Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. WILLIAM T. OLENASHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na Naibu wake kwa kuwasilisha hotuba nzuri. Hotuba hii imetoa dira ya sekta katika mwaka ujao kwa ufasaha mkubwa. Kama Mbunge wa Ngorongoro, Jimbo ambalo zaidi ya asilimia 80 ni hifadhi za wanyama pori, naomba kuchangia hotuba ya Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kubadilisha Sheria ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (Ngorongoro Conservation Area Act), Sheria ya Ngorongoro imepitwa na wakati na ni sheria ya siku nyingi sana, ni sheria ya kikoloni. Sheria hii haiendani na mazingira ya sasa ya uhifadhi na inapingana na sheria za sekta nyingine kama ardhi, barabara, Serikali za Mitaa na kadhalika. Aidha, Sheria hii ya Ngorongoro haiendani na Sheria Kuu ya Uhifadhi (Framework Legislation), yaani Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009.
Vilevile sheria hii haitambui dhana ya kushirikisha wananchi katika uhifadhi (community conservation), dhana ambayo ni muhimu sana kwenye eno la matumizi mseto ya ardhi (multiple land use). Ni rai yangu kwa Wizara ichukue haraka hatua za kurekebisha sheria hii kwa kushirikiana na wadau muhimu hususan wenyeji wanaoishi ndani ya hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vijiji kunufaika na uwekezaji Ngorongoro, vijiji vilivyopo ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro havinufaiki moja kwa moja (direct benefits) kutokana na uwekezaji wa kitalii unaofanywa kwenye ardhi zao. Aidha, kwa utaratibu wa sasa wawekezaji hawalazimiki kuingia mkataba na vijiji badala yake wanaingia mkataba na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA). Kwa utaratibu huu ni vigumu wenyeji kupata ajira na fursa zingine zinazopatikana kwa kuingia mikataba na wawekezaji kama ilivyo kwa vijiji vingine Ngorongoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Wizara iainishe utaratibu wa kuviwezesha vijiji vya Hifadhi ya Ngorongoro kuweza kushirikishwa katika uwekezaji unaofanywa katika ardhi yao. Wizara iwalazimishe wawekezaji wanaotaka kujenga hoteli na kambi ya kitalii kupata ridhaa ya kimkataba kabla ya kuingia lease na mamlaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mgogoro wa Pori tengefu la Loliondo, ningependa vilevile kuchangia kuhusu mgogoro wa muda mrefu uliopo ndani ya pori tengefu la Loliondo (Loliondo Game Controlled Area). Mgogoro huu kwa sehemu kubwa umechangiwa na muingiliano wa mamlaka ya usimamizi wa eneo husika kati ya Wizara ya Maliasili na Utalii na Serikali za Vijiji. Wizara ina mamlaka kuhusu rasilimali za wanyamapori lakini vijiji vina mamlaka kuhusu ardhi. Wizara ya Maliasili imetoa kibali cha uwindaji kwa kampuni ya OBC tangu mwaka 1992 bila ridhaa ya vijiji. Mgogoro huu umedumu kwa zaidi ya miaka 20 na hauelekei kuisha bila hatua maalum za kisheria kuchukuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rai yangu kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii itatekeleza matakwa ya Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009 inayomtaka Waziri kutenganisha mapori tengefu (Game Controlled Areas) na ardhi ya vijiji ili kuondoa migogoro isiyokuwa na maana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la manyanyaso ya wananchi ndani ya pori tengefu la Loliondo, ningependa kuwasilisha kero inayowakumba wananchi wa Jimbo langu wanaoishi ndani ya pori tengefu la Loliondo. Askari na watendaji wa KDU wamekuwa na tabia ya kuwakamata na kuwanyanyasa wananchi pale wananchi wakikata miti kwa ajili ya ujenzi kwa kisingizio cha kuharibu mazingira. Wananchi wa kabila la kimaasai hawana tabia ya kukata miti hovyo au kuua wanyama na ndiyo maana eneo hilo lina wanyama na mazingira mazuri mpaka leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ardhi hii iko chini ya mamlaka za vijiji ambazo hazijakataza utumiaji wa ardhi kwa matumizi ya kujenga nyumba na maboma. Aidha, watendaji hao wamekuwa wakiwasumbua wananchi wasilime kwenye baadhi ya maeneo kwa kisingizio kuwa wanaharibu mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Wizara iwaonye watendaji wake waache tabia ya kuingilia mamlaka ya Serikali za Vijiji ambazo ndizo zinazohusika na mipango ya matumizi ya ardhi. Serikali za Vijiji kwenye pori tengefu la Loliondo ndilo zenye mamlaka ya matumizi ya ardhi. Ni vizuri Wizara ya Maliasili na Utalii ikishirikiana na Serikali za Mitaa (vijiji) pale inapohitaji kuchukua maamuzi kuhusu matumizi ya ardhi kwani ndizo zenye mamlaka kisheria.
Mheshimiwa Mmwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naomba kuunga mkono hoja.