Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia katika hoja hii.
Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja na timu yao nzima, kwa kazi nzuri wanayoifanya na kwa hotuba nzuri waliyoitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba nafarijika sana kwamba kama Taifa, sasa tumefika tuna mjadala kuhusu matumizi ya rasilimali ya asili, ikiwemo ardhi kwa maendeleo yetu. Nafarijika kwamba sasa tuna mjadala kuhusu uhusiano kati ya mazingira na maendeleo, naamini kwamba mjadala huu unaweza kufanywa kwa busara, kwa hekima, bila jazba, wala vitisho ili tuweze kupata muafaka katika jambo hili muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, toka awali ni kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya wakulima, Serikali ya wavuvi, Serikali ya wafugaji, Serikali ya watu wanaofanya shughuli zote katika nchi hii. Asiondoke mtu na dhana hapa, kwamba Serikali ya Awamu ya Tano au Waziri katika Serikali ya Awamu ya Tano anapendelea kundi moja au lingine katika Taifa letu. Hilo siyo kweli na halipo tumechaguliwa na watu wote, tumechaguliwa na kura za Watanzania wote.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1961, kwenye Mkutano uliofanyika Arusha mwezi Septemba, Rais wa Tanganyika wakati ule Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alitoa hotuba ambayo ndiyo iliweka msingi wa uhifadhi ambao tunaendelea nao leo, Mwalimu Nyerere alisema, inaitwa Arusha Manifesto, kipande kimoja kizuri sana ambacho kwa kifupi kilisema, kwamba sisi kama Taifa tumepewa dhamana ya kuhifadhi wanyama pamoja na maeneo ambayo wanyama wanaishi na tumepewa dhamana hiyo kwa ajili ya enjoyment ya hivyo vitu, lakini pia kwa sababu ya uhai na maisha yetu yanayokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi wa misitu na uhifadhi wa wanyamapori, siyo kwa ajili ya misitu, siyo kwa ajili ya wanyamapori peke yake. Hifadhi ya misitu na hifadhi ya wanyamapori una uhusiano wa moja kwa moja na upatikanaji wa mvua na upatikanaji wa mvua, una uhusiano wa moja kwa moja na maendeleo ya kilimo, upatikanaji wa mvua una uhusiano na upatikanaji wa malisho. Kwa hiyo, hifadhi ya misitu ina uhusiano na ustawi wa ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, misitu inatoa huduma za kiikolojia ambazo zinafanya nchi yetu ipumue. Sasa hapa kumekuwa na mjadala, kana kwamba uhifadhi na ufugaji ni kama lila na fila hazifungamani. Uhifadhi na ufugaji siyo dichotomous, tunaweza kufanya vyote kwa wakati mmoja na tukafanya vizuri kabisa. Kuna dhana inajengwa kwamba hapa kuna ukinzani kati ya ufugaji na utalii. Msingi premise ya huo mjadala siyo sahihi. Kama Taifa tuna uwezo wa kufuga na kunufaika na ufugaji na tuna uwezo wa kuhifadhi na kunufaika na manufaa ya uhifadhi. Isijengwe dhana kwamba hizi ni shughuli zinazokinzana kwa hiyo lazima tuchague moja siyo kweli, kwa miaka yote tumekuwa tunafanya mambo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio sahihi cha wafugaji ni kwamba, kila mfugaji apatiwe eneo na amilikishwe eneo la kufuga, kilio sahihi cha wakulima ni kwamba kila mkulima apatiwe eneo na amilikishwe na hii ndiyo ahadi yetu Chama cha Mapinduzi, kwamba kila mfugaji na kila mkulima atamilikishwa eneo lake ili wafanye shughuli zao kwa tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo cha migogoro inayozungumzwa siyo shughuli watu wanazofanya. Chanzo cha migogoro inayozungumzwa ni kwamba maeneo haya hayakupimwa na ndiyo maana Waziri Mheshimiwa Lukuvi alikuja katika hotuba yake na mpango mkubwa wa matumizi ya ardhi pamoja na upimaji wa ardhi ambao utapelekea kupunguza migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha msingi sisi kama Taifa ni kwamba shughuli zile ambazo tunaamini zinaharibu mazingira ni lazima zifanyike kwa tija. Inawezekana kabisa kwamba kwenye kilimo, katika heka moja kama tutaweza kupata tani nyingi zaidi za mahindi, basi haihitajiki ardhi kubwa zaidi ili kuweza kupata manufaa. Vilevile katika ufugaji inawezekana kabisa kwamba ukafuga katika eneo na hautalazimika kutafuta eneo lingine lakini ukanufaika na manufaa ya ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ufugaji udumu kwa miaka 100 ijayo, lazima tuhakikishe kwamba tunalinda kile tunaita natural capital. Katika dunia hii nchi zinatofautiana na utajiri wa rasilimali asili. Tanzania tunayo, inawezekana hatuna mtaji mkubwa wa kifedha, lakini tunao utajiri mkubwa wa natural capital, tunaweza tukaamua hapa Bungeni kwamba basi tufuge vizuri kwa miaka 20 ijayo, lakini baada ya hapo hakuna ufugaji tena, hakuna kilimo tena na hakuna mazingira tena. Kwa hiyo, katika mambo ambayo Serikali inayapanga kuyafanya, ni kuhakikisha kwamba shughuli hizi watu wetu wanazofanya zinadumu katika miaka mingi ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu mfumo wake wa kiikolojia una mito na mabonde mengi ambayo ndiyo yanafanya maisha yetu yawezekane, tunayo mito mikubwa Mto Pangani, Mto Ruvu, Mto Ruaha na mingineyo. Sehemu kubwa ya vyanzo vya mito hii ni kwenye maeneo yaliyohifadhiwa. Tukitaka Taifa letu life, mito hii itoweke, mabonde haya ambayo yana-sustain uhai wetu yatoweke, basi tusijali hifadhi ya misitu na hifadhi ya maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja kwamba watu wameongezeka, mifugo imeongezeka, kwa hiyo basi tugawe. Ukweli ni kwamba kwa sababu hiyo kwamba watu wameongezeka ndiyo uhifadhi unahitajika zaidi. Katika nchi ndogo kisiwa Uingereza wamehifadhi asilimia 25 pamoja na kuwa na tatizo kubwa la ardhi katika ile nchi, asilimia 25 imehifadhiwa na bado maisha yanaendelea nasi kadri tunavyoendelea kama Taifa, shughuli zetu zitakuwa za tija zaidi na zitaondoka katika matumizi ya ardhi zaidi, na tutaweza ku-sustain maisha yetu bila shaka yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hapa bila shaka yoyote, kwamba binadamu ndio tunasemekana kwamba ni wanyama wenye akili kuliko wanyama wote. Tukishindwa kuhifadhi rasilimali asili, zinazowezesha maisha yetu leo, tukishindwa kuhifadhi rasilimali asili kwa watoto wetu na wajukuu wa wajukuu wetu, basi heshima yetu binadamu kama mnyama mwenye akili kuliko wote itabidi itiliwe shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja kwa kusema kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inawajali wakulima na wafugaji katika usawa wao. Serikali ya Awamu ya Tano haipo hapa kusema shughuli hii ni bora kuliko shughuli ile nyingine, ili mradi shughuli inaendesha maisha ya watu wetu kwetu ni shughuli muhimu na tutahakikisha kwamba wanayoifanya wananufaika. Wakati huo tunahifadhi nchi yetu kwa sababu sisi tumekabidhiwa tunapita, kuna wajukuu wetu na wajukuu wa wajukuu zetu watakuja kupita, na watakuja kutushangaa, kwamba urithi tuliopewa sisi tulioachiwa na waliotuachia nchi hii, tumeuharibu kana kwamba ndiyo watu wa mwisho kuishi katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.