Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wote wa Jimbo la Babati kwa kunirudisha kwa awamu ya pili kuwa mwakilishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano ikiongozwa na Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa mwendo na kasi na matumaini mapya ambayo wameonyesha kwa Watanzania wote. Vile vile nishukuru uongozi mzima uliochaguliwa ikiwa pamoja na wewe Mwenyekiti, Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wenzako na Mawaziri wote waliochaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Dkt. Mpango, Waziri wetu wa Fedha kwa kuja na mpango mzuri, mpango ambao unaonyesha na umeangalia sekta zote. Mpango huu ukitekelezwa vizuri nina uhakika kabisa kwamba yale malengo ambayo tunayo ya kufikia miaka mitano ijayo na huu wa mwaka mmoja ya kufikia kuwa nchi ya kipato cha kati, tutafikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika Mpango huu inabidi Serikali ijipange vizuri sana, kwanza kuwa na nidhamu ya hali ya juu sana kwa kutekeleza yale yote ambayo yamepangwa na ambayo yako kwenye Mpango. Pia Watumishi wengi ambao wako Serikalini kubadilika fikra zao, yaani mindset change. Tusipobadilika hayo yote yataendelea kubaki kama yalivyokuwa huko nyuma, mipango inakuwa mizuri lakini haitekelezeki.
Muhimu kuliko yote pia ni kuhakikisha kwamba suala lile la nidhamu kwenye matumizi ya fedha iheshimiwe hasa zile fedha ambazo ni ring-fenced. Yale yakiheshimiwa nina uhakika kabisa zile fedha ambazo zimepangwa kwenda kutekeleza miradi mbalimbali itakuwa inaenda. Kwa mfano, miradi ya REA na ule mpango wa maji. Yale pia tutaomba wakati wa majumuisho, basi tupatiwe taarifa rasmi ili tuweze kujua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la muhimu lingine ni kuhakikisha kuwa suala zima la PPP linafanyiwa kazi kwa undani kabisa. Serikali ikubali, hasa wale Watumishi wa Umma wajue kabisa kwamba Serikali haiwezi kutekeleza haya mambo yote yaliyoko kwenye Mpango. Sehemu kubwa hasa huko tunakoelekea kwenye viwanda, viwanda vidogo, vya kati, viwanda vikubwa na hata mambo mbalimbali ya miundombinu ya huduma, wakishirikiana na sekta binafsi, yaani PPP, tutaweza kufanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ni muhimu Serikali ijipange katika uratibu baina ya Wizara moja na nyingine, ile coordination iwe ya hali ya juu. Kila Wizara isiwe na mpango wake, kila Wizara ifanye kazi, Wizara zote zishirikiane ili mpango kama ni wa kutekelezwa basi coordination iwe ya hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kabisa kwamba safari hii, sekta kubwa imelengwa ni sekta ya kilimo. Kilimo kwa mapana yake. Kilimo, mifugo, uvuvi yote hayo yapo kwenye mpango huu. Muhimu naomba tujipange. Kulikuwa na ile ambapo Tanzania ilikubaliana kwenye Maputo Declaration kwamba asilimia 10 ya bajeti nzima. Kwa hiyo, bajeti ambayo tunategemea kwamba itapangwa safari hii 10% yake itaenda kwenye sekta hiyo ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia asilimia moja (1) ya bajeti nzima pia itaenda kwenye sekta ya utafiti kwa sababu bila utafiti hatuwezi kuendelea. Tukiangalia vituo vyetu vya utafiti vina hali mbaya sana, tukiangalia watafiti wetu wana hali mbaya. Sasa tukiwatengea bajeti, mengi tunaweza kuyafanya humu humu nchini kutokana na mazingira yetu na kutokana na hali yetu tunaweza kwenda tunapotarajia kwenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine muhimu ni suala la kwenye bajeti itakayopangwa hiyo ya asilimia 10 kwenye kilimo, suala zima lile la fedha ya kununua mazao, lisiwe kwamba ni moja katika asilimia inayoongezwa pale. Leo unaambiwa bajeti ya kilimo ni kubwa sana lakini utakuta zaidi ya nusu ya ile fedha inakwenda kununua chakula ya hifadhi. Sasa ile siyo maendeleo ya kilimo ile ni pesa tu imewekwa kwa ajili ya kununulia mazao, hiyo iwe kwenye kitengo tofauti kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine muhimu ni nidhamu ya matumizi na matumizi mabaya ya fedha. Ni muhimu sasa tujikite huko. Kila mwaka tunasikia na Wabunge wote hapa wamechangia, reli ya kati, unakuta barabara, kila mwaka fedha ya maafa inatumika kwa mabilioni. Kila mwaka sehemu hiyo hiyo. Ni vizuri sasa wale ambao wanaosimamia hayo maeneo kwa nini wanasubiri tu kwamba haya maafa yatokee kila mwaka wapate hizo fedha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maoni yangu naona kwamba, labda ni mradi wa namna ya kula hizo fedha, lakini muhimu ilitakiwa kwamba kama haya mafuriko yametokea sehemu fulani, tukaangalia chanzo chake ni nini, kama ni maji yanatokea sehemu fulani tuweke mabwawa huko juu, maji yasije yakaharibu huku chini ili yale maeneo ya huko juu maji yakivunwa yatumike kwenye umwagiliaji, maji ya kunywa, maji ya mifugo na hii fedha badala ya kwenda kila mwaka kwenye maafa itapungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka kuna mikoa ambayo tunapeleka chakula cha msaada ni mabilioni ya shilingi, lakini hayo mabilioni ya chakula yanayopelekwa kule kwenye mikoa hiyo, ingepelekwa miundombinu wa umwagiliaji, kuvuna maji na umwagiliaji. Baada ya mwaka mmoja mikoa ile ingezalisha chakula kingi, kuliko hii mikoa ambayo tunapeleka chakula huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la matumizi ya fedha Serikali ijikite, tuangalie maeneo yote yale ambapo tunaweza kubana matumizi. Tuweze kubana lakini kabla ya hiyo bajeti pia natarajia kabisa kwamba sheria ya manunuzi tutakuwa tumeifanyia kazi. Hata tungekusanya mabilioni ya shilingi asilimia yote inakwenda kutumika vibaya kwa sababu sheria mbovu, sheria kandamizi, sheria hiyo ya manunuzi. Nashukuru kwamba, miaka minne nilipigia kelele hiyo sheria, sasa italetwa na naamini Wabunge wote tutashirikiana kwa kuifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningeendelea kushauri, ni kwamba tumeambiwa safari hii katika ile Sheria ya Bajeti, Maafisa Masuuli wa sasa watakuwa wanapanga bajeti kutoka kila Mkoa, kila Idara. Ni vizuri basi ushirikishwaji wa wadau wote katika kila mkoa, katika kila Taasisi, uanze mapema ili maoni ya watu wote namna ya kwenda, namna ya kufanya ufanyiwe kazi mapema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine tunaposema tunaanza kuwekeza kwenye sekta nzima hii ya kilimo, ili tuweze kuwa na viwanda vidogo, viwanda vya kati na viwanda vikubwa ni vema tujikite maeneo ambayo tayari yanazalisha. Kwa mfano, sukari kuna maeneo ambayo tunazalisha miwa, kwa mfano kule Babati, lakini utakuta kwenye mpango mpya huu wa kuanzisha viwanda vipya, Wilaya ile haipo. Tunataka kuzalisha labda mafuta ya mawese, utakuta Wilaya husika haijahusishwa, kwa hiyo, vizuri yale maeneo husika yafanyiwe kazi na yawe kwenye mpango kwa awamu ya kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kwenye suala la namna ya kukusanya mapato zaidi ili Serikali iwe na wigo mpana wa kukusanya kodi. Suala la kutumia mashine za EFD’S tunashukuru na tunasema kila Mtanzania ambaye anafanya biashara atumie mashine ya EFD. La muhimu tulipendekeza kwamba, badala ya kuwa centralized, kwamba kampuni chache ndiyo ziruhusiwe kuleta hizo mashine na kusambaza, kila Mtanzania ambaye ana nia ya kuwa na mashine hizo na kufanya biashara hiyo, kwa mfano hapa Dodoma, unaweza kuwa mtu anataka mtaa fulani kama zile za cable aweze kuwa na bishara yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweke viwango vya zile mashine zinavyotakiwa kutumika ili service ya ile mashine pia ziweze kupatikana katika eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi Serikali iangalie namna ya kupunguza kodi na tozo mbalimbali, ili viwanda vya ndani viweze kukua. Leo niwape mfano, kwenye sekta ya mbegu tunaagiza asilimia 75 ya mbegu toka nje ya nchi. Ni kutokana na huko nyuma, ilikuwa asilimia 70 inazalishwa ndani 30 inatoka nje.
Baada ya Serikali kuweka kodi na tozo mbalimbali, kwa wingi tayari sekta hiyo imekufa kabisa leo tunaagiza mbegu kutoka nje, ambayo haina kodi kabisa. Madawa ya mifugo kutoka nje, hayana kodi lakini ukizalisha ndani ya nchi ina kodi. Kwa hiyo, mfumo mzima wa utozaji wa kodi, uangaliwe ili sekta binafsi na sekta zote ziweze kukua ndani ya nchi. Viwanda hivi, kama tusiporekebisha, mfumo mzima na tozo mbalimbali haitakua, na watu hawatawekeza katika suala hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia maeneo mengine tuangalie mbinu mbadala, tushirikishe watu, kwa mfano, kwenye Sekta ya Uvuvi, tulishapendekeza huko nyuma. Tunaweza kutumia nishati mbadala kama gridi ya Taifa haifiki, katika maeneo ya Pwani, katika maziwa mbalimbali, mahali kuna uvuvi tupeleke nishati mbadala, solar na hii ya upepo, ili wakulima wetu, wafugaji wetu, wavuvi kule wawekewe ghala/friji ndogo ndogo za kuhifadhi mazao yao ili badala ya kuuza samaki kwa vikapu, waweze kuhifadhi hawa samaki, waweze kuwauza kwenye soko ili waweze kupata bei nzuri zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo madini mengi, sasa Serikali ijikite kwa mfano, tuna madini ya gemstones vito vya thamani ya chini. Tuna kituo pale Arusha cha Kanda ya Kaskazini, ambapo Serikali ingewekeza fedha za kutosha….
MWENYEKITI: Ahsante sana.
MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja