Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kukushukuru nami kuwa miongoni mwa Wabunge ambao wanachangia hotuba hii ya Waziri wa Maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji, Naibu wake na watendaji wa Wizara ya Maji kwa jinsi ambavyo mnafanya kazi sasa kwa kujituma ili Watanzania waweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Wabunge wengine wanaosema kwamba tatizo siyo Waziri, tatizo ni upatikanaji wa fedha katika Wizara hii. Katika bajeti ya mwaka jana 2015/2016 ni asilimia 19 tu ya fedha ambazo zilipangwa kwenda Wizara hii zilipelekwa. Niwaeleze Waheshimiwa Wabuge kwamba hata hizi fedha mnazoziona sasa hazitokani na fedha za miradi ya maendeleo zilizopangwa, hizi ni fedha zinazotokana na Mfuko wa Maji ambao Waheshimiwa Wabunge tuliopita tuliuanzisha mfuko huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kama kweli tunataka maji yapatikane na tuweze kupata fedha zetu kutoka Wizara ya Fedha bila vikwazo ni lazima tuongeze fedha kwenye Mfuko wa Maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imetoa ushauri na mapendekezo kwamba angalau mwaka huu tozo ya kwenye mafuta kutoka shilingi 50 iwe shilingi 100, kwa hakika Waheshimiwa Wabunge, tuunge mkono hili ili tuhakikishe Mfuko wa Maji unapata fedha za kutosha, hizi ndiyo fedha za uhakika ambazo zinaweza kututoa na kutuhakikishia kwamba tunapata maji katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna asiyejua umuhimu wa maji katika Taifa letu, maji ni muhimu na hapa Mheshimiwa Gekul amesema maji kwanza na kwa vyovyote vile lazima tuhakikishe kwenye bajeti hii tunapata fedha za kutosha ili fedha zipelekwe kwenye miradi na tunapata maji katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye Jimbo langu la Lulindi, kwanza ninaishukuru sana Wizara kwa kuutengea fedha mradi wa Chiwambo, ambao upo kwenye Jimbo langu la Lulindi kule Masasi, bahati mbaya mradi huu hii ni bajeti ya tatu mradi haujakamilika, ni imani yangu Serikali hasa Wizara kwa kipindi kilichobaki cha miezi miwili kuelekea mwisho wa bajeti na ziko kila aina ya dalili kwamba Wizara ya Fedha huenda ikakusanya kufikia asilimia 100 kwa fedha za ndani. Ningeomba mradi huu sasa ukamilike ili wananchi wa Kata saba na vijiji zaidi ya 30 waweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo miradi ya vijiji kumi ambapo kila Jimbo tunalo, kila Mkoa ipo. Katika Jimbo langu kuna mradi wa Chipingo, mradi wa Shaurimoyo, mradi wa Mkululu, ningependa kuona miradi hii Wizara inaitekeleza ili kuhakikisha kwamba wimbo wa vijiji kumi au mradi wa vijiji kumi sasa unakwisha ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijaona kwenye miradi ya umwagiliaji katika Mkoa wetu wa Mtwara, nina uhakika hata Mkoa wa Lindi, ningeomba tuhakikishe kwamba tunakuwa na scheme za umwagiliaji kandokando mwa Mto Ruvuma, maji ni mengi, yote yanaingia baharini, ni imani yangu kabisa kwamba Wizara tukijipanga vizuri kwenye suala la umwagiliaji, kilimo kinaweza kukuzwa kandokando ya Mto Ruvuma na kuwafanya wananchi wanaoishi katika Mikoa hii hasa kandokando ya Mto Ruvuma wanufaike na kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie kwamba wote tunakuombea na Wizara tunaiombea ili ikamilishe azma ya kuhakikisha kwamba kila eneo ambalo linahitaji maji liweze kupatiwa maji. Hata tunapozungumzia suala la viwanda, maendeleo ya kilimo, suala la maji ni la kipaumbele cha kwanza. Kwa hiyo, Wizara ijipange upya ihakikishe kwamba inakuwa na usimamizi bora wa fedha zinazopelekwa kwenye Halmashauri. Hivi sasa miradi ile inasimamiwa na Halmashauri kwa asilimia kubwa zaidi kuliko Wizara, ninaomba Wizara iweke kitengo cha usimamizi wa miradi ya maji katika Halmashauri zetu, isisitize suala la ubora wa vifaa vinavyonunuliwa kwenye suala zima la maji. Kwa sababu yako maeneo, miradi imefanyika, lakini inadumu kwa muda mfupi kwa sababu vifaa vilivyotumika, mabomba, viunganishi na mambo mengine yanakuwa hayako katika kiwango kinachostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na fedha hizi zinazotengwa tunapeleka kule safari hii zaidi ya shilingi bilioni 900, lakini kama hakuna usimamizi, na hakuna uangalifu kuhakikisha kwamba vifaa vinavyonunuliwa vinakuwa kwenye kiwango kinachostahili, hakika hatuwezi kupata mafanikio kama tunavyotarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie pia mradi mkubwa ulioko Masasi, mradi wa Mbwinji. Mradi huu umeigharimu Serikali zaidi ya shilingi bilioni 51, ningeomba shilingi bilioni moja iliyotengwa kila mwaka ihakikishe ile shilingi bilioni moja ipelekwe, tunataka tuone kwamba katika bajeti hii inayoishia ya 2015/2016 kiasi kile cha shilingi bilioni moja kilichopangwa kiende ili kiweze kufanya kazi ya kusambaza maji vijijini.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niyaeleze hayo lakini msisitizo mkubwa ni kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kwa kauli moja tuhakikishe tunaunga mkono, suala la kuongeza shilingi 100 ili iwe tozo ya kuhakikisha kwamba tunapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono kwa asilimia mia moja.