Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na afya njema kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua nafasi hii ya kipekee kama wenzangu walivyotangulia kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wake madhubuti na makini unaoendelea kugusa sio tu Watanzania bali mfano wa kuigwa katika nchi na Bara zima la Afrika na dunia kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumpongeza kipekee Mheshimiwa Balozi Dkt. Agustino Philip Mahiga, Waziri wangu wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa uongozi makini na kuhakikisha tunapata ufanisi mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara anayoiongoza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uongozi wake ndani ya Bunge hili. Aidha, napenda kuwapongeza sana Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa namna wanavyoliongoza Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Andrew John Chenge; Mheshimiwa Mussa Zungu Azzan na Mheshimiwa Najma Murtaza, wewe Mheshimiwa Giga kwa kuchaguliwa kuwa Wenyeviti na kwa namna mlivyoonesha uwezo mkubwa wa kuliongoza Bunge hili katika kipindi hiki. Pia nawashukuru sana Wabunge wenzangu kwa ushirikiano wao wanaoendelea kunipa. Nawaombea kila la kheri katika utekelezaji wa majukumu yao hapa Bungeni na kwenye majimbo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwa namna ya pekee kuwashukuru sana wananchi wenzangu na wanawake wote wa Mkoa wa Njombe na kwa kipekee Jumuiya ya Wanawake Tanzania, Mkoa wa Njombe kwa kunichagua kwa kura nyingi kuwa Mbunge wa Viti Maalum katika Mkoa huo na kwa imani kubwa walionipa na wanaoendelea kuonesha kwangu. Nitaendelea kuwa nao karibu na kushirikiana nao kuleta maendeleo makubwa zaidi na naahidi kuwa sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru sana familia yangu ikiongozwa na mume wangu mpendwa Dkt. George Yesse Mrikaria kwa uvumilivu wao kwangu na kwa namna inavyonisaidia na kuniunga mkono katika majukumu yangu. Aidha, shukrani za dhati ziende kwa Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, viongozi, watendaji, wasaidizi wangu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa ushauri na msaada wao katika utekelezaji wa majukumu yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo sasa nianze kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Kwanza nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii. Ni dhahiri kwamba michango yao itatusaidia sana katika kufanikisha shughuli za Wizara na kuimarisha ufanisi wa watendaji. Tunashukuru michango yote iliyoletwa kwa maandishi, ni michango karibu ya watu 50 na wale ambao wamezungumza moja kwa moja tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nianze kujibu hoja za mzungumzaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani na nitazungumzia baadhi ya vitu na vingine Mheshimiwa Waziri wangu atamalizia. Kwenye suala lililozungumzwa kwamba ni chombo gani hasa kinachotumika kama kiunganishi kati ya Balozi zetu na Wizara nyingine ili Mabalozi hawa waweze kujua na kujifunza mambo mengi mazuri yanayofanywa katika Wizara mbalimbali na lile la namna gani wananchi wanaweza kupata ripoti za Balozi mbalimbali kwa njia rahisi ili wahamasike katika kutafuta fursa za kiuchumi katika nchi hizo zenye uwakilishi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu ni fupi, hili ni jukumu la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na wao kazi yao kubwa ni kuratibu shughuli hizo. Hata Waraka unaolalamikiwa na Waziri Kivuli wa Wizara yangu unatokana na wajibu wa Wizara yetu hii lakini unalenga na unasimamia sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la utaratibu uliotolewa na Wizara kuwataka Mabalozi kutoa taarifa Wizarani na kadhalika na kadhalika ambazo zimezungumzwa katika Kambi ya Upinzani kwenye taarifa yao, naomba nitoe maelezo haya kwa kirefu ili yaeleweke ili baadaye labda kila mtu apate ufahamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu unaolalamikiwa na Kambi Rasmi ya Upinzani unarejea Waraka wa Rais Namba Mbili (2) ambao ulitolewa mwaka 1964 na unatoa muongozo kuhusu utaratibu wa mawasiliano kati ya Taasisi za Serikali na wanadiplomasia wanaoziwakilisha nchi zao na Mashirika ya Kimataifa hapa nchini. Utaratibu huo si mpya na wala haujaanza kutumika Awamu hii ya Tano ya uongozi wa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli bali umekuwa ukitumika tangu mwaka huo 1964 kwa lengo la kuwa na utaratibu mahususi unaotakiwa kufuatwa ili kuweka mtiririko mzuri wa Mawasiliano baina ya Serikali na Taasisi tajwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya waraka huo, Mabalozi hawatakiwi kuomba ruhusua kama ilivyoelezwa na Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani bali hutakiwa kutoa taarifa ya maombi yao ya miadi au safari za nje za kituo chao cha kazi, yaani kama ni Dar es salaam, ili kutoa fursa ya Wizara ya Mambo ya Nje ambao ndiyo wasimamizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwa na kumbukumbu kuhusu miadi hiyo na kuratibu. Uratibu huo haupo Tanzania peke yake, bali hufanyika katika nchi zote duniani na kuwawezesha Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa kuwafikia kwa wepesi viongozi na taasisi mbalimbali za kiserikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile kuviwezesha vyombo vya Ulinzi na usalama kuhakikisha usalama wa Mabalozi hao katika nchi hiyo husika wawapo mikoani au sehemu nyingine yoyote. Hivyo Waraka huo wa Kibalozi, unatajwa katika maelezo ya Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani katika Wizara yetu ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa Wizara kuwakumbusha Mabalozi na taasisi za Serikali kuhusu wajibu wao katika Mawasiliano husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu waraka huo ulipotolewa, Mabalozi wameendelea kufanya kazi zao vizuri kama kawaida na hatujawahi sisi kama Wizara kupata malalamiko yoyote kutoka kwa Mabalozi hao wala taasisi hizo; na wala hawajawahi kuhamishwa kwa sababu waraka huo ni sehemu tu ya utekelezaji wa sheria ile inayohusiana na mahusiano ya kidiplomasia iliyotungwa mwaka 1963. Hivyo napenda kutoa wito kwa watumishi wote wa Serikali pamoja na taasisi zake, Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa waendelee kuzingatia waraka huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea, katika taarifa ile ya Kambi ya Upinzani, ilitumia tu sehemu moja na ikasema tu na ikataja article ile ya 41, lakini nataka niwasomee hapa, naomba kwa ruhusa yako Mheshimiwa Mwenyekiti, niweze kutoa quotation hiyo. Katika section ya pili ya article hiyo ya 41 inasema:
“All officials business with receiving state in entrusted to the mission of the same state shall be conducted with or through the minister of foreign affairs of the receiving state or such other ministry as be agreed. Kwa hiyo, waraka ule ni supplement tu ya hii sheria ambayo hata wao wanaitambua. Niliona nitoe maelezo haya yaeleweke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze suala la remitence kutoka diaspora. Ni kweli hatuna hesabu kamili ya remitence zote zinazofanywa lakini katika taasisi ambazo sisi tumezifanyia kazi, taasisi kama ya CRDB, Bank ya Watu wa Zanzibar, Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF) na Mfuko wa Mitaji (UTT), tunachojua ni kwamba kwa mchango wa diaspora so far kuanzia mwaka wa 2013 mpaka 2015 katika Taasisi hizo tunajua kwamba diaspora wamechangia karibu milioni 26.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kujibu hilo, niende kwenye suala la visa kutoka nje ya Tanzania. Kuna suala ambalo limeulizwa kwamba Uingereza wanatoa visa zao kule Pretoria-South Africa na Canada wanatolea Nairobi, Australia wanatolea Nairobi na kadhalika na kadhalika. Tunasema hivi, ili kubana matumizi, nchi mbalimbali duniani zikiwemo zilizotajwa hapo juu, zimeweka mfumo wa kuweza ku-centralize huduma zao za utoaji wa visa na hizi zinaratibiwa kutokana na wao kwa matakwa yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi kama Tanzania hatuwezi kuwalazimisha wao kufuata utaratibu wa kwetu ila tunaweza tu kushauriana nao na kuwashawishi. Kwa hiyo, ule mtindo wa kutoa visa labda kwa Watanzania kupata visa zao kupitia South Africa, sisi tunajua kwamba hawaendi lakini wana process wao wenyewe na wao wameamua kutolea visa South Africa hatuwezi kuwalazimisha. Hata hivyo, tuahidi tu, kwa sababu sisi ni Wizara ambayo inajali mahusiano na taratibu, tutajaribu kuendelea kuwashawishi ili jambo hilo lifanywe kama lilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ushiriki wa Ubalozi wetu Washington katika msiba wa Mtanzania aliyeuawa Houston-Marekani Marehemu Andrew Sanga. Ubalozi ulishiriki kwa kuhudhuria ibada na kutoa rambirambi kupitia Jumuiya yetu ya Watanzania wanaoishi Houston. Aidha, Ubalozi uliwakilishwa na Afisa wetu wa Ubalozi kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kutokuwepo kwa Balozi kwa Washington katika msiba ule siku ile ni kwamba Balozi huyo alikuwa anamwakilisha Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli katika Kongamano la Watanzania lililofanyika Dallas-Marekani. Hata hivyo, kama nilivyosema kwamba, Balozi alimtuma Afisa wa Ubalozi kumwakilisha katika msiba huo, kwa hiyo nataka kuweka taarifa hii wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vigezo vya kufungua Ubalozi. Niseme tu kwamba, kwa mujibu wa article namba 5 ya Mkataba wa Vienna kuhusu mahusiano ya Ki-consular ya mwaka 1963, ziko sababu kadhaa zinazoweza kuchochea kufunguliwa kwa Ofisi za Ubalozi. Baadhi ya sababu ni kama ifuatavyo:-
(i) Kuongezeka kwa wigo wa mahusiano kati ya Tanzania na nchi husika;
(ii) Kuongeza wigo wa kuendeleza mahusiano ya Kibiashara, Kiuchumi, Kiutamaduni; na
(iii) Ni kuwa na fursa ya kuwahudumia Watanzania waliopo katika nchi hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoona kwamba katika nchi hizo tunao Watanzania kwa hiyo, hiyo inatusukuma sisi kuhakikisha kwamba tunaweka Ubalozi sehemu husika na vile vile kuwa na Wawakilishi katika nchi husika ili kukuza uhusiano wetu na nchi inayohusika. Ili kwenda sambamba na vigezo hivyo, kwa kuwa hatuwezi kufungua Balozi kila sehemu na uwezo kama mlivyojua kwamba bajeti ni ndogo; lakini kwa mwaka huu na katika mpangilio na Mkakati wa Wizara tumeweka katika balozi ambazo tunategemea labda tutazifungua tukipata pesa baada ya kufungua ile ya Quwait mwaka huu. Katika mkakati huo, tukipata pesa, tumepanga kufungua Ubalozi Qatar, Uturuki, Korea ya Kusini, Israel, Namibia na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali inavyowashughulikia Raia wa Tanzania waliopo Magerezani. Wakati kuna swali ambalo limeuliza kuhusu Maafisa Uhamiaji wanafanya kazi gani katika Balozi zetu? Moja ya kazi ambazo wanazifanya ni kuhakikisha kwamba wanaweza kwenda kuwatembelea wafungwa hao wanapokuwa gerezani na kujua matatizo waliyokuwa nayo na kutoa utatuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Balozi za Tanzania zina utaratibu wa kuwatembelea raia wa Tanzania waliopo gerezani. Utaratibu huo unafanywa kwenye balozi zetu za China, India, Japan na sehemu nyingine ambazo tunazo balozi zetu. Pale ambapo tunasikia na tunapogundua kwamba tunao Watanzania kwenye magereza hayo hufanya hivyo kwa sababu ni moja ya wajibu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wafungwa kuja kutumikia vifungo nyumbani, utaratibu huo upo. Nchi yetu imeingia kwenye mikataba ya kubadilishana wafungwa, lakini vilevile katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, tunayo sheria ambayo tumekubaliana kwamba inapotokea kuna mfungwa anayetoka Uganda, Kenya, Burundi na Rwanda na sasa Sudan ya Kusini basi tuna utaratibu wa kubadilishana na practice hiyo ipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye hoja za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Kuhusu hoja kutokana na mwelekeo wa dunia ulivyo hivi sasa kuhusu uhusiano na ushirikiano wa Kimataifa, Serikali kupitia Chuo cha Kidiplomasia, iweke mitaala ambayo itazalisha wataalam wengi wa fani ya diplomasia kiuchumi. Aidha, Chuo kitawanye na kujipanua kuandaa mafunzo ya Kidiplomasia. Maelezo yetu ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Serikali kuanzisha Sera ya Mambo ya Nje inayotilia msisitizo wa Kidiplomasia ya Kiuchumi, Chuo kimeandaa mitaala maalum kufundisha Diplomasia ya Uchumi na tayari Chuo chetu kinatoa shahada ya Uzamili katika Diplomasia ya Uchumi; na Maafisa wa mambo ya nje wote walioko Tanzania na wale ambao wako katika balozi zetu nje ya nchi, wote wamepata mafunzo hayo; na moja ya kigezo ambacho kinamfanya aweze kutoka nje ya Tanzania ni pamoja na kupata mafunzo hayo. Aidha, mipango ya baadaye ni kuongeza mafunzo katika ngazi ya Cheti, Stashahada na Shahada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali kutoa fedha kwenye balozi zetu nje ili kueneza sera ya diplomasia ya uchumi ambayo itaongeza uwekezaji na Watalii. Fedha za matumizi Ubalozini hutengwa kulingana na ukomo wa bajeti na hutolewa na Hazina kwa mwaka hadi mwaka. Tutaendelea kuwashawishi Bunge hili pamoja na Hazina kuhakikisha kwamba ukomo huo wa bajeti unakuwa ni mkubwa ili kuhakikisha kwamba tunawawezesha vijana wetu au watumishi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali kuelekeza fedha ubalozini kwa ajili ya kuwarejesha maafisa wetu waliomaliza muda wao katika balozi, aidha, Wizara iangalie uwezekano wa kuacha kutoa barua kwa maafisa kurejea nyumbani kwa fedha kwa ajili ya shughuli hiyo kabla ya fedha hiyo haijatoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maelezo ni kwamba, ni kweli kwamba kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa mambo ya nje, ni lazima maafisa wa mambo ya nje warudi nchini kila baada ya miaka minne ili kubadilishana na Maafisa wengine. Changamoto kubwa inayotukabili katika Wizara yetu katika kutekeleza kanuni hiyo, ni ufinyu wa bajeti, ambayo nimekwishaizungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa taarifa tu, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Wizara imerejesha Mabalozi watano, watumishi tisa na wengine kumaliza muda wao wa kufanya kazi Ubalozini. Mabalozi hao wamerejeshwa kutoka katika Balozi zetu za Tanzania Rome, Tokyo na maelezo zaidi mtayapata tutakapokuwa tunawapa majedwali ya majibu ya hoja zenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hoja binafsi. Mheshimiwa Job Lusinde alikuwa amejaribu kutuuliza, tunazingatia umuhimu wa Chuo cha Diplomasia katika kuwajengea uwezo viongozi wake na Wanadiplomasia? Je, Serikali imetenga fedha kiasi gani kwa ajili ya kuwawezesha Chuo hicho kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Tunasema katika mwaka wa fedha 2016/2017, Chuo kimetengewa kiasi cha bilioni 3.1, kati ya fedha hizo kiasi cha Shilingi milioni 882.2 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo na Shilingi bilioni 2.2 ni kwa ajili ya mishahara ya wafanyakazi, mengine mtayaona katika sub votes zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Masele Steven, ameuliza Wizara imejipangaje ili kuhakikisha uwezekano unaoongezeka kwenye sekta za kilimo, biashara na viwanda kama ilivyo katika Sekta ya Madini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba Wizara imekuwa ikitumia mahusiano mazuri tuliyonayo na nchi nyingine kuvutia uwekezaji hapa nchini. Hii inafanyika kupitia itifaki ya soko la pamoja, kutumia balozi zetu mbalimbali huko nje ya nchi, viongozi wetu kwenye nchi mbalimbali, ziara za viongozi mbalimbali wanaotembelea katika nchi hizo na kadhalika; lakini maelezo zaidi mtayapata pale tutakapokuja kuwaletea majibu katika jedwali la hoja mlizoziulizia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye suala la Wabunge wa Afrika Mashariki. Naomba nitoe tu taarifa kuwa mara tu baada ya uchaguzi wa Wabunge wale ambao sasa hivi wanafanya kazi katika Bunge lile, Wizara iliitisha kikao baina ya Wabunge wa Afrika Mashariki, Ofisi ya Bunge na Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki ili kujadiliana namna bora ya kuwawezesha Waheshimiwa Wabunge wa EALA kufanya kazi kwa ufanisi na bila kero. Yote aliyoyasema Mheshimiwa Msigwa yalijadiliwa na kutolewa uamuzi na wao wanafahamu hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara zote, Wizara wanapokuwa wanaanza session zozote aidha Dar es Salaam au Arusha tunafanya nao vikao wanapoanza au wanapomaliza ili kuwapa mikakati. Niwaeleze tu, sisi tunapokwenda katika vikao vile, viwe ni vikao vya Bunge la Afrika Mashariki ama vikao vya Mabaraza ya Mawaziri tunakwenda na position ya Tanzania na inashauriwa na wale ambao nyinyi mnaowaita Mabalozi wa nyumba kumi kumi na matokeo ya kazi zao za taaluma na ujuzi zimeonekana. Ushindi wa bomba la mafuta la kutoka Tanga kwenda Uganda, hilo pia ni fundisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mtu ambaye anaweza kuwasaidia katika utafiti, tunae yuko Wizarani na wanajua. Vile vile nisisitize tu, Mheshimiwa Waziri wa Sheria aliposema kwamba hawa Wabunge makao yao ni Arusha, lakini unaposema kwamba tuwatafutie ofisi, ofisi Dar es salaam ziliwekwa. Vile vile hawa watu mfahamu kwamba ni Wabunge wanaotoka katika Majimbo tofauti. Kuna wanaotoka Dar es Salaam, Dodoma, Mara na Zanzibar. Sasa, unaposema watafutiwe ofisi centre yao iko wapi? Sisi tumeendelea na tutaendelea na wao wanajua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshiriki katika ku-coordinate mambo yao yote, wanapotafuta maelezo wanapewa, wanapohitaji kukusanya wadau tunafanya na Wizara hii itaendelea kufanya hivyo kwa sababu tumepokea jukumu hili kama viongozi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kufuatia uchaguzi wa Burundi 2015 na ule wa Uganda Februari, 2016, makundi ya wanasiasa, wanaharakati wa haki za binadamu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii, ahsante.