Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii nzuri ya Wizara ya Maji ambayo ninaamini maji ni uhai maana yake uhai wa Wana-Chalinze unaanzia kwenye hotuba hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru maana nasema usiposhukuru kwa kidogo huwezi kushukuru kwa kikubwa utakachopewa. Mheshimiwa Waziri na Wizara yake wametufanyia makubwa sana katika Jimbo la Chalinze, Mradi wa Maji wa Chalinze pamoja na kukwama kwake kwa mara kwa mara kunakotokana na tatizo la mazingira yetu kuharibika mara kwa mara inapofika hasa kipindi cha mvua, lakini siku zote wamekuwa pamoja na sisi kuhakikisha kwamba wanakabiliana na changamoto hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni bomba lilikatika pale karibu na kijiji cha Chalinze Mzee, Mheshimiwa Waziri alitutafutia kiasi cha shilingi milioni 90 kurekebisha miundombinu ile ndani ya muda wa siku mbili, tatu. Kwa kweli binafsi ndiyo maana ninasema kwamba nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri. Siyo hilo tu, hata pale Kihangaiko ilipotokea uwezo wake wa ku-react mapema zaidi na haraka kwa kweli binafsi yangu unanipa nafasi ya kuunga mkono hoja yake hata kama mambo yaliyopo humu ndani wengine wanaona kwamba hayatotekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kuchangia katika eneo la utekelezaji wa Mradi wa Maji Awamu ya Tatu wa Chalinze. Pamoja na mambo mazuri yaliyoandikwa katika kitabu pia pamoja na mazuri ambayo yamekwishaanza kutokea pale Chalinze, nina jambo moja la kushauri Mheshimiwa Waziri na hili jambo naomba sana utakapo kuja kutoa majibu yako ni vema ushauri wangu huu ukauweka kama kipaumbele sana kuliko yanayoendelea kufanyika sasa hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua fedha zimekwishatolewa zaidi ya shilingi bilioni 21 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa awamu ya tatu, ambao umetengewa dola milioni 41 ambazo zinatarajiwa kutumika katika kipindi hiki, lakini lipo tatizo ambalo naliona kwamba ujenzi wa awamu ya tatu umeanza katika kujenga matanki kwa ajili ya kuhifadhia maji. Tatizo kubwa tulilonalo Chalinze ni kwamba kila inapofika kipindi cha mvua Mheshimiwa Waziri unafahamu vizuri chanzo kinaharibika, matope yanajaa katika chanzo matokeo yake watu wa Chalinze hawapati maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri busara kubwa ziadi ungeielekeza kwenye kujenga lile tanki kubwa la kuhifadhia maji pale kwenye chanzo ili hata kama ikitokea hali hiyo baadaye yale maji yatakayokuwa yamehifadhiwa pale, ambayo kwa estimation zilizoandikwa humu ndani tanki litakuwa na uwezo wa kubeba lita zisizopungua milioni 11 maana yake ni kwamba watu wa Chalinze wanaweza wakanywa lita hizo milioni 11 wakati wanasubiri mambo yakae vizuri katika chanzo kile. Unapoamua kujenga matanki, halafu maji yakachafuka tena Mheshimiwa Waziri nataka nikuambie watu wangu wa Chalinze wataendelea kupata taabu wanayoendelea kuipata sasa na hivyo utakuwa hujawawezesha katika kutatua tatizo lao linalowakabili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo katika kitabu chako cha bajeti Mheshimiwa Waziri umezungumza juu ya usalama wa maji yetu. Mimi ninakushukuru sana kwa sababu kama maji hayatokuwa salama maana yake hata wanywaji wenyewe hali yetu nayo itakuwa ni mbaya sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo unapozungumza usalama wa maji pia huwezi kuepuka kuzungumzia usalama wa miundombinu yake. Kwa sababu yapo mambo yanayotokea katika maendeleo ya kibinadamu ambayo yanaharibu miundombinu na hata wakati mwingine hayo maji safi na salama tunayotarajia kuyapata hatuyapati katika muda. Kwa mfano, Chalinze Mjini katika kijiji cha Chalinze Mzee upo mradi uliokuwa unafanyika wa ujenzi wa nyumba, mtu amepima viwanja vyake vizuri lakini walipopewa kibali cha kuanza kukata viwanja yule mkandarasi aliyekwenda kutengeneza pale alivunja bomba.
Mheshimiwa Waziri unakumbuka ilikulazimu mwenyewe uje pale ili uone jinsi uharibifu ule ulivyofanyika. Sasa kama itakuwa kazi yetu tunatengeneza usalama tu wa maji, hatuangalii usalama wa miundombinu itakuwa kila siku unakuja Chalinze kama siyo kila siku unakwenda na maeneo mengine huko Geita na maeneo mengine ukihangaika. Sheria ziwekwe kwamba mtu anapopewa haki za kuendeleza maeneo basi pia haki hizo ziendelee na kulinda miundombinu ya maji yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, kipekee kabisa nizungumze katika Mradi wa Wami-Chalinze kulikuwa na extension ya maji inayotoka Wami inayotakiwa kufika hadi Mkata kwa upande wa Handeni Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua katika bajeti hii haijapangwa, hivyo ningeomba sana mnapojaribu kuangalia uendelezaji wa mradi huu ni vema pia jambo hili mkaliangalia kwa sababu watu wa Mkata kwa upande wa kupata maji ni rahisi sana kuchukua maji kutoka Chalinze kuliko kuchukua kutokea kwenye Mji wa Handeni Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali muangalie juu ya mradi wa maji wa Ruvu, mmetengeneza mradi wa maji mzuri wenzetu wa Dar es Salaam wanaendelea kufaidi na maji hayo lakini kibaya zaidi ni kwamba wananchi wa Ruvu kwa maana ya Mlandizi pale hawana maji. Ni aibu sana lakini ni jambo ambalo Wizara inatakiwa iliangalie. Natambua kwamba yapo marekebisho yanayofanyika sasa kwa ajili ya kuhakikisha mradi wetu huu wa Ruvu unaendelea kuwa efficient zaidi kwa ajili ya wananchi wa Miji ya Dar es Salaam, Kibaha na maeneo mengine. Lakini pia kuangalia sasa upatikanaji wa maji katika Mji wa Mlandizi na viunga vyake ni jambo la msingi sana ili watu hawa waliochagua Chama cha Mapinduzi waendelee kufaidika na uwepo wako Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Pia katika Mradi huo wa Ruvu lipo bomba linalotoka pale kwenye chanzo chetu cha Ruvu linafika mpaka kwenye Ruvu Ranch kwa maana ya pale kwenye mradi wetu ule wa Ruvu. Mheshimiwa Waziri lakini mradi ule ukiutazama kwa sura yake umezungukwa na vijiji vinavyotengeneza Kata ya Vigwaza, vijiji hivi mpaka leo bado vinalalamika kwamba havina maji na vimeendelea kupata maji kutoka Chalinze katika mwendo wa kusuasua. Nashauri kwamba sasa bomba hili tuweze kuwekea zile wanasema „T‟ ili maji yaweze kufika katika vijiji kama vya Kidogonzelo, Vigwaza yenyewe, Milo, huko kote watu waweze kufaidika na mradi huu ili mambo ya kuendelea kukithamini Chama cha Mapinduzi iendelee kufanyika. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, mwisho siyo kwa umuhimu sana ni maji Rufiji. Mheshimiwa Waziri natambua katika kitabu chako cha orodha hii ya miradi hujatuonyesha juu ya mradi huu, natambua kwamba mradi huu unaweza kuwa haupo katika kipindi hiki, lakini wananchi wanaoishi katika vijiji kama vya Ikwiriri, Utete, Mkuranga, Kisarawe na Temeke kwa maana ya upande wa Dar es Salaam wanategemea sana mradi huu ukiweza ku-mature ili mambo yao ya maji yaendelee kuwa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii katika mji kama wa Temeke watu wanakosa maji wakati mwingine kwa sababu maji yao mengi wanategemea kutoka Ruvu na wakati mwingine mradi huu unapozidiwa basi matatizo yanakuwa makubwa sana. Naomba sana Mheshimwia Waziri utakapokuja kujibu at least useme neno juu ya mradi huu ambao ndiyo utakuwa suluhu ya maisha ya watu wa Rufiji, Mkuranga, Kisarawe na maeneo ya Dar es Salaam kwa ajli ya kupata mahitaji yao makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo wapo wenzetu ambao wanafanya ujenzi wa bwawa la Kidunda. Mheshimwia Waziri ninakushukuru kwa kuonesha kwamba ndani ya bwawa la Kidunda upo mradi wa umeme ambao utafika mpaka Chalinze, pia kama ipo fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya kufikisha umeme Chalinze kwa nini sasa tusianze kufikiria badala ya maji yote kuelekezwa Dar es Saalam basi maji haya yapelekwe Chalinze ili wananchi hwapate nao kufaidika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, distance ya kutoka Kidunda panapochimbwa lile bwawa lenyewe mpaka Chalinze Mjini hapazidi kilometa 32 lakini kutoka Kidunda pale mpaka Dar es Salaam tunatarajia kwamba zitafika kilometa zaidi ya 68. Mheshimiwa Waziri ni vizuri ukaangalia kwamba miradi hii iwe inafaidisha pia watu wako, tunakushukuru kwa umeme lakini pia tunaendelea kukushukuru kwa kazi kubwa unayoendelea kuifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho la kuzungumza japo kuwa nilisema kwamba siyo la mwisho kwa umuhimu lile la Kidunda ni jambo la upatikanaji wa fedha..
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba fedha zifike haraka. Naunga mkono hoja, ahsante.