Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu katika mada yetu hii iliyokuwa mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukuke fursa hii kuipongeza Serikali kupitia Wizara ya Fedha na wataalam wao kwa kuleta bajeti nzuri kwa sababu ni bajeti ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano. Bajeti hii ndiyo inatoa mwelekeo wa Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na imeonesha anapita kutokana na maneno yake aliyokuwa anaahidi wakati wa kampeni. Aliahidi viwanda na kweli bajeti inatafsiri hivyo, inaanza kujiandaa kwa ajili ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niseme hii bajeti kubwa imejielekeza hasa kwenye miundombinu na elimu, miundombinu ni asilimia 25 na elimu asilimia 22, jumla 47. Hivi ni vitu muhimu sana katika maendeleo ya viwanda kwa sababu vikwazo vikubwa kwa wawekezaji wengi ilikuwa ni miundombinu sasa bajeti inaenda kutibu hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, naomba kwanza nipate…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nichukue fursa hii nipate tu ufafanuzi kutoka kwa Waziri wakati akija kuleta majumuisho yake hasa kutokana na hotuba yake kwenye ukurasa wa 57 hasa kwenye ushuru wa mafuta ya kulainisha mitambo kutoka Sh. 665 hadi Sh. 699 kwa lita. Kwa sababu kwa ufahamu wangu ushuru wa sasa hivi ni senti 50 kwa lita na kama ushuru ndiyo huu ulioandikwa hapa Sh. 665, ni ushuru mkubwa sana. Kwa hiyo, namwomba tu alete ufafanuzi wakati anakuja kufanya majumuisho yake ipi ni sahihi, hii iliyoandikwa kwenye kitabu au ni hii inayotumika sasa hivi huko field 0.5 cent kwa lita moja ya mafuta ya kulainishia mitambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, naomba ufafanuzi pia kwenye takwimu, nimesoma kwenye kitabu hiki cha Hali ya Uchumi cha mwaka jana hasa kwenye ukurasa wa 149, uzalishaji wa mazao ya mafuta. Nimeona kwenye ufuta, alizeti, kwa mfano alizeti Tanzania tunazalisha tani milioni 2,878,500, karanga tani 1,835,933, ufuta tani 1,174,589. Nichukulie kwenye ufuta tu, hata nchi zinazoongoza ulimwenguni kama ni Myanmar kule na China hawajafikia kiasi hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe tu Mheshimiwa Waziri na timu yake wakae vizuri waangalie hasa hii Idara ya Takwimu au hizi mlikozipata kwa sababu hizi data ziko kwenye mitandao na zinaenda, zinaweza zikapotosha wawekezaji wakaja hapa halafu malighafi hakuna au tunaweza kupanga mipango yetu kwa kuamini kwamba malighafi ipo kumbe hamna. Tunazo data za kutoka Custom kwenye Ofisi yake, mwaka jana usafirishaji wa ufuta kwenda nje ya nchi ni tani 133,000 kutoka mwezi Juni mpaka mwezi Desemba. Naomba tu wazipitie vizuri wakalete data halisi ambazo zinaweza zikawa kichocheo kwenye uchumi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda ufafanuzi wa mwisho, kama nilivyosema mwanzoni hii bajeti ni ya miundombinu. Kwa bahati mbaya sana sijaona kwenye bajeti hii miundombinu ya kwetu kule, barabara hasa ile ya Bigwa - Kisaki kwa kiwango cha lami. Mradi ule ulikuwa ugharamiwe na MCC na hao MCC sasa hivi wamejiweka pembeni. Kwa ajili ya mradi ule na miradi mingine Tanzania iliyokuwa inagharamiwa na MCC sijui sasa Serikali imejipangaje kwa ajili ya kutekeleza pengo hili lililoachwa na hawa jamaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kwa sasa nijielekeze kwenye mchango wangu. La kwanza ni kuhusu Mfuko wa Maji. Wabunge wengi wamezungumzia suala hili kwa sababu maji ni uhai. Nami lazima nijikite hapa kwa sababu tuna tatizo kubwa sana la maji katika Jimbo langu la Morogoro Kusini hasa katika vijiji kama vya Mkuyuni.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa maji uko miaka 15 haujawahi kufanyiwa ukarabati na vijiji vile ambavyo vilikuwa vitongoji sasa hivi vimekuwa vijiji kama vijiji vya Kivuma, Kibuka na Mwalazi wanategemea maji ya mradi huo huo ambao uliwekwa tanki la 10,000. Tukiomba tunaambiwa kwamba vijiji vingine havijapata maji wakisema ni lazima wamalize vijiji vingine ndiyo waje kwenye ukarabati wakati sasa vile vitongoji vimeshakuwa kata.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kibuka kilikuwa Kitongoji cha Mkuyuni sasa hivi ni kata inategemea mradi wa kijiji hicho hicho. Kwa hiyo, nimwombe Waziri akubaliane na mawazo mengi ya Wabunge kuongeza hii Sh. 50 katika lita ya petrol na diesel ili twende kutatua tatizo la maji vijijini. Sauti ya wengi ni sauti ya Mungu, Wabunge wote wana kilio cha maji na Sh. 50 kuongezwa. Wabunge kazi yetu ni kuishauri Serikali namwomba Waziri apokee ushauri huu ili tukatatue tatizo la maji na vituo vya afya na zahanati kwa sababu mzigo huu wananchi walishabeba muda mrefu sana kwa kuchangia zahanati na vituo vya afya huko vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kuchangia ni kupunguza tatizo la msongamano Dar es Salaam ili kufungua fursa za uchumi na kuharakisha maendeleo ya uchumi. Tatizo la msongamano Dar es Salaam linaathiri sana uchumi wa Taifa letu kwa sababu watu wanatumia muda mrefu kufika kazini na wanatumia muda mchache kufanya kazi. Tatizo hili nilishawahi kusema siku moja, ni lazima tufungue vituo vikubwa vya kibiashara na bandari kavu nje ya Dar es Salaam na ukisema nje ya Dar es Salaam basi Morogoro ina sifa mojawapo ambayo baadhi ya mikoa mingine haina.
Mheshimiwa Naibu Spika, Morogoro ni mkoa ambao umepitiwa na reli zote mbili, reli ya kati na reli ya TAZARA. Tunaweza kutumia reli hizi ili kuingiza na kutoa mizigo bandarini kwa kutumia treni badala ya magari yote kutoka mikoani na nchi zingine zikapakia mizigo pale Morogoro. Pamoja na juhudi kubwa za Serikali kutatua changamoto ya foleni Dar es Salaam lakini kwa kuanzisha bandari kavu Morogoro tutakuwa tumepata suluhu ya kudumu kumaliza changamoto hii lakini pia tumeinua hali za uchumi wa sehemu hizo zingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka kuchangia katika sekta hii ni suala la kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu na wengi wamechangia umuhimu wa kilimo, unaajiri asilimia 70 ya watu wetu, pato la Taifa asilimia 25, hela za kigeni zaidi ya asilimia 30 inatoka kwenye kilimo, chakula asilimia 100, malighafi asilimia 65 lakini bajeti hii imejikita zaidi kwenye miundombinu badala ya kutatua uchumi wa watu wengi walikojiajiri kwenye kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwamba niliona kwenye Mpango kwa ajili ya kuendeleza sekta ya kilimo katika suala la Mkulazi, lakini sikuona kwenye Mpango wa 2016/2017, nilijua sasa kilimo ndiyo kitapewa kipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushauri katika hili…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.