Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Innocent Lugha Bashungwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karagwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nianze kwa kukupa pole sana kwa changamoto ulizokumbana nazo lakini hata mimi nimekuwa na siku ngumu leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwanza kwa kuwashukuru wananchi wangu wa Karagwe kwa kuniamini na kunituma katika nafasi hii ya uwakilishi hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda nitumie nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais Magufuli na Serikali yake kwa kuanza kwa jitihada kubwa sana kutekeleza kaulimbiu ya „Hapa Kazi Tu‟.
Watanzania wengi wanamuunga mkono Mheshimiwa Rais na Serikali yake katika jitihada zake za kuhakikisha tunabana matumizi yasiyokuwa ya lazima ili fedha iende kwenye miradi ya maendeleo ya kuwasaidia Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili kuna jambo la ufisadi ambalo linaendeshwa kwa hii style ya operation tumbua majipu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais na kumwombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kuwa na moyo huu kwani kwa kuziba mianya ya upotevu kwa pesa sasa itakwenda kwenye huduma za jamii, wananchi wa Tanzania wapate dawa hospitalini na shule zetu ziwe na elimu bora na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitolea mfano wa Jimbo langu la Karagwe mpaka hivi sasa development grant hatujapata hata shilingi moja. Kwa hiyo, ni matumaini yangu katika jitihada hizi za kubana matumizi na kupambana na ufisadi ili hizi fedha ziende kwenye miradi ya huduma za jamii hata Jimbo langu la Karagwe mtatuangalia kwa jicho la huruma. Kwa sababu tumefikia katikati ya mwaka wa fedha lakini development grant hatujapata hata shilingi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamkumbuka Mheshimiwa Rais, wakati wa kampeni lile tukio la kihistoria la push ups lilitokea Karagwe kwenye viwanja vya Kayanga. Wanakaragwe wanamkumbuka sana na wana imani na Mheshimiwa Rais. Katika kampeni Mheshimiwa Rais aliahidi Wanakaragwe kwamba tutashirikiana kutatua mradi wa maji kwa sababu sehemu nyingi maji ni tabu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa maji wa Lwakajunju, ahadi hii imekuwa ni kiporo cha miaka mingi. Mheshimiwa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete aliahidi kwamba atawasaidia Wanakaragwe kuondokana na adha ya maji kwa kutoa maji Ziwa Lwakajunju lakini kwa miaka yote kumi mradi huu haukutekelezwa. Mheshimiwa Rais Magufuli alivyokuja kwenye kampeni Karagwe aliahidi kwamba akiwa Rais huu mradi wa maji wa Lwakajunju utatekelezwa haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais Magufuli aliahidi kwamba barabara ya Nyakahanga - Chamchuzi itapandishwa kwenye kiwango cha TANROADS na iwekwe kwenye mpango wa kuwekwa lami kwani kule Chamchuzi kuna ziwa ambalo linatutenganisha na Rwanda. Baada ya kuiweka barabara hii kwenye mpango wa TANROADS, Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba tutaweka kivuko ili kuboresha biashara kati ya sisi na wenzetu wa Rwanda.
Pia katika ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa wananchi wa Karagwe ipo Hospitali ya Wilaya. Karagwe hivi sasa ina wananchi shilingi 355,000/= na takwimu zinaonyesha kwa mwaka tunakua kwa wastani wa watu shilingi 10,000/=. Bila Hospitali ya Wilaya na hii idadi ya watu, kwa kweli tunapata adha kubwa sana. Tunaendelea kutegemea hospitali ya Kanisa la Lutheran, tunawashukuru sana lakini na wao wanaelemewa kwa hii idadi ya watu na ambao tunakua kwa wastani wa watu shilingi 10,000/= kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ahadi za Mheshimiwa Rais kuna suala la bei la kahawa. Napenda kuishukuru Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri Mwigulu kwa kukaa na Wabunge wanaotoka kwenye mikoa inayozalisha kahawa ili tuanze mchakato wa kupunguza hizi kodi ambazo ni kero kubwa kwa Watanzania wanaolima kahawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika ahadi za Mheshimiwa Rais lipo suala la kutatua migogoro ya ardhi. Napenda kutumia nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Lukuvi kwa kuanza vizuri kushirikiana na sisi kuhakikisha tunatatua migogoro ya ardhi. Katika hii awamu ya kujitahidi kuwa na uchumi wa viwanda, viwanda hivi havitajengwa kwenye sky, vitajengwa kwenye ardhi na ni vizuri tukatatua migogoro hii ili kuweza kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji wa ndani na nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ina upungufu wa walimu wasiopungua 400 hasa hasa wa shule za misingi. Naamini Waziri wa Elimu yumo humu ndani na kilio cha Wanakaragwe anakisikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kutumia nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kusambaza umeme vijijini. Wilaya ya Karagwe imepata umeme huu wa REA lakini kuna vijiji vingi bado havijapata. Naamini Serikali itajitahidi ili wale wananchi ambao hawajapata umeme katika Wilaya ya Karagwe nao wapate ili ahadi ambazo tumeahidi wakati wa kampeni ziweze kutekelezwa kwa muda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kushauri Serikali, kuna mfuko wa Halmashauri wa kukopesha vijana na akina mama. Kwa ninavyoona, tutafute namna ya kukuza mfuko huu ili uweze kukopesha vijana na akina mama zaidi kwani kama mnavyofahamu tatizo la ajira kwa vijana na akina mama ni la kitaifa na kwa kukuza mfuko huu wa Halmashauri tutakuwa tumewasaidia vijana wengi kujiajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia kero za Karagwe. Sasa niende kwenye machache ya kuishauri Serikali katika jitihada zake za kujenga uchumi wa viwanda. Pamoja na jitihada za kupambana na ufisadi ili kukuza mapato ya ndani ya nchi, hii peke yake haiwezi kutosha hata tukitumbua majipu namna gani. Lazima Serikali ijipange katika kuhakikisha tunajenga miundombinu ambayo itasaidia kukuza sekta binafsi lakini wakati huohuo itasaidia nchi yetu kupata kipato zaidi. Kwa mfano tuna natural harbors, hizi bandari tukiziboresha na zikawa efficient, landlocked countries ambazo zinatuzunguka zitaweza kupitisha cargos zao nyingi na tutaweza kupata mapato kwa njia ya customs. Hiyo itakuwa ni income lakini kwa wakati huohuo itakuwa imejenga miundombinu ya kusaidia sekta yetu binafsi ikue.
Mheshimiwa wenyekiti, pia ipo haja ya kujenga reli nchini na kuunganisha na nchi za jirani ili kukuza biashara na uchumi wetu. Kama takwimu za TRA zinavyoonyesha, mapato makubwa tunayapata kupitia customs. Kwa hiyo, ujenzi wa bandari na reli siwezi kusisitiza vya kutosha namna ambavyo tukizijenga pamoja na kwamba zipo capital intensive, zitatusaidia sana kukuza mapato, kuongeza tax base ili hii flow ya income kupitia customs iweze kukua kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kuhusu nia ya Serikali ya kuwa na uchumi wa viwanda. Napenda kutoa angalizo. Ukiangalia takwimu za mwaka jana kwa ukuaji wa sekta, sekta ya mawasiliano ilikua kwa 15.3%, sekta ya ujenzi ikakua kwa 13%, huduma za fedha 9.9%, usafirishaji 8.8%...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge ahsante, muda wako umekwisha.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)