Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nami niendeleze pale wenzangu walipokuwa wanakupongeza na pia kukupa moyo na kukuhakikishia hiyo kazi yako kila mmoja ameridhika kuwa ni nzuri, unafanya kazi vizuri, uendelee na moyo huo huo na uendelee na uzi huo huo na wengi tuna imani ya kwamba hiyo kazi kwako ni Mwenyezi Mungu amekupatia. Bunge hili ndilo lililokuweka wewe hapo siyo mtu mwingine na unafanya kazi vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hilo, napenda nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na timu yake. Naye niendeleze kumtia moyo kwa kusema mtoza kodi hasifiwi hata siku moja. Kwa hiyo, awe na moyo huo kuangalia kwamba chochote atakachokifanya hata mimi mwenyewe unaponitoza kodi sitakufurahia. Mheshimiwa Waziri anafanya kazi vizuri, Wizara yake inafanya kazi vizuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanza labda ningenukuu hitimisho la hotuba ya Waziri kidogo tu, ukurasa wa 93 anasema:-
“Mheshimiwa Spika, wananchi wetu wengi wamechoka na adha ya umaskini: Watanzania wanataka kipato cha kuweza kukidhi mahitaji yao ya msingi. Wananchi wanataka huduma bora zaidi hususan upatikanaji wa maji, elimu, afya, umeme na makazi”.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri hili ni hitimisho zito sana na kwamba Waziri imani yake ni hiyo, anatambua kuwa Watanzania tupo katika dimbwi la umaskini. Asilimia 75 ya Watanzania tunaishi vijijini, ni wakulima lakini ajaribu kuangalia na hilo hitimisho lake ametuangalia vipi sisi wananchi wa vijijini na hasa wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika ukurasa wa 95 amesema kuwa:-
“Misaada pia inaweza kuchochea rushwa na kuzorotesha jitihada za ndani hususan za ukusanyaji wa mapato”.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia amemnukuu mwanazuoni anaitwa Sebastian Edward ambaye naye alikiri kwamba Tanzania hii misaada nayo imesababisha kuharibu uchumi wetu na haikutusaidia, nami nakubaliana naye.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kulisoma hilo na mimi nikaenda kwenye kitabu kingine ambacho ameandika mwana dada Mzambia Mchumi Mbobezi, Dkt. Dambisa Moyo katika kitabu cha Dead Aid naye ameelezea hivyo hivyo kwa uchungu kabisa. Huyu ni mtaalam wa Benki ya Dunia na amepingwa na watu wengi ambao wamekuwa wakileta misaada huku. Alichosema nchi zetu hazihitaji misaada ya handout wanatufanya tuwe maskini zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, akaendelea kusema, sasa kuondokana na hilo, sisi Waafrika tunachotakiwa ni kwamba, tuweke mazingira mazuri ya kuvutia ili hawa watu waweze kutuletea mitaji ambayo itaongeza ajira kwa watu wetu. Nami nakubaliana na hilo na ndiyo sababu Serikali yetu ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli amesema anataka Tanzania iwe ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, ukiangalia katika bajeti hii nafikiri Waziri kwa kiasi kikubwa hakupata muda wa kuiangalia vizuri, inawezekana wataalam wetu wanapotosha Mawaziri wetu. Huwezi ukazungumza maneno mazito namna hiyo halafu ukiangalia bajeti ya kilimo haieleweki. Utakuwa vipi mchungu na umaskini wakati mkulima bajeti yake ya pembejeo hujaonyesha kuwa umemwekea kiasi gani kwa ajili ya kupunguza bei ya mbolea. Watanzania tunafanya kazi kwa bidii sana, wakulima tunazalisha lakini masoko yetu hayaeleweki. Hii bajeti haioneshi ni namna gani sisi mazao yetu yatakuwa shindani na wenzetu wa Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi tunaolima kahawa, chai, pareto, viazi, tumbaku, bei zetu ni ndogo mno. Bei ya Kahawa ya Tanzania (Arabica) ni karibu nusu ya bei ya kahawa ile ile ya Kenya, ni kwa nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kumtoa umaskini huyu Mtanzania tuangalie tu kuboresha haya masoko.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameonesha kuna mkakati wa kuanzisha commodity exchange ambalo ni wazo zuri sana, lakini sijaona huo mkakati ameuelezea wapi. Faida za commodity exchange ni kubwa mno, wakulima tunalima hatuna mahali pa kuweka mazao yetu yanaharibika. Walanguzi ndiyo wanasubiri wakati wa mavuno waweze kuwanyonya wakulima. Kahawa yetu inanunuliwa na wale wanunuzi wa kutoka Ulaya ambao wananunua na Kenya lakini kwa nini kahawa yetu tulipwe nusu ya bei ya Kenya, Ethiopia au Rwanda? Naomba hilo Waziri aliangalie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumsaidia mkulima, naomba pia aangalie uanzishwaji wa Benki ya Kilimo, huu mtaji hautoshi. Nami naendelea kumshauri, najua labda hilo atakuwa halipendi, ile shilingi milioni 50 ingeenda kwenye Benki ya Kilimo. Uzoefu unaonesha hizi pesa zikienda moja kwa moja zinaenda huko kuharibu hata uchumi wa nchi yetu. Naomba tuziwezeshe SACCOS zetu, tuiwezeshe Benki ya Wakulima ili ziweze kutoa huduma kwa wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni huduma za kibenki. Huduma za kibenki ni muhimu sana kwa uchumi wetu, lakini unapoanza kuweka tozo (VAT) kwenye huduma za kibenki ina maana unazifanya zile huduma ziwe ghali zaidi na unawakatisha tamaa Watanzania kutumia huduma hizi, naomba hilo aliangalie. Waziri kwenye hotuba yake ameongelea kuwa tofauti iliyoko kati ya riba ya deposit na riba ya lending ni kubwa, sasa ukiongeza hii VAT ina maana nayo itaongeza zaidi gharama za kibenki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania sasa hivi tunahitaji financial inclusion na huwezi ukaanza kuweka tozo wakati huo huo una-encourage financial inclusion. Huwezi ukaanza kuweka tozo kwenye capital market, capital gains tax unataka u-introduce ya nini, limetoka wapi hili wazo? Sasa hivi Watanzania tunataka tuwekeze kwenye soko la hisa unaanza kuwakatisha tamaa watu wasiwekeze huko. Utakusanya vipi kwanza hiyo tozo kwani transaction cost zinaweza kuwa kubwa kuliko hata hiyo unayotaka kukusanya. Kwa hiyo, naomba Waziri hilo aliangalie kwa upana wake na huko ndiyo mahali ambako Watanzania tunataka kwenda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie…
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia. Ahsante.