Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kutoa maoni yangu katika kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha, hotuba ya Bajeti ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze pia kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Dkt. Philip Mpango kwa hotuba yake ambayo kwa ujumla ni nzuri na kama wenzangu wengi walivyosema, ni bajeti ya kwanza hii, anachukua mambo mengine ya nyuma, anaangalia huko tunakokwenda mipango iko vipi, pamoja na ushauri mwingine, naamini na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge atauzingatia, kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nielezee masikitiko yangu makubwa kwa kusema kweli, kwamba Jimbo langu la Morogoro Kusini tulijipanga sana katika kipindi hiki tuweze kukuza uchumi, hasa wa kilimo na kwa sababu hiyo tulitegemea sana kupata miradi ya miundombinu ya barabara. Tumezungumza sana, tumeomba sana, tumeeleza sana, lakini kwa bahati mbaya sana haikupewa umuhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili nalisema wazi kabisa, limenisikitisha na litawasikitisha wananchi wengi sana wa Morogoro Kusini. Hata hivyo, naamini Serikali itakuwa na jicho lingine la kuangalia ukweli kwa sababu huko ndiko kwenye kuzalisha mazao, huko ndiko kwenye vijiji, huko ndiko kwenye nafasi ya kutengeneza viwanda hivi tunavyovizungumza, lakini bado haki haitendeki, bado wenzetu hawaoni hicho ambacho sisi wengine tunaona, bado hawaoni hata umuhimu wa ile barabara ya Bigwa kwenda Kisaki kwa kiwango cha lami ambacho watu kama Wamarekani waliiona na wameiweka kwenye Mpango wa MCC II, lakini Serikali yangu hii hawataki kukubali, hawataki kuona, hakuna haki inayotendeka na hili si jambo jema, hatulikubali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizunguzie hali ya uchumi wa Taifa, nimesoma hali ya uchumi wa Taifa katika mwaka huu tulionao 2015, kwa sehemu kubwa, kwa sekta nyingi hatukufanya vizuri ukifananisha na hali ilivyokuwa mwaka 2014. Yapo maeneo tumefanya vizuri sana, ukuaji wa Sekta kama za Ujenzi, hususan barabara na ujenzi wa nyumba za makazi, tumefanya vizuri na kwenye eneo hili nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu ni eneo ambalo yeye mwenyewe akiwa Waziri wa Ujenzi amelisimamia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nipongeze Sekta Binafsi, niipongeze pia Serikali upande wa TBA, pamoja na mashirika na taasisi za kifedha ambazo ziliweza kwa sehemu kubwa kujenga hizi nyumba za makazi ambazo tunazizungumzia sasa hivi na sehemu nyingi ni mfano. Ni nzuri, ni za kisasa zinafurahisha hata kwa kuziangalia, nawapongeza sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hilo halitoshi, hatukufanya vizuri kwenye upande wa biashara. Kwenye upande wa biashara hatukufanya vizuri, kwenye biashara kwenye ranking zetu Kimataifa kwa upande huu, malalamiko ni yale yale. Kunakuwa na usumbufu kidogo wakati wa kuomba leseni, kunakuwa na mzunguko sana, hata wakati wa kulipa kodi tu hizi bado watu wanazungushwa. Sasa Serikali ifike mahali tuweke utaratibu mzuri, tujirekebishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sababu nchi kama Rwanda kila siku wenzetu wanasifiwa kwamba wao wanarahisisha sana mambo yao kuliko sisi na viongozi wetu hawahawa, Mawaziri wetu hawahawa wana uwezo mkubwa sana, lakini bado tatizo hili linaonekana kuwa linatusumbua. Nawaomba sana tujipange kwa makusudi kabisa, tuondoe tatizo hilo, tuondoe tatizo la rushwa, tuondoe tatizo la ukiritimba, watu wafanye biashara. Tunahitaji hawa watu wengi wa biashara waongeze mapato ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie maeneo machache machache ambayo nayaona pengine yataleta tija kidogo kwenye hii bajeti. Wengi wamezungumzia suala la uvuvi kutopata nafasi inayostahili. Ni kweli, ukisoma kwenye vitabu hivi huamini kwamba hii ni nchi yetu ambayo imezungukwa na maziwa na bahari, hatujaweza kutumia vizuri nafasi yetu. Inanifanya nikumbuke kwamba inawezekana tulifanya makosa sana tulipoliharibu Shirika letu la TAFICO, naamini kabisa uvuvi tunaoufanya huu ni mdogo sana, lakini bado tumepata mapato haya, tungeweza kupata zaidi ya mara nne kama tungeweza kufanya uvuvi mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu Msumbiji wamenunua meli kubwa za uvuvi kwa ajili ya bahari hii ambayo tuna-share nao, wamenunua meli 34 zinafanya uvuvi wa viwanda na sasa hivi nyingine wanazitengeneza ili sasa wa-meet zile standards za kuuza samaki wao kwenye soko la Ulaya, sisi hakuna, huoni kama kuna jambo la namna hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningewaomba sana twendeni kwa spidi, twendeni na sisi kama vile si Taifa dogo hivi. Tuchukue uzito wetu, ukubwa wetu hata kwa jiografia tu, hawa wenzetu wanashinda vipi sisi tushindwe? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo linanihusu moja kwa moja ningependa nichangie, nisije nikalisahau, ni hili la milioni 50 za vijiji. Wengi wamelizungumza, kila mtu ana mawazo yake, wengine wanataka waanzishie benki, wengine wanataka waanzishie vitu vingine. Hizi ni pesa ziko maalum kwa ajili ya wajasiriamali wetu vijijini, ni vizuri tusiende nje ya malengo ya hizi pesa zilipowekwa. Tugawiwe kwa utaratibu mzuri lakini ulenge kule ambako ilani ilisema na Mheshimiwa Rais alisema, tuwasaidie wajasiriamali kule, hili ndilo lengo kubwa la hizi pesa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mikoa 10 itakayoteuliwa mwanzo sina uhakika nayo, vigezo gani mtatumia sina uhakika, nitashindwa majibu ya kuwaambia watu wangu kule jimboni. Ninachoomba hizi pesa zigawiwe, vijiji vipate ili na wao waweze kufanya shughuli zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la ununuzi wa ndege tatu za Air Tanzania (ATCL) jambo zuri, limekuja wakati muafaka, ushindani mkubwa kwenye eneo hili. Sikatai pendekezo linalozungumzwa la kuangalia partners tunaoweza tukafanya nao, lakini hilo halizuii sisi kuanza na hizo ndege ambazo tunataka tuwe nazo. Wasiwasi wangu ni madeni ya ATCL, kama bado yapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma nilihusika kwenye vikao vidogo vidogo, nafahamu vitu vingine. Upo wakati ndege zao zilitaka zikamatwe wakiwa nje ya nchi, sasa kama madeni haya hayajamalizika, wanaweza wakanunua ndege mpya, wakaanza safari, hukohuko zikawa grounded, zinachukuliwa na wenye madeni. Kwa hiyo, tahadhari naiweka tu kwa Serikali waangalie, je, suala hilo limekaa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie…
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante.