Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi nitoe mchango wangu katika Wizara hii muhimu ambayo ni ya Mipango na Fedha. Nichukue fursa hii pia kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha kufika siku ya leo. Pia nitakuwa mnyimi wa fadhila kama sijampongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Mpango na timu yake kwa hotuba nzuri na mipango ambayo tunaiona Tanzania mpya iko mbioni kuja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nichukue fursa hii kukupongeza wewe binafsi. Nakupongeza kwa umahiri wako mkubwa, kwa weledi mkubwa na unavyoendesha Bunge hili la Kumi la Moja. Usitishike na hivi vitisho kutoka upande wa pili, simamia hapo kwa sababu ya kutenda haki. Walizoea kupindisha sheria, sasa wamekutana na nguli wa sheria ambaye ni wewe ndio maana wanagonga ukuta. Usivunjike moyo, sisi tuko nyuma yako. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nijielekeze katika kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii hasa kwenye Benki ya Kilimo kwa sababu kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa hili. Serikali kwa kuliona hilo walianzisha Benki mahsusi ya Kilimo na Bunge hili la Kumi ambalo sisi hatukuwepo lakini tulikuwa tunasoma kwenye magazeti na taarifa mbalimbali lilipitisha sheria ya Serikali kuweka mtaji wa kutosha katika benki ile ili kutatua changamoto za wakulima wa nchi hii. Kwa sababu tatizo kubwa la nchi hii, sekta kubwa inayoajiri watu wengi ambayo ni kilimo imekuwa haikopesheki na niipongeze Serikali kwa kuliona hilo kwa kuanzisha benki hii. Walitenga zaidi ya shilingi bilioni 300 iwe kwenye Benki ya Kilimo, lakini mpaka sasa nasikitika Serikali wamepeleka shilingi bilioni 60 tu. Hizi shilingi bilioni 60 hazitoshi kutimiza malengo na mipango ya Serikali iliyopanga kwa ajili ya kukwamua Watanzania walio wengi waliojiajiri katika sekta ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili limekuwa ni kubwa sasa matokeo yake benki hii badala ya kujielekeza katika lengo kuu la kuendeleza sekta ya kilimo hasa zile skimu za umwagiliaji na kuwakopesha wakulima, wanafanya kazi kama za benki za biashara, kutoa mikopo ya muda mfupi kwa sababu wanaogopa kupata risk kubwa. Wanaweza kutoa mikopo ya muda mrefu na pesa ikazama na wakakinzana na masharti ya Benki Kuu ya mtaji unaohitajika. Kwa dhamira hiyohiyo ambayo Serikali mliiona mwanzoni na mipango mizuri iliyokuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hii benki iongezewe fedha ili iweze kujitanua na kuwawezesha wakulima wengi kufaidika wakiwepo na sisi huku wa mikoani katika Jimbo langu la Morogoro Kusini Mashariki na Tanzania kwa ujumla, hii benki ndio mkombozi wa mkulima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ikiiwezesha benki hii inaweza kufungua matawi yake na kuongeza rasilimali watu. Kwa sasa hivi ule mtaji waliopewa hawawezi kujitanua zaidi ya kuwa Dar es Salaam ambapo ndiyo makao makuu, lakini kama mnavyojua Dar es Salaam siyo wadau wakubwa sana wa kilimo, kilimo kiko mikoani, Morogoro na sehemu nyingine. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali yangu iongeze mtaji katika benki hii ili lengo na kusudio lililokusudiwa liweze kutimia.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili nijielekeze katika Tanzania Commodity Exchange. Ni wazo zuri kwa sababu utakuwa ndiyo muarobaini wa soko la uhakika la bidhaa zetu za kilimo hususan kwa wakulima wa Tanzania. Kwa sababu ni soko ambalo litatoa haki kwa wadau wote wa soko hili kuanzia mkulima, madalali, wafanyabiashara, mawakala lakini hata na wanunuzi wenyewe. Pia kutakuwa na uhakika wa ubora ambao unajulikana kwa sababu mambo yataenda kisheria na kimtandao, hawezi mtu yeyote kudanganywa, bei itakuwa wazi lakini hata na ubora utajulikana, ule udanganyifu mdogomdogo utaondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu tu katika hili na niiombe Serikali kwa sababu katika utaratibu wa soko hili miongoni mwa wadau wakubwa watakuwa wale madalali wa hilo soko, madalali wa wanunuzi na wa wauzaji. Katika kitabu cha hotuba nimesoma anasema mpaka sasa hivi kuna makampuni matano ambayo yameshajiorodhesha katika soko hili. Kwa hiyo, niombe wakati anakuja kujumuisha angetutajia angalau makampuni haya ni yapi ili tuwe na uelewa mpana zaidi na tuone ni makampuni yale yale ya kiujanja ujanja yameshakamata fursa au sasa ni makampuni ya ukweli yako kwa ajili ya kumkomboa mkulima halisi wa Tanzania?
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ni pana sana na imeajiri watu wengi kwa maana ya wafanyabiashara wadogo, wafanyabiashara wa kati, mawakala, madalali, ajira zao kubwa ziko hapa. Kwa hiyo, naomba kuishauri Serikali pamoja na kwamba tunaenda kwenye utaratibu huu wa soko ambao ni mzuri sasa makundi haya ni vizuri tukayatambua katika ushirika wao mbalimbali. Kwa mfano pale Dar es Salaam kuna Chama cha Madalali cha Mazao ya Mahindi na Ufuta lakini Morogoro pia viko vyama vya madalali na mikoa mingi vipo. Kwa sababu mitaji yao ni midogo ni vizuri tukawatambua kisheria kwenye umoja wao huo tukaweka utaratibu wakaingia kwenye soko hili nao wakatumika kama ndio madalali wa wakulima au wa wazalishaji. Badala ya kuwaacha nje tukaachia makampuni makubwa ndiyo yashike kazi hiyo basi tujue tutakuwa na kundi kubwa la vijana wa Kitanzania watakosa ajira jambo ambalo ni hatari. Sisi lengo letu kubwa ni kutengeneza ajira kwa ajili ya kuongeza vipato kwa wananchi wetu wengi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu katika taratibu huu, Wizara hii ivitambue vikundi vyote au umoja wowote wa madalali Tanzania nzima. Kwa sababu kwanza itasaidia sana wakitambuliwa kisheria na kupewa leseni inaweza kuwa tax base nyingine kwa sababu nafahamu wanapata mapato makubwa hawa madalali wa mikoa mbalimbali. Suala la udalali mtu akienda kununua atatumia dalali na akiuza atatumia dalali. Wakitambuliwa kisheria na mapato yao yakijulikana watasaidia kuchangia katika pato la Taifa kwa maana ya kulipa kodi na kila kitu. Pia kama Serikali mkawatengenezea fursa ya kushiriki katika huu utaratibu mpya unaokuja ili tusiliache kundi kubwa nyuma baadaye tukaenda wachache. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ambalo siyo kwa sababu ya umuhimu, hii Wizara ndiyo Wizara nyeti inayogawa mafungu ya fedha. Sisi kama Bunge hapa tunapitisha bajeti lakini kuna changamoto kubwa pesa haziendi kama tulivyopitisha na pia hazifiki kwa wakati. Nimuombe Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango, ni mpya kwenye Wizara hii na ndiyo maana sasa hivi hatuwezi kuchangia sana tunampa nafasi, changamoto zilizotokea huko nyuma tunaomba uzirekebishe ili pesa hizi tunazopitisha zifike kwa wakati na zifike kama tulivyopitisha ili zile shughuli za maendeleo tulizopanga katika Majimbo yetu na Wilayani kwetu ziende kama zilivyopangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano mmoja tu, suala la MKUKUTA katika Halmashauri yangu ya Morogoro Vijijini mwaka wa tatu huu haijafika hata senti tano. Hata ile miradi ambayo ilianzishwa imeishia palepale badala yake tumeelekeza nguvu kwamba wananchi wajichangie, wameshajichangisha tumeshamaliza vyumba vya madarasa zaidi ya miaka mitatu lakini mafungu hayapo. Kwa hiyo, nimuombe kwa niaba ya Serikali hiyo basi walete haya mafungu ili tuweze kumalizia miradi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja kwa 100% na nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.