Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri Mheshimiwa Maghembe, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Maofisa Watendaji wa Wizara hii kwa hotuba nzuri na mipango mizuri ya kuboresha shughuli za Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ina vivutio vingi vya utalii, lakini kwa uzoefu wa muda mrefu utalii huu umeonekana kuwa ni kwa ajili ya wageni tu wanaokuja Tanzania kufanya ziara za utalii nchini. Iko haja sasa kwa Wizara kuhamasisha utalii wa ndani ili na Watanzania nao wafaidi utalii na Taifa lipate kipato kutokana na hili. Serikali iweke mikakati mahsusi ya kuwavutia Watanzania wengi zaidi kushiriki katika utalii wa ndani. Makundi mbalimbali ya kijamii yawekewe vivutio na mikakati ya kutembelea maeneo ya utalii. Wizara kupitia Maofisa Maliasili waandae ratiba katika maeneo waliyomo ili watembelee vivutio vilivyo karibu na maeneo yao. Hii itajenga utumiaji wa utalii kidogo kidogo hadi hili lizoeleke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wapewe hamasa wakatembelee vivutio hivyo pamoja na kupanda Mlima Kilimanjaro na kufaidi mlima wetu ulioliletea sifa kubwa Taifa letu. Niwahimize Serikali kuwekeza kwenye matangazo ya ndani kwa kutangaza vivutio vilivyomo nchini ili wananchi watamani kuvitembelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuibua mazao mengine tofauti ya utalii ili kuvutia utalii zaidi, kushirikisha maeneo mengi zaidi na wadau wengi nchini kwenye shughuli za utalii na kujenga ajira na kuongeza mapato ya wananchi na Taifa kwa ujumla maeneo mengi ya Tanzania hasa ya milimani, kwenye maporomoko ya maji kuna fursa nzuri ya utalii wa jiografia kama mountain trekking, hiking, photographic tourism, cultural tourism na kadhalika. Utalii huu unaofanywa na jamii, vijiji na watalii wanapendelea kujifunza juu ya maisha yetu na utamaduni wetu. Ileje na Mkoa wa Songwe kwa ujumla wana fursa nyingi za cultural geographic tourism na Serikali iangalie jinsi ya kuboresha aina hii ya utamaduni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ina misitu yenye aina ya nyani wa kipekee black and white collobus ambaye hapatikani sehemu nyingine yoyote. Mapori ya Kitulo yana aina ya maua ya orchids ambayo aina yake hazipatikani sehemu nyingine yoyote. Songwe, Mbeya na Nyanda za Juu Kusini kuna fursa nyingi sana za utalii kuanzia Udzungwa, Ruaha, vinajenga utalii wa Southern circuit, kwa hiyo Serikali sasa ihamishe nguvu kwenda kuendeleza utalii katika Southern circuit na ijumuishe aina zote za utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa ya Songea na Mbeya wana utamaduni wa ngoma za kimila nzuri sana ambazo zingeweza kuwa sehemu ya utalii wa kiutamaduni. Hii ni fursa ya ajira kwa wananchi na mapato kwa Taifa. Nataka kuhamasisha Serikali kupitia Maofisa Maliasili wa Wilaya kuhakikisha kuwa wanaanza kuangalia utalii vilevile kwenye maeneo yao badala ya kujikita kwenye magogo na mazao ya misitu peke yake.
Watanzania wenzangu tubadilike na tuanze kushiriki utalii wa ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bajeti ya utangazaji wa utalii ni ndogo sana Tanzania ukiilinganisha na nchi jirani. Changamoto kubwa ya kukua kwa utalii nchini ni kukosa kufanya utalii vya kutosha. Vivutio vya utalii vitangazwe zaidi kwa watalii wa ndani na wa nje ili vivutio vifahamike na watalii waongezeke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii ni ndogo sana ukiitazama kuwa Tanzania inaongoza kwa vivutio vya utalii na kuliingizia Taifa pato kubwa. Inasikilitisha sana kuwa bajeti ya Wizara hii ni ndogo wakati Taifa linategemea sana sekta hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya utalii haipo kwenye mpango wa BRN pamoja na sekta hii kuchangia pato kubwa la Taifa. Hii ni hitilafu kubwa na inatakiwa irekebishwe haraka na Serikali itoe tamko juu ya mikakati yote hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna haja ya kuongeza uwekezaji katika vivutio vya utalii kwa mfano kuna huduma hafifu hasa vituo vya kufikia watalii kama hoteli, huduma ya kwanza kwenye vivutio kama Mlima Kilimanjaro. Huduma ya vyoo vizuri na sehemu za kupumzika. Gharama za kupanda Mlima Kilimanjaro ni kubwa na wananchi wa kawaida watashindwa kufaidi. Upatikanaji wa chupa za oxygen karibu na kileleni, kuwezesha Watanzania kuwekeza kwenye miradi ya utalii katika ngazi zote Wilayani. Serikali itoe tamko juu ya mkakati wa kuendeleza utalii katika ngazi ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ufinyu wa bajeti bado Bodi ya Utalii haifanyi kazi kwa kujituma, ubunifu wa maarifa yako mengi wangeweza kufanya kwa kutangaza utalii kwa kushirikisha wadau kwenye maonyesho ambayo watalipia wenyewe au kutumia fursa za maonyesho mengine na mikutano mikubwa ya Kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itoe kipaumbele kwenye kujenga miundombinu mizuri katika maeneo ya kitalii. Serikali imefanya nini katika mbinu kuhakikisha wanaweka kipaumbele kuonesha miundombinu ya biashara na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kupendekeza kuwa Serikali iondoe kwa miaka mitatu kodi na ushuru kwenye uwekezaji katika mahoteli ya kitalii, kuruhusu wawekezaji kujenga hoteli za kitalii za kiwango cha nyota tatu hadi tano. Katika kipindi chote cha ujenzi mwekezaji asitozwe chochote akimaliza na uendeshaji ukiaanza atozwe asilimia 15 mwaka wa kwanza na ikifika mwaka wa tatu wa uendeshaji alipe kodi zote, hii itaiwezesha Tanzania kupata vitanda vinavyotosheleza mahitaji na kupata watalii wengi. Pia hoteli zilizopo waboreshe miundombinu na huduma kwa kupatiwa mafunzo na wafanyakazi wenye uwezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ufugaji wa nyuki, Tanzania ina fursa sana na nzuri za kuzalisha asali kwa wingi duniani ambayo ikitumiwa ipasavyo itasaidia kukuza kipato cha mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla. Tanzania ni nchi ya pili Barani Afrika na inazalisha tani 56,000. Hata hivyo, kiwango hicho ni kidogo kwa sababu Tanzania ina uwezo wa kuzalisha asali tani milioni 1,038 kwa mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa ninaloliona ni utashi hafifu wa jamii kujishughulisha na kazi za ufugaji nyuki na kupanda miti kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira. Serikali kupitia Maafisa Maliasili wahamasishe vya kutosha jamii juu ya faida ya ufugaji nyuki na upandaji miti ili ilete matokeo ya haraka kwa sababu asali ina faida kubwa ikiwemo ya kiafya na kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe teknolojia ya kisasa inatumika kwenye ufugaji wa nyuki na kupanda miti. Idara ya Misitu iachane na shughuli za uchuuzi wa magogo na ukataji miti kiholela na badala yake wajikite kwenye upandaji miti ya kibiashara na kuhifadhi mazingira na hivyo hudumisha mazingira bora ya kuishi pamoja na ufugaji wa nyuki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe na eneo lote la Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini, Rukwa kuna fursa kubwa sana kupanda miti na kufuga nyuki na hata kuendeleza utalii wa kitamaduni, kijiografia ki-photographic kuwepo kwa kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Songwe ni fursa kubwa ya kuboresha utalii na uhifadhi wa misitu na kukuza utalii katika Sourthen circuit.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaitaka Serikali kupitia Wizara hii kutumia Idara ya Misitu kutusambazia miche ya miti na mizinga ya nyuki ya kisasa. Pia kushirikisha sekta binafsi katika utalii kwa kupunguza tozo nyingi zinazowazidishia gharama na kupunguza idadi ya watalii.
Lakini pia kuunganisha watalii na wajasiriamali wadogo wadogo wanaotoa huduma na kutengeneza bidhaa za sanaa na kuwauzia watalii, kutoa mafunzo unganishi yatakayoweka programu za mafunzo, kuwatayarisha wananchi kwa pamoja kati ya sekta ya umma na binafsi ili ushiriki wa jamii ya wafanyabiashara na wafanyakazi wa maeneo hayo kwenye shughuli za utalii na uhifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ninaunga mkono hoja.