Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti iliyowasilishwa kwenye Hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki ni vizuri ikatekelezwa ipasavyo ili kuweza kuleta matokeo mazuri yaliyotabiriwa. Tatizo kubwa la bajeti za Wizara mbalimbali ni kutopatikana kwa fedha zinazoidhinishwa na Bunge kwa wakati ili utekelezaji wa mipango iliyotengewa fedha kwenye bajeti uweze kufanyika kwa wakati uliopangwa. Ni muhimu Hazina izingatie hili na kutoa fedha kwa wakati unaostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje na Serikali kwa ujumla haikutoa tamko lolote kwenye Hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje, kuhusu vitendo vya ubaguzi na udhalilishaji unaofanywa na baadhi ya wananchi wa India dhidi ya Waafrika waliopo India. Matukio ya udhalilishaji wa Mtanzania mwanafunzi, aliyevuliwa nguo zake na kuburuzwa mtaani, raia mwingine wa Congo ambaye aliuawa kikatili na matukio mengi dhidi ya Waafrika huko India, haya ni mambo makubwa ya kidiplomasia ambayo hayapaswi kuachwa yapite bila kukemewa na kuyatolea tamko na Waziri mwenye dhamana ya mahusiano na nchi za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 23 Juni, 2016, Uingereza itapiga kura ili wananchi wake waamue ama kuendelea kuwemo ndani ya Jumuiya ya Ulaya (EU) ama kutoka kwenye Jumuiya hiyo, mpango ulio mashuhuri kwa kujulikana kama BREXIT. Ni vizuri Wizara hii ingefanya tathmini na kushauri je, nchi yetu itaathirika vipi na kunufaika vipi na hatua hiyo ya Uingereza hasa kwa kuwa Uingereza imekuwa na ushawishi mkubwa kwa baadhi ya sekta za maendeleo ndani ya Jumuiya ya Ulaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tathmini hizi ni muhimu ili kuiandaa nchi yetu ipasavyo. Je, kama Uingereza itajitoa kwenye Jumuiya ya Ulaya bila Uingereza kwa nchi yetu itapungua au itaongezeka? Haya ndiyo maswali ambayo wananchi wa Tanzania wangependa kupata majibu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii inabidi kuratibu kwa weledi zaidi mahusiano ya nchi za nje ili nchi wahisani wasiathiri mipango ya maendeleo ya wananchi wetu Watanzania kwa kuvunja makubaliano tunayoyafanya kwa sababu za kisiasa. Uamuzi wa Marekani kusimamisha mpango wa MCC II kwa Tanzania ni mfano mzuri. Hali ya kutegemea misaada kutoka kwa wafadhili na marafiki zetu ina gharama zake. Tusipoweza kuratibu kwa weledi wa hali ya juu tutavuruga mipango mizuri ya maendeleo ya wananchi wetu. Tanzania ni nchi huru ina heshima yake hatutaki mahusiano ya kudharauliana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.