Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu katika mjadala unaoendelea. Awali ya yote nakupongeza sana kwa kazi nzuri unayoendelea kuifanya. Tunaomba uendelee hivyo hivyo na hao wanaotoka kwa hiari yao waendelea kutoka, lakini najua sasa uko nje wameshaanza kung‟atana wenyewe kwa wenyewe. Uendelee na kazi vizuri kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nianze na suala la msamaha wa kodi kwa ajili ya Mashirika ya Kidini. Kwa kweli Waswahili wanasema akufaaye wakati wa dhiki ndiye rafiki wa kweli. Sisi na Serikali yetu lazima tujiulize, Mashirika haya ya Dini yamekuwa yakitoa huduma nzuri sana. Leo hii tumejenga Zahanati zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumejenga Zahanati za Umma, Zahanati za Mashirika ya Dini zinakufa. Mashirika ya Dini yamejenga hospitali, yanahudumia wananchi; na ukijaribu kuangalia utakuta kwamba kwa Mikoa ile ya Nyanda za Juu Kusini, Mashirika yale yana vifaa bora sana vya matibabu na vifaa vile wanaviomba kutoka kwa wafadhili. Wanapewa bure kabisa; na vifaa vile ni gharama sana. Leo unasema walipe kwanza kodi. Unapotaka walipe kodi, maana yake, hawana hata senti tano ya kununua vile vifaa. Wamepewa bure, halafu wewe unasema walipe kodi kwanza, halafu tukishahakikisha kwamba kifaa hicho kimefika hospitali ndiyo wadai; watadai vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tuwe waungwana kama Serikali kwamba huduma wanayotoa ni kwa ajili ya wananchi wetu. Ningeomba Serikali yetu, wakati fulani tunasema Serikali yetu ina macho; iende pale Ikonda Makete, ikaangalie ile hospitali jinsi ilivyo bora na inavyohudumia idadi kubwa ya watu na inavyohudumia kwa bei ndogo. Iende Peramiho, iende Ilembula, wakaone zile hospitali jinsi zinavyohudumia wananchi. Waende pale Uwemba Mission wakaangalie jinsi wanavyohudumia wananchi; halafu unasema wakipata vifaa vya huduma, wakipata madawa walipe kodi kwanza halafu ndiyo warudishiwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali ifikirie upya jambo hilo na ione kwamba jambo hili ni la msingi sana kuhakikisha kwamba Mashirika haya yanaendelea kutoa huduma kwa ajili ya wananchi wetu. Vinginevyo tutasababisha hali ya afya kwa wananchi kuwa mbaya sana. Zipo Zahanati zimefungwa baada ya sisi kuanzisha Zahanati zetu, japokuwa Zahanati zetu za Serikali hazijasimama, lakini katika Jimbo la Njombe Mjini najua kuna Zahanati ya Kifanya imefungwa, kuna Zahanati ya Rugenge imefungwa, kwa sababu tu Serikali imeanzisha Zahanati. Ni vizuri basi tunapoanzisha Zahanati za Umma, tuangalie hawa waliotufaa kwa miaka mingi, tunafanya nao nini kuliko kuwaacha tu solemba namna ile, inakuwa haipendezi na wala haifurahishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la elimu. Katika mfumo wetu wa elimu tunao vijana ambao huwa tunawachagua kuingia kwenye ufundi. Wengine wanakwenda sekondari lakini wengine wanachaguliwa kwenda kwenye ufundi. Vijana wale wanachaguliwa kabisa kwenye chaguo la Serikali kwenda kujiunga na zile shule za ufundi, lakini kwenye mpango huu wa elimu bure hawamo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wanasoma katika madarasa yale ya Elimu ya Ufundi hayana vifaa kabisa, hawana bajeti, hawana vifaa vya kutendea kazi wala hawana Walimu. Kama tunaona mpango huu ni mzuri, uendelee kuwepo; kama siyo mzuri, ufutwe kwa sababu watoto wale tumewapoteza pale. Tunawapotezea muda wao, lakini vile vile tunawanyanyasa, kwa sababu hatuwapi vifaa vya kufanyia kazi, hawana bajeti na wala hawana Walimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine katika suala la elimu, naomba sasa tufike mahali tufanye tathmini; tunao mtihani unaoitwa Mtihani wa Kidato cha Pili. Hebu Serikali sasa iangalie, hivi mtihani ule tija yake ni nini? Kwa sababu zamani tulivyoanza na ule mtihani wa Kidato cha Pili, shule zilikuwa chache, leo shule zinafika 4,000 tunaendesha mtihani wa Kidato cha Pili, mtihani ambao wastani wa kufaulu uko chini sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Serikali iangalie ifanye tathmini; unaweza ukakuta pale tunapoteza fedha nyingi bila sababu na wala ule mtihani hauna tija. Vinginevyo, naishauri Serikali sasa itumie utaratibu wa wastani. Ni kweli utalalamikiwa na wengi, lakini ifanyike pilot study zichaguliwe shule kama 100 zianze na utaratibu wa wastani.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa wastani utakuwa na gharama ndogo kuliko utaratibu wa sasa ambao unatumia fedha nyingi kwa ajili ya mtihani wa kidato cha pili na mtihani wenyewe sioni kama una tija yoyote kwa sasa. Ni vizuri Serikali ikaliangalia hilo, ikafanya utafiti na kuona kwamba huu mtihani je, uendelee kuwepo ama ufutwe kabisa, tutumie utaratibu wa wastani ili kuboresha elimu yetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni VETA. Waheshimiwa Wabunge wengi wanaomba sana VETA zijengwe, hata mimi kwangu naomba VETA ijengwe, lakini tunajenga VETA za kitu gani? Hii ni hoja ya msingi sana kujiuliza. Unapojenga Chuo cha VETA kama kile cha Makete, Makete umejenga Chuo cha VETA unatoa ufundi wa magari. Hivi Makete kuna magari mangapi? Halafu una zana ngapi za kufundishia magari?
Mheshimiwa Naibu Spika, naona tunajenga vyuo ambavyo kazi yake kubwa ni kuhamisha vijana vijijini kupeleka mjini. Kwa sababu ukifundisha ufundi wa magari Makete, maana yake unataka Wanamakete wasome ufundi wa magari halafu wahame Makete waende kuishi mjini, kwa sababu idadi yao ni kubwa na haiwezi kuhudumia kama mafundi ndani ya Makete. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Serikali iangalie, chuo kinachofaa kwa Makete ni Chuo cha Useremala; lakini ni useremala wa aina gani? Ni lazima tujikite kwenye useremala wa kisasa. Uko mfumo ambao sasa namwomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda atusaidie kuona, tutapata wapi teknolojia inayoitwa knock down system kwenye mbao? Kwamba unaunda furniture halafu unaitenganisha unaifunga kwenye box halafu unaisafirisha; ukifikisha unakofikisha unaenda unaiuganisha tena. Tukianzisha vyuo kama hivi kwenye Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini likiwemo Jimbo la Njombe Mjini, vitakuwa na manufaa zaidi kwa sababu mbao zipo na vijana wapo, kuliko mnatuletea vyuo vya teknolojia ambayo hatuwezi tukaitumia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tunaomba VETA hizi zifundishe kilimo, kwa sababu kilimo ndiyo kinaajiri vijana wengi zaidi. Zifundishe kilimo cha kisasa, lakini zifundishe usindikaji wa mazao. Liko Shirika letu la SIDO. SIDO inafanya kazi nzuri, lakini imejikita kwenye vyuma sana. Vijijini huko tunaomba SIDO ijikite kwenye kilimo. Wataalam wa SIDO wafanye kazi za kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunakwenda kwenye hoja ya viwanda; nafahamu kwamba unapohitaji viwanda unahitaji uwe na ardhi, uwe na miundombinu, uwe na nguvu kazi yenye taaluma, unahitaji malighafi, mtaji, soko na teknolojia. Hivi ndiyo vitu vya msingi. Sasa hivi tunazungumza viwanda, lakini ardhi tunayo, je, hali ya miundombinu ikoje? Kiwanda kinahitaji maji, kinahitaji umeme. Hali ya nguvu kazi yetu ikoje?
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tunaenda kuanzisha Mchuchuma na Liganga kwa nguvu zote. Vijana wetu kule wana elimu gani juu ya nini kinaenda kufanyika kule? Pia liko suala la mitaji; mitaji tunaitoa wapi? Vijana kwanza hawana dhamana hiyo; moja, lakini vile vile riba ni juu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye Benki yetu ya Kilimo ina fedha kidogo mno; tuangalie sana katika huu utaratibu wa viwanda, tunapohamasisha viwanda, tunaweza tukajikuta hii nchi tunaigawa bure kwa wawekezaji na vijana wetu wanakuja mahali sasa wanakuwa watumwa ndani ya nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala la bodaboda. Vijana wengi ndiyo wanaendesha bodaboda na wamejiajiri kwenye bodaboda, leo hii wanaongezewa hii kodi. Vijana hawa ukiacha hii kodi ya usajili, lakini vile vile wana kodi za Halmashauri, vijana hawa wana kodi ya SUMATRA, wanalipa bima. Bima ya pikipiki moja ni sh. 60,000/=, unajiuliza mara mbili mbili, hivi ni kweli tumedhamiria kuwasaidia hawa vijana? Ukiangalia mpango wa Serikali sasa ni kwamba vijana wamiliki bodaboda zao. Ina maana tumewageuza vijana hawa kama kitega uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri jambo hili liangaliwe upya, vijana hawa sasa wapewe pikipiki hizi kama tunavyosema, ama waendeshe hizi pikipiki, lakini kodi nyingi zihamishiwe kwenye mafuta. Labda tuone, Serikali ije ituambie, hivi tukihamishia hizi kodi kwenye mafuta, kutatokea nini? Kwa sababu malalamiko haya yako mengi ya kodi ya SUMATRA, kodi za road licence, yako mengi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji vijana wafanye kazi kwa utulivu na tukiwawezesha vijana hawa wakalipa kupitia mafuta na wote wanatumia vyombo vya moto, tutaepuka usumbufu wa kukimbizana na askari, tutaepuka watu wa makampuni ya minada kuajiriwa na TRA, kukamata wasiolipa road licence.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ugumu gani hapa kufanya hii iingie kwenye mafuta? Kwa sababu tutasaidia vile vile magari mabovu; hatutalalamikiwa, kwa sababu mtu anasimamisha gari miaka miwili, akiingiza barabarani anaanza kudaiwa road licence. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iangalie ili kodi hizi ziingie kwenye mafuta. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie sula la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji…
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kuunga mkono hoja.