Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia hoja katika Bunge lako Tukufu, kabla sijafanya hivyo naomba nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuijalia amani nchi yetu na kutuwezesha sote kuwepo hapa kushiriki katika Mkutano huu ambao ni wa kwanza wa bajeti tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Aidha napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli pamoja na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kwa kupata ushindi wa kishindo katika chaguzi zilizopita. Ushindi huo ni ishara ya imani kubwa ya wananchi waliyonayo kwa Rais, Makamu wa Rais na kwa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa, Mbunge kwa kuteuliwa kwake kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile napenda kuwapongeza Mheshimiwa Spika na Naibu Spika kwa kuteuliwa kwao kuliongoza Bunge hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mhandisi Gerson Lwenge, Mbunge, kwa kuteuliwa kwake kuwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji na pia namshukuru kwa ushirikiano mkubwa anaonionesha katika kutekeleza majukumu yanayozikabili sekta za maji na umwagiliaji. Natoa shukurani zangu kwa Mheshimiwa Rais kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Wizara inayomgusa kila mwananchi katika kurudisha imani hiyo kubwa ninaahidi kuwatumikia wananchi wa Tanzania kwa uadilifu haki bila upendeleo, nina ahidi kufanya hivyo kwa kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia na kwa ufupi niseme hapa..Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe shukrani kwa wananchi wa Jimbo la Katavi kwa imani yao waliyonipa kwa kunichagua kuwa Mbunge wao kwa kura nyingi za kishindo.
KUHUSU UTARATIBU...
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe shukurani kwa wananchi wa Jimbo la Katavi kwa imani yao waliyonipa kwa kunichagua kuwa Mbunge wao kwa kura nyingi za kishindo. Nawaahidi nitawatumikia wote, kwa nguvu zangu zote kadiri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwapongeze Wenyeviti wote wa Bunge kwa kuchaguliwa kuliongoza Bunge letu Tukufu na pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchaguliwa kwao kwa kuwawakilisha wananchi waliowachagua katika Bunge hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nichukue fursa hii kuishukuru familia yangu nikianzia na mke wangu kwa ushauri na ushirikiano mkubwa wanaonipa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, sasa naomba nichukue nafasi hii kuchangia hoja mbalimbali ambazo zimeibuliwa na Wabunge kupitia kwenye bajeti ambayo imewasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda niliopewa ni dakika 15, itabidi nipite kwenye maeneo machache ya ujumla, maeneo mengine yatahitimishwa na Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na suala la madeni. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia changamoto ya madeni kwamba ni kweli Wakandarasi ambao waliingia mikataba kwa ajili ya miradi ya maji, kumekuwepo na madeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe taarifa ifuatayo:-
Miradi ya Maji Vijijini tuliingia mikataba ya shilingi 887,844,161,282. Hadi leo fedha ambazo zimeshalipwa ni shilingi 553,175,872,452 na kiasi kilichobaki ni shilingi 334,668,288,830. Hata hivyo, certificates tulizonazo mkononi ni za thamani ya shilingi 10,822,464,268. Tunamshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha anaendelea kutupatia pesa na ameahidi kutupatia fedha hizi na zitakuwa zimelipwa kabla ya mwaka wa fedha huu tulionao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Miradi ya Maji Mjini, tuliingia mikataba ya shilingi 1,379,471,322,665. Fedha iliyolipwa ni shilingi 1,266,610,684,020. Fedha tunayodaiwa ambayo tuna hati za madai mkononi ni shilingi 50,594,881,957.
Waheshimiwa Wabunge, kwa bahati nzuri kwa sababu hii miradi imekuwa inachangiwa na wafadhili, wadau wanaopenda kuchangia katika maendeleo yetu ya kuleta maji, Benki ya Maendeleo ya Ufaransa tayari wamekubali kwamba deni hili wao watalilipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari wameshaanza kutoa tayari fedha kwa ajili ya kulipa deni hili. Kwa hiyo, mpaka tunamaliza mwaka wa fedha huu tulionao, mwezi Juni tarehe 30, tutakuwa hatudaiwi katika miradi ya maji kwa maana ya hati ambazo zimeshawasilishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu wakandarasi wanaendelea na kazi, wanaweza wakaleta certificates nyingine na tutaendelea kwamba kila tukipata certificate tunapeleka Hazina ili tuweze kupewa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe maelekezo katika hili. Mamlaka zote kuanzia category A, B, na C; ambapo category C mara nyingi ziko upande wa Halmashauri; pale ambapo Wakandarasi wa miradi ya maji wana mkataba, wakishapata certificate, basi watutumie ili tuweze kuipeleka Hazina, tuweze kupata pesa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi hatuwezi kupeleka hela mahali ambapo hujaingia mkataba na ambapo hujazalisha. Tumegundua hilo tatizo kwamba watu wengi wanasema kwamba hela haijaja, kumbe unakuwa hujaleta certificate ili tuweze kuipeleka Hazina. Hazina haiwezi kutoa hela kama wewe hujaingia mikataba na kama wakandarasi hawajazalisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nitoe maagizo kwa Wakurugenzi wote ambao wanahusika na Miradi ya Maji, kwamba hatuwezi kuleta pesa mpaka walete hati za madai, kuhakikisha kwamba kazi hiyo imeshatekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge pia katika michango walioneshwa kutokuridhishwa wakati mwingine na hali ya utekelezaji wa miradi. Wakati mwingine viwango vya utekelezaji vinakuwa viko chini. Certificates hizo tukizipokea, wakati mwingine tutalazimika kuunda timu katika Wizara na kwenda kukagua hiyo miradi kuangalia kama kweli kazi hiyo imetekelezeka.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, Waheshimiwa Wabunge wamechangia kuhusiana na fidia kwenye maeneo oevu. Mpaka sasa hivi kwa upande wa Mkoa wa Kagera kwa ajili ya mradi wa kujenga mabwawa yale ya kutibu majitaka, tayari tumeshapeleka shilingi 1,800,000,000 kwa ajili ya kulipa fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Mkoa wa Singida tayari tumeshapeleka shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kulipa fidia kwa chanzo cha Mwankonko na chanzo cha Irawo tunaendelea kufanya tathmini ili baada ya kukamilisha basi tuweze kupeleka hela kwa ajili ya fidia. Kwa hiyo, nako naagiza, maeneo yote ya vyanzo oevu, tathmini ikishafanyika tunaomba mtuletea hati za fidia ili tuweze kuzipeleka Hazina ili kutupatia pesa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge pia wamechangia kuhusu madeni ya maji ambayo yanatokana na Taasisi za Serikali ambazo hazijalipa bili zao. Mpaka hapa tunapozungumza, tuna deni la shilingi bilioni 31, ukikusanya kwa mamlaka zote nchini. Sasa hivi tunafanya mazungumzo na Hazina na tayari wameonesha mwelekeo kwamba madeni haya watayalipa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja hii ilichangiwa pia na Mbunge wa Viti Maalumu wa Tabora, Mama yangu Mheshimiwa Munde, ambaye alionesha kwamba Mamlaka ya Maji ya Mkoa wa Tabora inashindwa kujipanua kwa sababu inadai taasisi za Serikali. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Munde kwamba sasa hivi Serikali inafanya utaratibu wa kuhakikisha kwamba sasa hivi fedha hizi zinalipwa ili hizi Mamlaka za Maji ziweze kuendelea kupanua mitandao ya maji kwa ajili ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge pia walichangia kuhusu tatizo la upungufu wa wataalam wa Mamlaka za Maji. Ni kweli tuna upungufu mkubwa wa wataalam kwa Mamlaka zote za Maji nchini. Kwa upande wa Wahandisi tunahitaji Wahandisi 6,282. Kwa sasa waliopo ni Wahandisi 1,538. Upungufu huu ni mkubwa, ni upungufu wa zaidi ya Wahandisi 4,744. Vilevile tunahitaji Mafundi Sanifu na Mafundi Mchundo 4,005. Waliopo ni 752 na upungufu ni 3,253.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto hiyo, Wizara tayari imeshachukua hatua zifuatazo; tuliomba kibali cha kuajiri watumishi 475, kwa bahati nzuri kibali hicho kimetolewa kwa hiyo kwa mwaka huu wa fedha tunaomaliza, tayari tumeajiri wataalam 475 na wameshasambazwa kwenye Mamlaka mbalimbali za Halmashauri pamoja na Mikoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto moja tunaipata tunapopeleka hawa wataalam; nitoe taarifa kwamba kuna baadhi ya Mikoa wamewakataa hawa wataalam, na Mikoa hiyo ni pamoja na RAS Dodoma, RAS Mbeya, RAS Arusha, RAS Dar es Salaam, Halmashauri za Manyara, Songea, Urambo na Geita. Hawana makosa kufanya hivyo kwa sababu na wao pia wanayo mamlaka ya kuajiri. Kwa hiyo, tunaona kwamba kama wamefanya hivyo, hao waliowarudisha tutawapeleka maeneo mengine ambayo wanahitajika. Kwa hiyo, tunaomba nao wachukue hatua ya kuajiri ili tusiwe na upungufu wa wataalam.
Mheshimiwa Naibu Spika, najua muda wangu mdogo, nimeshapigiwa kengele, lakini niliona nisimalize bila kuzungumzia maombi ya Mheshimiwa Mchengerwa, ambaye ameomba tuanze kufikiria, kutengeneza mradi wa kuchukua maji kutoka Mto Rufiji na kuyaleta Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2005 mawazo hayo yalikuwepo na Serikali ilichukua hatua kutafuta vyanzo 26. Vyanzo hivyo vilitembelewa lakini ikaonekana kwa mahitaji ya maji ya Jiji la Dar es Salaam na Miji ya Kibaha na Bagamoyo, vyanzo vilivyopatikana ambavyo viko karibu vina uwezo wa kulisha maji mpaka mwaka 2032. Kwa changamoto ambazo sasa hivi tunaanza kuzipata, tayari tunaanza kujipanga ili kuhakikisha kwamba tunaanza usanifu wa kutoa maji kutoka Mto Rufiji ili tuweze kukidhi mahitaji ya maji ya Mji wa Dar es Salaam; na hasa baada ya kuwa na kiwanda cha kuchakata gesi kwa ajili ya kutengeneza umeme, ambacho miaka miwili ijayo kitakuwa kinahitaji lita milioni 100 kila siku kwa ajili ya kupooza ile mitambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mchengerwa kwamba hatujatenga fedha katika mwaka wa fedha unaokuja, lakini wazo hili tunalichukua na taratibu pengine mwaka kesho kutwa wa fedha tutaanza kuweka fedha kidogo, kwa ajili ya kuanza kufanya upembuzi yakinifu.
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, nimalizie pia kwa kuzungumiza mradi wa maji wa kutoa Mto Ruvuma kuleta Mjini Mtwara Mikindani. Taratibu za kuongea na wafadhili zinaendelea vizuri na hivi ninavyoongea, wale Wachina, Wafadhili wenyewe wapo hapa Tanzania na mazungumzo yanaendelea vizuri. Kama hali itaendelea kama ilivyo, tunatarajia mpaka mwezi wa saba tunaweza tukawa tumesaini mikataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nanyamba ana vijiji kwenye chanzo cha huu mradi. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba vijiji vyako hivyo vitapewa maji pia kutoka katika huu mradi. Kwa bahati nzuri ni kwamba mtambo wa kutibu maji utajengwa kwenye chanzo. Kwa hiyo, wananchi wako watapata maji ambayo ni safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nisingependa nipigiwe kengele. Basi kwa haya machache, naomba niishie hapo, nashukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.