Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa kukuza uchumi wa nchi yetu. Msitu wa Shagayu uliopo Wilaya ya Lushoto uliungua mwaka 2012 ambapo hekta 49 ziliungua hata hivyo mpaka sasa ni hekta 11 tu ambazo zimepandwa katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuungua kwa eneo la msitu huo lilisababishwa ardhi kutokuwa na vizuizi vya maji, hivyo mvua za mwaka 2015 zilisababisha maafa makubwa ya maporomoko na mafuriko katika maeneo yanayozunguka msitu huu. Mheshimiwa Waziri pamoja na eneo kubwa la msitu ambao unazungukwa na vijiji 15, lakini msitu una wafanyakazi wawili tu ilhali unazo nyumba za kutosha familia sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo tunaomba Idara ya Misitu kupitia Wizara watuongezee watumishi wanne kufikia sita ili waweze kuhudumia vizuri eneo la msitu ikiwa ni pamoja na kuwapatia usafiri wa pikipiki kwani kwa sasa ipo pikipiki moja tu. Tunaomba ziongezwe pikipiki mbili zaidi ili ziweze kuleta tija katika kuhudumia msitu huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miundombinu inayozunguka maeneo ya msitu wa Shagayu sio rafiki, tunaomba Wizara kupitia Wakala wa Misitu ya Asili ili kuboresha miundmbinu hasa ya barabara ili isaidie kukabiliana na majanga hasa ya moto pale unapojitokeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mbuga ya Mkomazi iliyopo katika Mikoa ya Tanga na Kilimanjaro, lakini Mlanga (lango) la kuingilia hifadhini lipo katika Wilaya ya Same, hivyo kuwasumbua watalii wanaotembelea Wilaya ya Lushoto na vivutio vyake kulazimika kwenda mpaka Same.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa na hususani Hifadhi ya Mkomazi kutuwekea mlango wa kuingia hifadhini kupitia Wilaya ya Lushoto katika Kata ya Lunguza, Kijiji cha Kiringo ili kukuza na kuchochea shughuli za utalii katika eneo hili la Tarafa ya Umba ili kusaidia kupunguza umaskini na kuchochea maendeleo ya watu wa Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi na ujirani bado unasuasua katika Hifadhi ya Mkomazi, hivyo kuweka mazingira hafifu ya ushirikiano baina ya hifadhi yetu na wananchi wa maeneo husika. Tunaiomba Wizara ihakikishe ile asilimia saba ya mapato yatokanayo na makusanyo ya hifadhi husika basi yaelekezwe kwenye vijiji na jamii inayozunguka hifadhi ili kuchochea shughuli za maendeleo na kupunguza uhasama baina ya hifadhi na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi baina ya hifadhi zetu bado ni jambo linalosumbua sana hasa katika Kijiji cha Kiringo ambapo mpaka upo jirani sana na makazi ya watu hivyo kuleta misigano isiyokuwa ya lazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Operesheni Tokomeza katika Wilaya ya Lushoto umeacha ardhi ya watu wakiwa na athari za kimwili, kiafya na kiuchumi. Silaha ambazo zimechukuliwa toka kwa wananchi waliopo jirani na hifadhi lakini hazikuhusika katika shughuli haramu za ujangili zirejeshwe kwa wamiliki halali ili waweze kujilinda kwa usalama wao kama walivyoziomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matarajio yetu kuwa uhifadhi wa misitu na mbuga zetu utaenda sambamba na ustawi wa jamii yetu ya Kitanzania kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.