Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii kwa dakika tano hizi. Nami nichangie Wizara hii ya Maji. Sina wasiwasi na dhamira ya Mawaziri wote wawili wa idara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu ni hizi takwimu. Takwimu hizi tunazoletewa, nina wasiwasi nazo kwa sababu hapa takwimu inasema kwamba, wanaopata maji safi na salama imefikia asilimia 72, hapo ndipo wasiwasi wangu unapoanzia, ndipo hapo unapokuja umuhimu wa kuwepo na Mamlaka ya Maji Vijijini, kwa sababu najua hizi takwimu siyo wao wamezileta ila wao wameletewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano; kwenye jimbo langu tunapata maji kwa asilimia 47 katika mradi wa Vijiji 10, vile ambavyo World Bank walitoa fedha, sisi tumefanikiwa kupata vijiji vitatu tu ambavyo sasa maji yanapatikana. Katika vijiji 76, tumepata vijiji vitatu tu, ambavyo ni Vijiji vya Mpigamiti, Mbaya na Barikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, kulikuwa na mradi wa kutafuta chanzo cha maji kwa ajili ya maji ya Liwale Mjini. Palitolewa pesa, shilingi milioni 200, lakini katika zile pesa, mpaka sasa hivi shilingi milioni 55 zimeshatumika na bado chanzo mbadala cha maji hakijapatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 20 zimetumika katika kutafuta chanzo cha maji katika Mji wa Makunjiganga lakini maji hayajapatikana. Shilingi milioni 35 zimetumika katika Kijiji cha Mikunya, pale kumepatikana maji ya lita 5,000 kwa saa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya Wilaya ni lita 25,000 kwa saa. Kwa hiyo, Mkandarasi Mshauri akasema, pampu ile sasa ifungwe kwa ajili ya Vijiji vya Mikunya na Liwale „B‟. Kwa hiyo, chanzo cha maji katika Liwale Mjini bado ni kitendawili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, tulikaa kwenye kikao cha Halmashauri, tukawashauri, badala ya hizi pesa kuendelea kutafuta vyanzo, zitakwisha shilingi milioni 200 bila kupata chanzo mbadala. Tukaiagiza Halmashauri sasa ifanye utaratibu mwingine labda tutafute kuchimba mabwawa; labda tuvune maji kwa mabwawa badala ya kuendelea kutafuta vyanzo mbadala kwa sababu hakuna mahali ambapo itachimba, utapata maji yenye ujazo wa lita 25,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, tuna Vijiji vifuatavyo ambavyo kwa shida ya maji iliyopo Liwale, watu wanahama kuanzia asubuhi wanarudi jioni na ndoo moja. Vijiji kama Kichonda, Kipule Magereza, Kiangara, Mbumbu, Nangano, Kikulyungu, Mkutano, Miluwi na Makata; hivi vijiji watu wanaamka asubuhi, wanarudi jioni na ndoo moja. Sasa ninapoambiwa kwamba kuna asilimia 72 ya watu wanaopata maji, napata wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye miradi ya umwagiliaji; tunayo miradi miwili ya umwagiliaji katika Jimbo langu. Kuna mradi wa Ngongowele. Ule mradi wa Ngongowele umeshakula pesa zaidi ya shilingi bilioni moja mpaka sasa hivi zimeteketea na ule mradi umesimama. Tulipokwenda kuwafuata pale, Mkandarasi Mshauri anasema ili huu mradi uweze kuendelea, panatakiwa bilioni nne ili uweze kutumika masika na kiangazi. La sivyo, utumike kwa masika tu, panahitajika shilingi milioni 800.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ule mradi kutumika masika tu, wanakijiji hawako tayari. Wanasema kama mradi unatumika masika tu, sisi masika tunalima. Sisi tulivyokubali huu mradi lengo lilikuwa utumike masika na kiangazi. Kwa hiyo, hata kama zitapelekwa shilingi milioni 800 leo, ule mradi wanakijiji hawako tayari kuupokea kwa sababu hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi wa Mtawango, nashukuru Alhamdulillah kwamba sasa hivi unaendelea vizuri, umefikia asilimia 95. Ushauri wangu, kama ambavyo wachangiaji waliotangulia walisema, kweli tunahitaji Mamlaka ya Maji Vijijini kwa sababu hawa Wakandarasi na Wasimamizi wa miradi hii Vijijini hakuna wasimamizi wa kutosha. Kwa ilivyo jiografia ya Liwale, juzi nilikuwa naongea na Naibu Waziri, nafikiri; ameshindwa kufika Liwale kukagua ile miradi miwili kwa sababu ya jiografia ya Liwale, hakufikiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Liwale tunakwenda sisi tunaokujua, lakini kwa watu kama Mawaziri kama ninyi kufika Liwale inakuwa ni shida. Sasa itakapoundwa hii Mamlaka ya Maji nafikiri hawa ndio wanaweza kufanya usimamizi huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hivyo tu, katika Halmashaui ya Wilaya ya Liwale, tunao uhaba wa mafundi kwa maana ya wataalam. Mtaalamu aliyepo pale mwenye cheti ni mmoja tu, wengine wote waliopo ni mafundi wa spana tu wa mitaani. Kwa hiyo, hili nalo ni tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii miradi ya vijiji hivi vitatu nilivyovitaja, kuna kijiji kimoja kisima kimechimbwa; Kijiji cha Kiangara, kijiji hiki maji ni ya chumvi, hayatumiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri, nimeona kuna shilingi milioni 300 nyingine zimetengwa hapa. Naendelea kusisitiza kuhusu usimamiaji wa hizi fedha. Kama tusipopata usimamizi wa kutosha, kitakachotokea ni hiki hiki ambacho kimetokea kwenye hizi shilingi milioni 200 za awali na hii miradi ya kwanza Vijiji 10 na badala yake tukaambulia vijiji vitatu tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, naomba kwa sababu nilipewa tu dakika tano na shida yangu ilikuwa ni hiyo tu, naomba niishie hapo. Ahsanteni sana.