Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza. Napenda nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu - Balozi Mlima, watendaji wakuu, watumishi na maafisa wote wa Wizara ya Mambo ya Nje kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kazi yangu ya kwanza baada ya shule nilikuwa Afisa wa Mambo ya Nje, daraja la II, chumba changu kilikuwa 132. Katika Wizara hapa nchini kwetu au taasisi zenye kiwango cha juu cha uweledi wa utendaji ni pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje. Tunayo fahari kubwa ya kusema kwamba utamaduni huo wa uweledi na professionalism umeendelea na umezidi kuimarika chini ya Waziri mpya na Serikali mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vitu wanavyohitaji wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Nje kutoka katika Bunge hili ni support, ni kuungwa mkono kwa sababu wanatuwakilisha nje ya nchi wanabeba bendera yetu. Foreign policy (Sera ya Mambo ya Nje) ni extension ya domestic policy, ni extension ya mambo tunayotaka kuyafanya, ni kiwezeshi cha malengo ya maendeleo ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Serikali hii iingie madarakani sasa hazijafika siku 180. Kwa hiyo, hukumu iliyotolewa leo dhidi ya Serikali hii hasa kwenye hotuba ya Upinzani kwamba hatukufanya vizuri kwenye Sera ya Mambo ya Nje ni hukumu ambayo siyo ya haki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mambo mengi yakiwemo masuala ya uteuzi wa Mabalozi. Kwanza nadhani Waziri pia atalieleza, procedure ya uteuzi wa Mabalozi inabidi uielewe kabla hujatoa hukumu ya aina ya Mabalozi wanaoteuliwa. Vilevile Rais Magufuli ameteua Mabalozi watatu tu tangu aingie madarakani. Amemteua Dkt. Asha Rose Migiro, Dkt. Dau na Chikawe na taratibu za uteuzi zinaeleweka na huwezi kuniambia katika hawa walioteuliwa hakuna mwenye sifa ya kushika nafasi ya Ubalozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba kuna baadhi ya mambo ambayo tunaruhusiwa kuyafanyia siasa lakini suala la hadhi na heshima ya watu Rais anaowatuma kutuwakilisha nje ya nchi siyo ya kufanyia siasa. Hawa watu tunapowatuma kule nje wanabeba bendera yetu sisi, Bunge hili halipaswi kutumika kuwadhalilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi mkuu wa Sera ya Mambo ya Nje ni kulinda, kutetea na kusukuma maslahi ya Taifa katika mawanda ya kimataifa. Unapoihukumu Serikali hii katika mambo ya Sera ya Nje lazima useme ni wapi, ni lini na ni kwenye jambo gani tumeshindwa kutetea maslahi ya nchi yetu. Huwezi kuihukumu Serikali hii kwenye Sera ya Mambo ya Nje ukashindwa kusema ni kwenye jambo gani, ni lini na ni wapi tumeshindwa kulinda na kutetea maslahi ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu ni kwamba wenzetu hawakusema hayo mambo kwa sababu hakuna, tumeweza na tumefanikiwa. Kwa sababu ingekuwepo mahali ambao tume-fail tungeona kwenye hotuba yao. Tangu Serikali hii iingie madarakani katika mikutano yote na katika forum zote ambazo maslahi ya Tanzania yalihusika tuliwakilishwa na tuliwakilishwa kwa mafanikio makubwa iwe ni Paris, New York na kwingine kokote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Mambo ya Nje haiendeshwi kwenye vacuum bali inaendeshwa katika context ya sifa ya nchi, katika context ya sifa ya Rais na katika historia ya nchi. Sifa ya Tanzania duniani ni nzuri na sifa ya Rais wetu duniani ni nzuri na sifa ya Tanzania leo ni nzuri zaidi kutokana na kazi nzuri anayoifanya Rais hapa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Rais ameamua kuweka mambo sawa hapa ndani, kazi nzuri anayoifanya ndani inazidi kufungua fursa na milango kwa nchi yetu nje na kwa Watanzania waishio nje. Moja ya nyenzo kubwa ya diplomasia ni reputation na sifa ya kiongozi. Sifa ya Rais wetu imeiongezea sifa nchi yetu, imewezesha kazi ya nje ya nchi ambayo wenzetu hawakuifanya vizuri. Kwa hiyo, unaposema Rais hasafiri wakati huo huo kazi anayoifanya inawezesha Sera yetu ya Mambo ya Nje iende vizuri kunakuwa hakuna mantiki hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba moja ya matunda ya kazi nzuri ya Wizara ya Mambo ya Nje ni kwamba sasa hivi sisi tuko kwenye viwanda, ndiyo msingi mkuu wa mpango wetu wa maendeleo ya miaka mitano. Nchi ya China imechagua nchi nne Afrika ambapo itahamishia sehemu ya viwanda vyake. Nchi hizo ni Ethiopia, Kenya, South Africa na Tanzania. Hilo halikutokea kwa ajali, halikutokea kwa kurusha karata, limetokea kutokana na jitihada nzuri za wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Nje na limetokana na kazi nzuri anayoifanya Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya urithi tunaoachiwa na viongozi waliotutangulia ni sifa ya nchi. Moja ya wajibu wetu viongozi wa siasa bila kujali vyama ni kuulinda urithi. Tunao wajibu Wapinzani na sisi kwenye Serikali na Chama Tawala kulinda urithi tulioachiwa na waliotangulia kwenye nchi hii.
Unapoitukana nchi yako ndani ya Bunge unajitukana wewe nje kwa watu tunaowawakilisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mchezo mmoja wa Shakespeare unaitwa Macbeth na nataka nizungumze kwenye quote moja kwenye act five inasema:-
“Life is but a walking shadow, a poor player,
That struts and frets his hour upon the stage,
And then is heard no more.
It is a tale told by an idiot, full of sound and fury,
Signifying nothing”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni is full of sound and fury amounting to nothing. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kuzungumzia suala alilolizungumzia Mheshimiwa Jaku na Mheshimiwa Keissy Mohamed. Nchi yetu sisi ni ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar. Baadhi ya kauli tunazozitoa humu ndani lazima ziheshimu Muungano wetu. Mheshimiwa Keissy Mohamed ni Mbunge wa CCM lakini lugha aliyoitumia sisi kama Serikali hatuikubali na Mheshimiwa Jaku vilevile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inafanya mambo makubwa matatu katika concern walizoleta. Kwanza, Ofisi ya Rais, Utumishi imetoa Waraka wa kuwezesha taasisi za Muungano zitengeneze utaratibu wa mgawanyo wa watumishi wa umma kutokana na quota iliyokubalika ya asilimia 79 na 21. Nimewaandikia Mawaziri wenye taasisi za Muungano kuhakikisha kwamba tunatimiza agizo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Tume ya Pamoja ya Fedha ilitengeneza mapendekezo kuhusu mgawanyo wa mapato na vyanzo vya mapato ya kuchangia shughuli za Muungano. Tumetengeneza Waraka wa Baraza la Mawaziri kwa ajili ya mgawanyo mpya kupitiwa ili tuweze kupata mgawanyo unaoakisi ukubwa wa uchumi na idadi ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, sasa hivi Zanzibar kwa makubaliano inaweza kutafuta misaada yake yenyewe nje ya Tanzania. Hayo ni mafanikio makubwa yaliyotokana na Serikali yetu katika kuimarisha Muungano wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake na naunga mkono hoja hii.