Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nianze kwa kukupongeza kwa kazi nzuri unayofanya. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi walivyowasilisha vema bajeti ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kitabu cha Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2016/2017 ukurasa wa tisa mpaka wa kumi inabainisha kwamba kuna mikoa mitano ambayo inaongoza kwa umaskini. Nimesikia wenzangu walivyosema, sina sababu ya kukataa jinsi hiyo mikoa ilivyobainishwa kwa sababu nitaingia kwenye ubishi wa kiuchumi na wachumi siku zote huwa hawana jibu moja, kwa hiyo kwa sasa hilo naliacha. Nakubaliana na jinsi Mheshimiwa Waziri alivyowasilisha mikoa mitano lakini hoja yangu ni kwamba baada ya kuwa nimeiona hiyo mikoa mitano nikisoma kitabu cha bajeti sioni sasa kwa nini Mheshimiwa Waziri aliwasilisha hiyo mikoa mitano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilifikiri baada ya kuibainisha basi bajeti hii ingekuja na mikakati maalum ya kusaidia hiyo mikoa mitano. Kwa kuwa sijaona, nitajaribu kubainisha baadhi ya maeneo ambayo tukitumia hoja hiyo hiyo kwamba tunayo mikoa mitano maskini sana, mambo yapi tusifanye ili kuendelea kuifanya hiyo mikoa kuwa maskini zaidi. Najua yapo mambo mengine ambayo yanaweza yakafanywa lakini nijikite kwenye bajeti yenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, katika ahadi tulizotoa kwa wananchi, maana ukiangalia mikoa hii baadhi yake inalima kahawa na wengine wanalima pamba, lakini kahawa kwa mfano tuna aina ya kodi 26 ambazo tulibainisha kwamba kodi hizi zitapunguzwa au kufutwa kabisa. Bajeti hii mapendekezo pekee ya kodi inayopendekezwa kufutwa ni ada ya kukaanga kahawa kwa ajili ya kuuza soko la nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, ile ada inayofutwa ni moja kati ya 26 zilizopendekezwa kupunguzwa au kufutwa. Kwa hesabu ya haraka haraka maana yake ni kwamba, hapo Mheshimiwa Waziri atakuwa ametekeleza asilimia tatu ya kile tulichoahidi. Kwa hiyo, mapendekezo yangu ni kwamba zile kodi 25 zilizobaki ingekuwa vizuri na zenyewe zikafutwa na zifutwe sasa katika bajeti hii kwa sababu hivyo ndivyo tulivyoahidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia haraka haraka, je, wenzetu waliotuzunguka ndani ya Afrika Mashariki wanafanya nini? Uganda wao wana kodi ya asilimia moja tu katika zao la kahawa na ndiyo maana utakuta Watanzania wengi wanapenda kahawa yao wauze kupitia Uganda kwa sababu kule kuna unafuu wa kodi lakini sisi tuna kodi 26. Ukiangalia kwa nini tusifute kodi hizo hupati sababu. Vietnam kwa mfano wao wana asilimia moja tu kwenye zao la kahawa ambayo inakuwa charged kwenye point of exit, Uganda wana asilimia moja, sasa sioni sababu kwa nini na sisi tusifanye hivyo na tufanye hivyo katika bajeti hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, wataalam wa uchumi wanatuambia mkulima wa Tanzania hasa wa kahawa yeye anatozwa wastani wa asilimia 70 ya fedha yote inakwenda kwenye kodi, lakini kwa Tanzania corporate tax ni asilimia 30 na akiwa amepata hasara halipi kodi hiyo, lakini kwetu sisi mkulima asilimia 70. Huyu mkulima apate faida, apate hasara, asilimia 70 ipo palepale. Kwa hiyo, nadhani hilo eneo tunaweza kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ukiangalia hii ada ya kukaanga kahawa inayopendekezwa kufutwa inamnufaisha nani? Ada hiyo inayanufaisha makampuni makubwa yanayofanya biashara ya kuuza kahawa nje na siyo wakulima wadogo wadogo. Kwa hiyo, nadhani kuna haja ya kulitazama hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tulipopitisha sheria hapa ya kuruhusu haya makampuni makubwa kuingia kwenye ushindani wa kununua kahawa, tulitoa angalizo na sheria iko wazi kwamba hawa tuliowaruhusu kununua kahawa kushindana na Vyama vya Ushirika, wasishindane na Vyama vya Ushirika kwenye grass roots. Tuliwaambia wakitaka kununua kwenye grass root, basi kule Moshi wasiende kushindana, wasifanye mambo mawili. Huwezi ukawa unanunua kwa mkulima, halafu unakwenda Moshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilichotokea hadi sasa ninavyozungumza, wanunuaji hawa wakubwa, kina OLAM na wengine wananunua kwenye grass roots, wakienda mnadani wanakwenda kununua kahawa yao tu waliyonunua, kwa hiyo unaua ushindani na inaleta tatizo kubwa kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ambayo napenda kuizungumza haraka haraka, maana tuna mikoa mitano ambayo tunaambiwa ni maskini sana na sina ubishi lakini tufanye nini sasa. Kuna ugonjwa wa mnyauko fizari. Huu ugonjwa wa mnyauko fizari umeleta janga la kitaifa kwa sababu kwa muda mrefu Mikoa ya Kigoma, Kagera na mingineyo tumekuwa tukijitosheleza kwa chakula lakini baada ya huu mnyauko fizari kuanza hatuwezi kujitosheleza kwa chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli nafikiri kutaja tu mikoa hii inaongoza kwa umaskini haitoshi, ningefurahia kama Mheshimiwa Waziri angetangaza kwamba kuna janga la kitaifa la kupoteza migomba, kwa hiyo tunakuja na mkakati maalum. Tunajua wataalam wetu wa kilimo wamejitahidi kutafuta ufumbuzi, ufumbuzi peke yake waliopata ni kufyeka, kwamba migomba ikipatwa na ugonjwa wa mnyauko fizari dawa ni kufyeka tu, kwa hiyo wanatembea na mapanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani dawa si kufyeka tu, hata kama ni kufyeka Mheshimiwa Waziri anaweza akaja na physical, bajeti inaweza ikasema tutakuja na panga la kufyeka lakini wakati huo huo tuna milioni moja, tunasema tukifyeka hapa kwa sababu umekumbwa na ugonjwa wa mnyauko fizari tunakupa fedha ya kukuwezesha kuishi kwa miezi sita, miezi saba, mwaka mmoja mpaka hapo utakapoanza kuvuna. Watakuita wenyewe wakulima kwamba njoo ufyeke hapa, lakini kama unatembea na panga tu na kama akili yetu inaishia kwenye kutembea na panga tu na kufyeka, basi tujue tutazidi kuongeza umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la msingi kuna Benki ya Maendeleo ya Wakulima. Benki hii ya Maendeleo ya Kilimo yenyewe inasema kahawa si zao la food security. Napenda nitoe hoja hapa kwamba kahawa ni zao la food security kwa sababu mkulima akiweza kuvuna vizuri atauza atapata chakula. Kwa hiyo, ni uwezo mdogo wa kufikiri kusema kwamba zao la kahawa halihusiani na food security, si kweli. Kwa sababu ukishasema hivyo maana yake Vyama vya Ushirika vinalazimika kuendelea kukopa kutoka CRDB asilimia 18 ili viende kununua kahawa na vinakwenda kushindana na wanunuzi wengine wanaokopa nje kwa asilimia tatu na kuendelea, huwezi kushindana namna hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa harakaraka naomba nimtahadharishe Mheshimiwa Waziri, anafahamu kwamba alipokutana na wenzake katika Afrika Mashariki wamekubaliana kwa Kenya, vile viwanda vinavyozalisha ngozi na mambo mengine, wanapozalisha wa-offload kwenye soko la Kenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, unapo-offload bila kulipa italeta madhara makubwa kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, natarajia Mheshimiwa Waziri atanipa ufafanuzi akiwa anajibu hoja.