Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia mawazo na kutoa ushauri wangu katika bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/2017. Nashukuru na kuipongeza Serikali kwa kuleta bajeti nzuri ambayo inajali maslahi ya Watanzania wote kwa ujumla wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo kama sitakupongeza kwa ujasiri uliokuwa nao katika kipindi hiki kigumu ambacho umepitia lakini nakuamini wewe ni mwanamke jasiri na unaendelea kutuongoza vizuri bila kutetereka. Sisi tuko pamoja na wewe katika kuhakikisha kwamba kanuni na taratibu za Bunge zinafuatwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa bajeti nzuri lakini kuna haja ya baadhi ya maeneo tukayasemea na kuyaboresa. Cha msingi tunachomuomba Mheshimiwa Waziri asikilize mawazo ya Wabunge na kuyafanyia kazi, penye wengi pana mengi.
Mengi yaliyosemwa na Wabunge ni kwa niaba ya wananchi wengi walioko huko nje. Tunaomba Mheshimiwa Waziri ayafanyie kazi ili kuleta ufanisi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nigusie baadhi ya mambo ambayo yanagusa jimbo langu nikianza na suala la maji. Niungane na Wabunge wenzangu waliounga mkono na waliotoa wazo la kuongeza pesa katika Mfuko wa Maji kutoka Sh.50 kwenda Sh.100. Tunahitaji tupate pesa za kutosha katika Mfuko wa Maji ili kutatua kero kubwa ya maji iliyopo katika maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali isiwe na kigugumizi katika hili, Wabunge wengi wanahitaji kutatuliwa kero za maji katika maeneo yao, akina mama wanapata taabu kubwa ya maji katika maeneo yetu tunakotoka. Tunahitaji miradi mingi ya maji itekelezeke katika maeneo yetu ndiyo maana tunashauri Sh.50 iongezwe kuwa Sh.100 ili pesa nyingi ziende zikatatue kero za maji katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeamua kuanza na hili kwa sababu mimi na wananchi wa Jimbo la Igalula tuna masikitiko makubwa sana. Katika mradi wa maji wa kutoka Ziwa Victoria Jimbo la Igalula lililopo katika Mkoa wa Tabora hatumo katika mradi huu. Majimbo yote maji ya kutoka Ziwa Victoria yatafika lakini Jimbo la Igalula tumesahaulika. Napenda kujua wananchi wa Igalula wameikosea nini Serikali hii mpaka kutusahau kutuingiza katika mradi wa maji wa Ziwa Victoria wakati tuna shida kubwa ya maji? Katika kuchangia Hotuba ya Rais nilisema tuna shida ya wafugaji wanahitaji maji kwa ajili ya mifugo yao kwa maana ya malambo, tunahitaji mabwawa ya maji kwa sababu ya kutatua kero kubwa ya maji iliyopo katika Jimbo la Igalula. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumejaribu kuchimba visima vifupi na virefu havitoi maji kwa sababu eneo kubwa la Mkoa wa Tabora hakuna maji chini. Nilishauri, katika Jimbo letu la Igalula kuna maeneo mengi ambayo tunaweza tukatega mabwawa ya maji na watu wakapata maji lakini Serikali mabwawa imetunyima, malambo imetunyima, maji ya kutoka Ziwa Victoria hatuna, tunaambiwa tutapata maji ya kutoka Mto Malagarasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Malagarasi ni zaidi ya kilometa 150, lakini maji yanayotoka Ziwa Victoria yanapopita Uyui kwenye Jimbo la Tabora Kaskazini ni chini ya kilometa 30 kufika katika Jimbo letu la Igalula. Ni rahisi zaidi kuyatoa maji ya Ziwa Victoria kutoka Uyui kwa maana ya Makao Makuu yetu ya Wilaya kuyaleta katika Jimbo la Igalula kuliko kuyatoa katika maeneo mengine. Niombe Serikali itueleze, Waswahili wanasema awali kuu, sasa Ziwa Victoria tunakosa tunaahidiwa ya baadaye. Sisi tunahitaji kuwepo katika mradi wa maji wa Ziwa Victoria ili kuondoa tatizo la maji katika Jimbo letu la Igalula. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie kidogo kuhusu afya, tulipitia bajeti ya Wizara ya Afya na Wizara ya TAMISEMI. Lakini katika ilani ya Chama cha Mapinduzi ya miaka kuanzia ya 2000 mpaka sasa tulizungumzia ujenzi wa zahanati katika kila kijiji, lakini pia tulizungumzia vituo vya afya katika kila kata. Nataka nisikitike, sioni ilani hii inatekelezwa namna gani kwa sababu Serikali katika bajeti zote za Wizara ya Afya, TAMISEMI na hii bajeti kubwa haijazungumza kwa uzito mkubwa kuhusiana na tatizo kubwa la afya vijijini kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, zahanati nyingi zimejengwa hazijakwisha, zilizokwisha kwa nguvu za wananchi hazina wataalam. Katika Jimbo la Igalula tumeanzisha kujenga vituo vya afya katika kila kata, lakini mpaka leo hatujui Serikali itakuja kukamata namna gani miradi ile ambayo wananchi wanawekeza pesa nyingi kuondoa tatizo la afya katika maeneo yetu. This is very serious. Tuiombe Serikali iangalie, ione umuhimu wa ku-implement upatikanaji wa vituo vya afya na zahanati katika kila kijiji na katika kila kata ili kuondoa tatizo la afya katika maeneo yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye reli, unapozungumzia reli umuhimu wake kila mmoja anajua. Kwa sisi wana Igalula ni usafiri unaoturahisishia kufika maeneo mbalimbali. Wananchi wangu wanafanya biashara katika maeneo ya reli zile, lakini reli katika uchumi wa nchi unasaidia sana katika maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumetoa ushauri mara nyingi, umuhimu wa reli kuunganishwa na RAHCO. TRL inategemea kwa kiasi kikubwa ruzuku kutoka Serikalini kwa sasa, RAHCO wanategemea ruzuku kutoka Serikalini. RAHCO tegemezi, TRL tegemezi, lakini kuna uwezekano wa TRL ikiunganishwa na RAHCO, TRL ikaweza kujiendesha kiuchumi, ikaweza kukopa na ikaweza kulifanya Shirika hili likajiendesha bila hata wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuliomba Serikali ilete sheria ya kubadilisha ili tuunganishe tena RAHCO na TRL ili kuleta ufanisi wa haya mashirika mawili; lakini mpaka sasa Serikali imekuwa kimya. Tunaomba Serikali ifanye umuhimu katika kuunganisha mashirika haya mawili ili kuleta ufanisi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda nisemee zao la tumbaku. Tumbaku ni nguzo ya uchumi wa Wilaya yetu ya Uyui na Mkoa wa Tabora. Mapato makubwa ya Wanatabora yanategemea sana zao la tumbaku. Serikali kila siku inasema inazijua changamoto za mkulima wa tumbaku, utatuzi wake, kila siku tutatatua kesho lakini kero za mkulima zinazidi kuongezeka, mkulima anazidi kunyonywa, masoko yanakuwa shida. Nataka niiombe Serikali sasa, badala ya Waziri kuahidi kuja Tabora kuzungumza na wakulima kero hizi tumezileta sisi wawakilishi wao, kero hizi wanazijua, sasa Serikali tunataka majibu ni lini mkulima wa tumbaku atapata afueni na zao lake la tumbaku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kodi nyingi, makato mengi, bei ndogo, soko tabu, wanadhulumiwa. Mfano mdogo, Mheshimiwa Waziri, CRDB waliingia mkataba na Vyama vya Msingi kujenga magodauni katika maeneo yetu mbalimbali. Mkandarasi walimtafuta wao, wakaingia mkataba, wakajenga magodauni yale, mwisho wa siku magodauni yale hajakwisha, yamedondoka, hayasaidii mkulima, lakini mpaka kesho mkulima anakatwa pesa kulipia magodauni yale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba kero ya mkulima wa tumbaku sasa iweze kwisha. Mkulima…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.