenye mbuga hizi; na vyombo vya ulinzi vikafanya operation maalumu ya kusaka majangili hawa; nafikiri inaweza ikasaidia kupunguza tatizo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri wa Maliasili na Utalii, pembe za nduvu ambazo ziko kwenye bohari, wazifanyie audit na wazifanyie DNA. Iko hatari kuwa takwimu za pembe za nduvu ziko sahihi, lakini ndovu zile ambazo ziko kwenye magodauni haya zisiwe sahihi. Inawezekana pembe nyingine wala hazitolewi kwenye mbuga, zinatolewa kwenye ma-godown haya ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri kwa taarifa yake na Mapendekezo ya Mpango wake. Ametoa taarifa Bungeni kwamba gharama za kujenga reli ya kati itafika kama bilioni saba, fedha za Kimarekani, takribani kama shilingi trilioni 15. Fedha hizi ni nyingi sana na tusijitie hofu kwa gharama kubwa kama hii ili reli hii isijengwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Zambia wamejenga reli yao kilometa 2,200 na madaraja 48, kwa one billion US Dollars. Sisemi train ya Zambia ipo sawasawa na ya kwetu, lakini naomba design cost zipatikane ili tujue gharama sahihi ya reli hii ili iweze kujengwa, iweze ku-support bandari yetu na bandari nyingine ili uchumi wa Taifa yetu uweze kukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye Mpango, kuna Mpango wa kununua ndege. Kununua ndege na kujenga hii reli, Serikali haiwezi. Serikali ijikite kwenye mipango ya huduma za afya, elimu na kilimo. Miradi mikubwa kama hii iachiwe sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta binafsi ipo tayari kufanya. Sioni kwa nini Serikali miaka yote haitaki kushirikisha sekta binafsi ikajipunguzia gharama za kutumia fedha za umma kujenga reli hii au kununua ndege hizi na badala yake ikatumia kwenye mipango mingine. Sekta binafsi ikifanya shughuli hizi, itapunguza hata tatizo la watu kula rushwa kwa fedha hizi za umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndege hizi ambazo Serikali inataka kununua; ushauri wa kwa Serikali, wasafishe vitabu vya ATC ili wakaribishe sekta binafsi iendeshe na ilete ndege nchini mwetu. Watanzania wanataka usafiri. Ukienda Marekani, hakuna Shirika la Ndege la Serikali. Sioni sababu kwa nini Serikali ijiingize kwenye miradi mikubwa na baadaye ikaingia kwenye hasara sababu ya kutokuwa na watendaji waaminifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa kuleta elimu bure Tanzania. Sasa hivi wazazi wengi sana wanapeleka watoto wao kusoma na kujiandikisha. Zipo changamoto, mwanzo ni mgumu. Fedha haziwezi kwenda kwenye shule zote kwa muda mfupi sana ambao umewekwa, lakini changamoto hizi tukiipa muda Serikali, itatafuta njia ya kuhakikisha agizo hili la Rais linatekelezwa kwa ufanisi na Watanzania wakapata win-win situation wao na Serikali yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo issue ya Watanzania kushindwa kuwa na viwanja kutokana na Serikali kutokuwa na mipango madhubuti ya ku-ring fence viwanja maalum vya watu wenye kipato cha chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Malaysia, Serikali imeweka sheria kabisa ya kuweka viwanja na madhumuni yake ni kusaidia watu wao wa kipato cha chini. Viwanja hivi vinawekewa sheria kwamba yeyote mwenye kipato cha kati, haruhusiwi kuingia kwenye viwanja hivyo. Serikali ikijenga nyumba katika viwanja hivyo, watu wenye kipato cha kawaida hawaruhusiwi kuingia au kumiliki nyumba hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano, maana yake watu kama sisi Wabunge ambao wana uwezo wa kukopa na kujenga, hawataruhusiwa kuchukua viwanja kama hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo inasababisha watu kujenga kwenye mabonde. Hakuna mtu anayetaka watu wake wajenge kwenye mabonde wapate matatizo ya mafuriko, inasikitisha sana, lakini hawana njia nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa kuna mradi wa World Bank kwenye maeneo haya ya mabonde ambayo watu wanaishi. Ninachokiomba, taarifa ambazo ziko kwenye mitandao, World Bank wanataka kufanya huu mradi lakini wameweka component ya fidia. Kama hizi fedha zimefika, fidia hii ilipwe tunusuru maisha ya hawa watu. Tusiingie tu na mazoezi makubwa ya kuvunja bila kutazama na mustakabali wa wananchi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sitetei wananchi wakae katika maji, wala msinielewe vibaya; wanataka wao waendelee kukaa katika mabonde maeneo ambayo ni hatarishi; lakini taarifa za wao kupewa viwanja Mabwepande, siyo kweli. Nalizungumza hili na ninazo takwimu. Wananchi wa Mchikichini ambao walikumbwa na mafuriko mwaka 2011 walikuwa 4,200; viwanja allocation ilitoka kwa wananchi 80 tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna taarifa kwamba Mawaziri hawa wanapewa na Mamlaka ya Mkoa kuambiwa kuna watu wanakimbia Mabwebande au wameuza Mabwepande, siyo kweli! Kama kuna mtu ameuza kiwanja chake Mwabwepande watuletee taarifa na majina ya watu waliouza na waliokimbia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie, kuna watu wako tayari kuliboresha bonde hiliā€¦
MWENYEKITI: Tunakushukuru kwa mchango wako.