Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa hisani yako ya dakika tano. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge katika ku-support lile suala la kuongeza fedha kutoka petroli na dizeli na tukaomba kwenye simu vile vile ili Mfuko wa Maji uwe na fedha zaidi. Tatizo la maji ni kubwa na wote tunakubaliana kwamba Maji ni Uhai na ili fedha hizo zitumike vizuri ni vyema tukawa na wakala ambao utakuwa na wataalam na utasimamia kazi ya kuleta maji kwenye vijiji mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hilo nililoongelea, naomba niongelee kidogo juu ya Jimbo langu la Hanang. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri amekubali kuja kutembelea Hanang. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne aliahidi shilingi milioni 300, kwa ajili ya maji ya Mji Mkuu wa Hanang, Kateshi na zile fedha zikatolewa na kazi nzuri ikafanywa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naamini kuna tatizo la utaalam ambao kama litakuja kuangaliwa na Ma-engineer itasaidia na naomba Mheshimiwa Waziri anitumie watu kutoka Makao Makuu waje waone tatizo ni nini. Tunaamini kwamba gharama ni kubwa, lakini tunaweza tukafanya linalowezekana ili maji ya Kateshi yapatikane kwa uhakika na kwa gharama inayohimilika.
Mhesheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Hanang iko kwenye Rift Valley na sehemu kubwa iko kwenye mwinuko na ni mpakani na Singida. Hatuna maziwa isipokuwa ziwa la Basotu ambalo chanzo chake ni maji ya mvua, hatuna mto wa kudumu. Kule kwingine chini kwa ajili ya Rift valley kunakuwa na joto chini ya ardhi, kwa hiyo maji yako mbali, sisi hatuna maji. Maji yetu yanapatikana kwa visima au kwa mabwawa, hatuna mto, naomba sana kwa yale yaliyofanyika, nawashukuru lakini bado sehemu kubwa ya Hanang haina maji. Naomba awatume watu na yeye kuja Hanang ili basi maeneo yale ambayo hayana maji yaweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la maji Hanang ni kubwa kweli na jana tu jioni kulikuwa na watu wanalalamika kwamba wanapata maji kutokana na chanzo kimoja na ng‟ombe na hata wanyamapori. Kwa hiyo, naomba sana tuwatume watu na Wakala wa Maji Vijijini utasaidia kufanya surveys kwenye vijiji vyetu kwa sababu kila wakati hatuwezi kwenda kufanya kazi mara moja, kuchimba kisima kimoja. Ni vizuri kwa mfano Wilaya ya Hanang iliyo na tatizo la maji kwa ujumla Serikali ikaenda pale na kujua vyanzo mbalimbali na namna ya kuondoa matatizo ambayo yanawasibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Wabunge kwamba akinamama wanapata tabu sana na kutokana na akinamama kutumia muda mrefu kutafuta maji watoto wamekuwa wakiungua, watoto wamekuwa wakifanya utundu na kuumia na vile vile kazi zingine za nyumbani zimelala ukiacha sababu ya kwamba wanaume wanawa-accuse kwamba labda wanatumia muda kwenye mambo mengine kumbe wako misituni wanatafuta maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaombeni sana hili la wakala tulitilie mkazo kwa sababu watafanya kazi ambayo itajulikana na kutakuwa na mtu ambaye tunaweza kumnyooshea kidole kwa sababu Halmashauri hazina watu wenye uwezo na Halmashauri hazina capacity ya kuweza kuletea Wilaya mbalimbali au Majimbo yetu maji. Kwa hiyo, naombeni sana tuwe pamoja na na-declare interest kwamba ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maji, Kilimo na Mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa pamoja, tukiamua tuongeze fedha za kuchangia kutoka kwenye mafuta na vile vile kutoka kwenye simu na tukiwa na wakala tutakuwa tumeondokana na tatizo la msingi na tutakuwa na uwezekano mkubwa wa kuondoa tatizo la maji katika nchi yetu ikiwemo Wilaya yangu ya Hanang.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutaja vijiji ambavyo havina maji na ningependa kutaja miradi ambayo ina matatizo lakini muda hauko na sisi, na mimi na…
MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mtolea.