Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mboni Mohamed Mhita

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata fursa ya kuweza kuchangia katika suala zima la maji. Awali ya yote, naomba nitumie fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini kwa kunichagua kwa kura nyingi na za kishindo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nijikite moja kwa moja kwenye adha ya maji katika Jimbo Handeni Vijijini. Maji ni tatizo sugu katika Jimbo la Handeni Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa ni mtoto wa kike, nateseka sana kushuhudia akinamama wakitembea umbali mrefu kuhangaika kwenda kuyafuata maji. Naamini kwamba, moja ya sababu kuu ya akinamama kujitokeza sana kwenye uchaguzi huu kunipigia kura ni matumaini makubwa kwamba mtoto wa kike basi nitakuwa mstari wa mbele kwenye kuhangaika kuhakikisha kwamba adha ya maji inaisha ama kupungua katika Jimbo la Handeni Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite moja kwa moja katika mradi wa HTM (Handeni Trunk Main). Mradi wa HTM ndiyo mradi ama ndiyo chanzo kikuu cha maji katika Jimbo la Handeni Vijijini. Nina hakika mradi huu ukitiliwa nguvu zaidi shida ya maji kwa wananchi wa Handeni Vijijini itakwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu ulitengenezwa mwaka 1974 ukiwa na tegemeo la kuwa na life span ya miaka 20. Hivyo basi, tangu mwaka 1994 miundombinu ya mradi huu ni chakavu na hakika wananchi wa Handeni Vijijini wanateseka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu ulianzishwa ukiwa na lengo la kuweza kuhudumia vijiji 60 na sasa hivi Jimbo la Handeni Vijijini lina vijiji 122. Hivyo basi, ni dhahiri kwamba kuna ongezeko kubwa sana la wananchi. Mahitaji ya kuweza kufufua huu mradi ni USD milioni 84.4. Nimeona hapa kwamba Wizara inategemea Euro milioni 60 kutoka BAM International ya nchini Uholanzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya mradi huu kwa mwaka 2016/2017. Hivyo basi, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nguvu ya ziada iongezwe ili hizi Euro milioni 60 ambazo zinategemewa kutoka BAM International ziweze kupatikana; kwa sababu hakika mradi huu ukiweza kufanyiwa kazi, basi hakika Jimbo la Handeni Vijijini na Handeni nzima kwa ujumla adha ya maji itakwisha kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Jimbo la Handeni Vijijini tulibahatika kupata mabwawa matatu chini ya mradi wa World Bank.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bwawa la kwanza lipo Manga, lingine Mkata na la tatu liko Kwandugwa; mabwawa ambayo tulitarajia ndani ya miezi sita yaweze kuwa yamemalizika, lakini mpaka nasimama hapa, huu ni mwezi wa 30 na bado yale mabwawa hayajamalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, basi tumwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, fedha ziweze kuelekezwa kwenye miradi hiyo ili wananchi wa Manga, Mkata na Kwandugwa waweze kuondokewa na shida na adha hii ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niishie na ahadi kwa wananchi wa Handeni ambayo ilitolewa na Rais wa Awamu ya Nne ya mradi wa Wami Chalinze, mradi ambao kwa namna moja ama nyingine ungepunguza adha ya maji kwa wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini, tukiwa tuna maana kwamba mradi huu wa Wami, Chalinze ambao uko kwenye Jimbo la jirani, kaka yangu Ridhiwani Kikwete ametoka kulizungumzia sasa hivi, angeweza kutuvutia maji mpaka Manga na maji yakifika Manga, basi hakika yamefika Mkata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, basi naomba pia Mheshimiwa Waziri aweze kutukumbushia kwa sababu Handeni Vijijini bado tunaingoja ahadi hii; tunangoja utekelezaji wa hii ahadi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.