Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza kwa kunipa nafasi hii ili nitoe mchango wangu lakini pia niweze kuipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo imetoa bajeti ya tofauti ya trilioni saba. Hiki ni kiwango kikubwa sana kwa nchi yetu kama ambavyo tutafikia haya malengo na kwa vyovyote mafanikio yatakuwa makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mchango mdogo wa kuishauri Serikali. Kwanza tusimamie mapato ili tuweze kufanikiwa katika hali hii ya ukusanyaji. Nilikuwa nategemea pengine tukusanye mapato kwenye forodha, viwanda na pia tuweze kukusanya kwenye makampuni makubwa. Eneo hili tukifanikiwa tukafika hiyo asilimia mwaka huu ni dhahiri kwamba tumefaulu kwa kiasi kizuri na mwakani ni mlango wa kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie eneo la CAG. Hawa wakaguzi wanafanya kazi katika mazingira magumu sana kwa sababu Mkurugenzi anayekaguliwa ndiye anayemwezesha. Nashauri kama itawezekana kitengo hiki cha ukaguzi kiweze kujitegemea katika nchi yetu kutoka ngazi ya Taifa, Mkoa na Wilaya ili tuweze kufikia malengo mazuri. Kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamelalamikia sana hela ndogo ya CAG, kwa kweli kama hatujaweza kumwezesha CAG katika dhana nzima ya fedha, watumishi na dhana nzima ya vitendea kazi kwa vyovyote vile tunachokifanya hakipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri kule chini tuna mambo mengi sana. Kuna ya maabara, zahanati pamoja na nyumba za Walimu yameachwa. Kila mwaka tumeshindwa hata kutatua baadhi ya yale maboma. Kwa hiyo rai yangu kwetu sote ni kwamba, fedha zilizoombwa na Halmashauri hizi zifikishwe katika ngazi hizo za Halmashauri na tuweze kufuatilia. Kwa sababu hiyo tunaweza tukafika na huduma itatolewa katika ngazi hiyo ya chini na kutatua kero kwa ngazi ya Jimbo. Kwa jinsi ambavyo miradi mingi ni viporo hata miaka mitano ya sisi Wabunge inaweza kwisha hatujatatua hata kitu kimoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama ambavyo nilizungumzia hilo, naomba utoaji wa fedha zile ambazo zinapelekwa kwenye ngazi za chini ziweze kufanya vizuri. Pia nchi yetu imekuwa na hali mbaya ya bidhaa feki. Hizi tumebaki kuteketeza kwa sababu tayari baada ya muda tunaona zimeshaingia nchini, ziko ndani ya soko, kwa hiyo kiwango hiki kinaathiri sana uchumi wa jamii na kwa hivyo hali hii inawafanya wananchi washindwe kuelewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kama itawezekana wale wanaodhibiti na kuangalia ubora wa bidhaa zinazoletwa kutoka nje na zile za ndani waweze kuwa makini kuangalia ni kwa namna gani ambavyo bidhaa hizi zinadhibitiwa ili zisiwe zinavuruga soko kwa sababu tunapokwenda kuchoma au kuteketeza ni tayari wananchi wanapata hasara kubwa kiuchumi na pia wanadhurika kiafya, kwa sababu kuna madhara ya afya na kuna madhara ya kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika ngazi hii ya Halmashauri tungeomba ikafanye semina ya Waheshimiwa Madiwani. Miradi mingi ya ngazi za chini Waheshimiwa Madiwani hawawezi kutambua na kujua miradi hii na thamani yake kifedha. Kwa hiyo, tukiweka fedha za semina na fedha za uwezeshaji katika zile Kamati, hasa Kamati ya Uongozi ni imani yangu kwamba watatusaidia sana katika kukagua miradi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia bado hatujanufaika katika rasilimali gesi na mafuta kwa kuwa labda ni mwanzo, lakini naomba kwa mwaka unaokuja pia tuone ni namna gani tunanufaika katika rasilimali hizi za gesi na matuta kwa kiwango kizuri ili nchi yetu iweze kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji wanalalamika, ifike baadae huko tufike na wao tunawawezesha, tukikusanya hela vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, si vibaya tukawa na chombo kinachofuatilia ukusanyaji wa mapato katika Taifa letu. Ukusanyaji huu wa mapato sio ukusanyaji mzuri kwa sababu kwa vyovyote vile kuwaachia tu TRA wao ndiyo wakusanye na hatuwezi kubaini na kufanya utafiti kwa vyovyote hatutafika. Nashauri tuwe na chombo kinachoweza kufuatilia ukusanyaji wa mapato ili kiwe kinaielekeza Serikali kufanya kile kinachowezekana. Kwa hiyo, kwa vyovyote vile mara nyingi Serikali yetu imekuwa na wakati mgumu pale ambapo mifumo ya bajeti inapokusanywa na baadaye katika matumizi, hatuna vipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kuwe na uwiano wa vipaumbele vya matumizi ya bajeti kwa pale ambapo pesa hizi zimepatikana katika Central Government na Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi nilipokuwa kule ngazi za Halmashauri nilikuwa nafikiri huku kuna neema, nimekuja huku vilio ni balaa. Kwa hiyo, naomba kama itawezekana kwa vyovyote ngazi hizi za chini ziweze kuletewa hela kwa kuwa wao ndiyo walio karibu sana na wananchi wetu na kwa vyovyote wasingeweza kufanya kazi hiyo na wasingeweza kuona.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naishauri Serikali iweze kuratibu ahadi za Mheshimiwa Rais ili kwa mwaka tujue ni ahadi ngapi tumetekeleza na ahadi zipi zimebaki na kupitia Mbunge wa Jimbo na Serikali tuone basi yale yatakayotatuliwa chini ya uwezo wa Serikali yanapata kutatuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vyovyote vile katika hali hii ya nchi yetu kutafuta mapato na tunatoka trilioni 22 tunaenda 29 ni kiwango kikubwa sana na hali hii itatufikisha mahali pazuri jinsi ambavyo fedha hizi zikipatikana zitatatua kero za wananchi. Sisi tunaotoka kwenye Majimbo tuna wakati mgumu sana. Wakati wa kuomba kura unasema jamani nitajenga daraja, baadaye uchaguzi ukiisha daraja linakuwa kubwa na uwezo wa kujenga lile daraja unakosekana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina ushauri kuhusu fedha za maji. Miongoni mwa maswali mengi yaliyoulizwa na Waheshimiwa Wabunge ni juu ya miradi mingi ya maji nchini. Nizungumzie uzoefu wa Jimbo la Mbulu au majimbo yote mawili ya Mbulu. Wataalam wanateua wazabuni ambao hawana fedha, hawana uwezo na kwa hivyo baadaye wale wazabuni wanashindwa kutekeleza ile miradi na tusitarajie kwamba hiyo miradi ya maji itakamilishwa kwa Juni, 30 hii siyo rahisi hata siku moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kwa vyovyote Serikali iratibu, ipitie miradi upya, itoe maelekezo kwa ngazi za Halmashauri ili waweze kuvunja mikataba inapobidi, kwa sababu katika Jimbo la Mbulu tuna miaka miwili wananchi hawajapata huduma, lakini pia miradi imetelekezwa. (Makofi)
Kwa hiyo, nashauri, Serikali itoe maelekezo ipitie upya mikataba iweze kuondoa ile mikataba ili wananchi wapate huduma stahiki. Nia hiyo ya Serikali kusema tunalipa kile kilichokamilika ni utaratibu mzuri wa Serikali, lakini kama hawawezi kufika na hawawezi kutekeleza ungefanyaje? Kuna miradi toka mwaka 2013 haijakamilika mpaka leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nashukuru na naunga mkono hoja.