Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Napenda kukupa hongera kwa kazi unayoifanya kwa ujasiri mkubwa na kukwambia kwamba endelea kuchapa kazi, wala usiwe na wasiwasi, tuko na wewe. Pambana na wote wanaovunja kanuni bila kurudi nyuma, usirudi nyuma, nasi haturudi nyuma, tuko na wewe bega kwa bega. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uchumi wetu kwa kiasi kikubwa bado tunategemea kilimo kwa asilimia kubwa sana. Kilimo hiki bado ni duni sana, tunatumia jembe la mkono, mbegu hafifu, mbolea tabu, dawa tabu na kadhalika. Kwa hiyo, napenda kuona bajeti hii kama ingesisitiza kwenye kilimo kwa mtindo ambao nimewahi kuusema hapa siku za nyuma na bahati nzuri kwenye Ilani ya CCM mpango huo umeingizwa, kambi za kilimo za vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijana wengi Dar es Salaam na miji mingine mingi tu wanakaa hawana kazi za kufanya, lakini tuna maeneo mengi sana nchi hii yana rutuba nyingi sana, yana maji ya kutosha na yanafaa kwa kilimo kizuri. Niliwahi kusema na leo naomba nirudie kwa umuhimu wake kwamba tuanzishe kambi za kilimo kwa vijana hawa ambao wanakaa bila kazi. Juzi Mheshimiwa Rais, Dkt. John Magufuli alisema kwamba wasiopenda kulima wapelekwe kwa nguvu, lakini mimi nasema wapelekwe kwenye hizo kambi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yenye maji, yenye rutuba yaainishwe, peleka vijana kama 500 kambi moja, wawe na msaada wa usimamizi. Bwana Shamba awepo, Daktari wa kuwatibu awepo wakiugua matumbo na malaria, wapewe mbolea, wapewe trekta kwa sababu kulima kwa jembe la mkono ni tatizo. Huwezi kutoka kwenye uchumi duni kwa jembe la mkono, wapeni matrekta ya mkopo moja au mawili. Wapewe power tillers tano au kumi, hazina gharama kubwa waanze kulima mahindi, maharage, karanga, alizeti na mazao mengine yenye thamani kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka wa jana nilikuwa hapa, nikaona watu wa Uganda, Kenya, wanakwenda kwa Waziri wa Kilimo aliyekuwepo wakati huo kutafuta mahindi kwa sababu kwao wana njaa lakini yakakosekana kwamba hatuna mahindi ya kutosha kupeleka nchi za nje. Tukiwa na mahindi, maharage, alizeti na kadhalika tutauza nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijana hawa wakikaa kwenye kambi kwa mwaka mmoja, hata miezi tu, maharage ni siku 60, watavuna maharage mengi sana, watavuna mahindi mengi, tutapata chakula kingi nchini na tutauza nchi za nje lakini wasaidiwe, wasimamiwe, wafanye kazi, hapa kazi tu. Wafanye kazi vizuri, kwa ufasaha na kisasa kuliko kukaa wanazurura mitaani kule Dar es Salaam au humu barabarani Dodoma na sehemu nyingine bila kazi za kufanya. Kazi ni kilimo, wakivuna vizuri ni utajiri mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mwaka mmoja watakuwa matajiri hawa. Zile kambi kama watajengewa nyumba za bati zile full suit baada ya miaka miwili watajenga nyumba nzuri za kudumu, watakuwa na fedha, utakuwa mji ule baada ya muda mfupi wa kufanya kilimo hiki kwa namna ambayo naipendekeza. Haya ndiyo mawazo yangu kuhusu kilimo. Maeneo ya namna hii yako mengi sana kote nilikopita, maeneo ya Morogoro kuna rutuba nyingi sana, kuna mito mingi sana, maji mengi, Kigoma rutuba nyingi sana, maji yapo, maeneo ya Ruvuma, Rukwa na maeneo mengine mengi ambayo kuna uwezekano huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala ambalo limesemwa na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake kwamba Mkoa wa Kagera ni kati ya mikoa mitano maskini sana Tanzania. Ni kweli, Kagera ni mkoa maskini sana na sababu zinajulikana. Zao la biashara Kagera ni kahawa, kahawa hii ina kodi 26, kwa nini wananchi hawa wa Kagera wasiwe maskini? Hii kahawa ikiuzwa nje kwenye soko la dunia kila Sh. 100 mkulima anaambulia Sh. 20, ni wazi atakuwa maskini tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimelisema hili jambo, nilimwambia Mheshimiwa Rais kwenye kampeni, akaja akalisema hapa kwamba kodi hizi zitafutwa. Akasema Waziri wa Fedha, Waziri wa Biashara na Waziri wa Kilimo wafute kodi hizi haraka iwezekanavyo. Juzi nilirudia kuliuliza hapa kwenye swali, nikategemea kwamba kwenye bajeti hii kodi hizi zitaondoka, bado sijasikia zikiondoka lakini Waziri anatuambia Kagera ni maskini, sababu kubwa ndiyo hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hii haitoshi, kule Kagera barabarani kuna barriers za kutisha. Kila kilometa tano kizuizi barabarani, kama una ndizi toa Sh. 2,000, kama una nanasi toa Sh. 1,000, jamani, lazima wananchi hawa watakuwa maskini, lazima watakuwa maskini wa kutupwa. Hali ni ngumu sana, niombe sana jambo hili liangaliwe kwa kina. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hii haitoshi, kule kuliingia ugonjwa wa mnyauko wa migomba, migomba yote imeungua na ugonjwa. Wananchi hawana chakula, hawana zao la biashara, kwa nini wasiwe maskini? Huu ugonjwa wa mnyauko si mkubwa, ulikuwepo Uganda wakauondoa kwa jitihada za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni rahisi sana, sheria ndogo zinatungwa na zinasimamiwa. Sasa Kagera ugonjwa huu umekuwa kama vile UKIMWI, hauna dawa, lakini dawa yake ni ndogo mno, ni kuing‟oa migomba ile na wananchi wasimamiwe ugonjwa huo uondoke. Inatakiwa wananchi wapate msaada ugonjwa huu uondoke ili mkoa huu uondoke kwenye dimbwi la umasikini la mikoa mitano ya mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba miaka nyuma kidogo tumechangia sana kujenga maabara za sekondari. Tumejenga sekondari nyingi nchini chini ya mpango maalum, majengo mengi yamekamilika tukaanza kujenga maabara. Maabara hizi sasa zimeachwa, hazijengwi tena, nyingine ziko kwenye lenta pale, kwenye ring beam, nyingine ziko chini ya hapo, nyingine zimeezekwa lakini hazijakamilika. Ni jitihada nzuri iliyofanyika lakini zimeachwa tu hazina kazi, ujenzi haujakamilika na maabara hizi hazijaanza kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe mpango ufanywe kwenye bajeti hii, maabara hizi zikamilike ili shule hizi zikamilike ziwe shule nzuri za sekondari, ziwe na vifaa vya maabara za kisayansi ili wanafunzi wasome masomo ya sayansi kwa vitendo. Zisiachwe zikaanza kuota ukungu, nyumba hazijakamilika na hazina vifaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.