Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyo mbele yetu, hoja ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru sana wewe na kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa nafasi ya kuweza kusimama na kuweza kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu iliyo mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nianze kuungana na Wabunge wenzangu wote kukupongeza sana wewe Naibu Spika kwa kazi nzuri unayoifanya ya kuendesha Bunge letu Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa weledi na uwezo mkubwa sana wa kiwango cha kupigiwa mfano. Hakika Dkt. Tulia ni kijana mdogo, ni mara yako ya kwanza kuwa Naibu Spika na ni mama ambaye kwa muda mfupi umetushangaza wanawake, umewashangaza Watanzania na umeshangaza hata ulimwengu kwa jinsi ulivyo mwaminifu, mvumilivu na siyo hivyo tu na jinsi unavyojua Kanuni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, umetukumbusha mpaka enzi za Mzee Mkwawa na Maspika waliopita. Una muda mfupi ndani ya Bunge, umepitia Hansard kwa muda mfupi na kila unaporejea Kanuni pia unarejea Hansard na unatoa mifano ya Maspika wenzako. Kwa kweli, wale wanaokubeza nakuambia lala usingizi, wanawake tupo nyuma yako na tumejiandaa kikamilifu, wameanza wao tutamalizia sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema hatuna muda wa kupoteza, mara baada ya Bunge Tukufu kukamilisha kazi zake utatusikia na huko tutakwenda kuongea na wananchi kwa sababu uwezo tunao. Dkt. Tulia tutakutetea, chapa kazi na tupo nyuma yako maana kama ingekuwa ni adhabu wangempa Mzee Chenge ambaye yeye ndiye aliyewatoa leo iweje wanakususia wewe ambaye umesimamia Kanuni na taratibu za Bunge! Hongera sana Dkt. Tulia, songa mbele, tupo nyuma yako, Watanzania na wananchi wenye weledi wanakuunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waswahili wanasema ukiona baadhi ya wanaume anapokalia mwanamke kiti wanakimbia, nafikiri hapo jibu lao mnalo, maana mwanaume hakimbii boma. CCM oyee, aah, sorry. (Makofi/Kicheko) [Maneno haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo, nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja hii ya bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa asilimia 100 na sababu ninazo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya kwanza ya kuunga mkono, Mheshimiwa Waziri na timu yake yote imeandaa bajeti hii kwa weledi wa hali ya juu sana. Bajeti hii kwa kweli imekonga moyo wangu na imekonga mioyo ya Watanzania kwa sababu ni bajeti inayokwenda kujibu matatizo ya wananchi, inakwenda kujibu kero za wananchi, inakwenda kuwapa wananchi fursa mbalimbali katika utekelezaji wa Ilani ya CCM, inakwenda kutekelezwa kwa kuhakikisha inaweka nidhamu ya uwajibikaji ndani ya watumishi wa umma na siyo kwa watumishi wa umma peke yake na hata wananchi na inakwenda pia kutekeleza maandiko ya Vitabu Vitakatifu ambavyo vinasema asiyefanya kazi na asile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Fedha na timu yake kwa sababu bajeti hii pia inakwenda kuondoa kodi zote ambazo zilikuwa ni kero kwa wananchi. Mfano, bajeti hii inakwenda sasa kuondoa kodi ya madawa ya maji, mimi kama mama ni jambo ambalo nimelizungumza. Katika miaka mitano nilikuwa kwenye Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, Kamati ile ilipiga kelele kwa miaka mitano haikufanikiwa lakini bajeti hii inakuja na pendekezo la sisi Wabunge kwenda kuondoa kodi ya madawa ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii inakuja na pendekezo la kuondoa ushuru na kodi katika mazao ya kunde ikiwemo maharage ya soya, karanga na siyo hivyo tu, mboga mboga na hata mazao mengine ambayo yanakwenda sasa kuimarisha lishe ya Watanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba kwa mujibu wa tafiti zilizofanyika inaonesha bado Tanzania na hasa watoto na wanawake wanaojifungua wana utapiamlo. Kwa hiyo, kupitia bajeti hii pia inakwenda kuwakomboa wanawake na watoto kwa sababu imeondoa kero ambazo ni sumbufu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo nijielekeze katika mambo ambayo nimechagua kuyazungumzia ambayo ni machache kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nimefurahishwa na kufutwa misamaha ya kodi ambayo haileti tija kwa wananchi na moja ya jambo hili ni kwenda kufuta misamaha ya kodi katika maduka ya majeshi na maduka mengine katika taasisi zetu za kijeshi. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hapa asituambie kwamba atakwenda kushauriana na viongozi wa wakuu wa majeshi, no! Namuomba na kumshauri aje kabisa na mpango mzima utakavyokuwa, kama inawekwa posho kwa ajili ya hawa askari wetu ijulikane, kama ni shilingi laki moja kwa mwezi ijulikane, ni shilingi laki moja na hamsini ijulikane. Maana akisema anakwenda kushauriana nao endapo watasema ni shilingi laki tatu ataipata kupitia bajeti ipi? Ina maana itakuwa ni mwaka mwingine wa fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hivyo kwa sababu askari wa nchi hii wamenituma, ma-CP, ma-WP ma-Constable huwa naongea nao sana, wanataka Serikali itoe kauli leo kwamba inakwenda kufanyaje sasa kwa sababu ushuru umeondolewa katika maduka yale ambayo yalikuwa ni msaada kwao. Serikali iweke kabisa fedha kama ni shilingi laki moja na hamsini kama ni shilingi laki tatu kwa kila mwezi ijulikane badala ya kwenda kufanya mazungumzo na viongozi wa jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu nyingine ni suala zima la kupeleka fedha kwa Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali. Naomba niungane na wenzangu wote walioiomba Serikali yetu Tukufu ambayo ni sikuvu kuongeza fedha, shilingi bilioni 47 kwa ajili ya CAG haitoshi! Kwa bahati njema katika Bunge hili umenipa fursa ya kuwa Mjumbe wa Kamati ya LAAC kwa muda mfupi tumekagua Halmashauri 30 hazikufanya vizuri, tumejionea madudu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za miradi ya maendeleo zinaliwa sana kwenye baadhi ya Halmashauri zetu lakini Mkaguzi wa Hesabu za Serikali ndiye anayetuletea taarifa. Wenzangu wameshafanya uchambuzi sitapenda kurudia, ili TAKUKURU aweze kufanya kazi yake vizuri lazima na huyu CAG tumpe fedha ili ziende kutekeleza kazi ambayo tumekusudia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waliposikia kwamba CAG hana fedha baadhi ya Wakurugenzi wasio waaminifu wameanza kushangilia maana wanajua kuna baadhi ya madudu yanafanyika huko hawachukuliwi hatua yoyote, CAG peke yake ndiye atakayetukomboa. Tunamuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha hebu akae na timu yake tena, akaa na timu ya Mama Segasia na wenzake, wajaribu kuona ni wapi wanaweza wakapunguza fedha tukampa huyu CAG ili aweze kufanya kazi yake kikamilifu. Changamoto ya kukosa fedha tumeshaanza kuiona. Mimi niko kwenye Kamati ya LAAC, sasa hivi tunajiandaa kwenda Mikoani, tunajiandaa kuita Halmashauri, unamuona CAG anavyokuja anasuasua maana fedha anazopata hazitoshi. Kama hatumpi fedha za kutosha CAG, tutatenga fedha lakini zitaishia mikononi mwa wajanja kwa sababu watakwenda kufanya sivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie utaratibu wa upelekaji wa ujenzi wa miundombinu ya maji katika Serikali yetu. Hapa naomba nianze kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana ambayo imekuwa ikifanya. Tumejionea wenyewe imejenga miradi mikubwa sana ikiwemo jiji la Dar es Salaam na katika miji mingine saba hapa nchini na miradi ya mikakati katika nchi yetu na taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha imeeleza vizuri zaidi na hata taarifa ya Wizara ya Maji. Ombi langu kwa Serikali, kwa sababu zipo shilingi milioni 900 zimetengwa kwa ajili ya maji, tunaomba ule mfuko kwa ajili ya kupeleka maji vijijini uimarishwe, badala ya kutoza Sh.50 kwa kila lita ya mafuta ya diesel na lita 50 ya petrol iwe Sh.100. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu hali ya upatikanaji wa maji na hasa vijijini ni mbaya sana. Mheshimiwa Waziri sijui kama amepata fursa ya kwenda vijijini, mimi ninayezungumza ni mdau wa wanawake na nikienda vijijini sifanyi mikutano ya ndani naitisha mikutano ya hadhara. Hivi navyozungumza nimetoka site siongei mambo ya mezani. Napoitisha mikutano ya hadhara kuongea na wananchi ukiuliza kero ya kwanza kwa wananchi wote, wanawake, wanaume, vijana na watoto ni maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa jinsi alivyoanza kazi vizuri hebu sasa huu Mfuko wa Maji akubali uongezwe tozo kutoka Sh.50 mpaka Sh.100 kwa kila lita ya diesel na lita ya petrol. Ushauri huu unakuja sasa mara ya pili, Wizara ya Fedha kuna kigugumizi gani cha kufanya uamuzi? Mnahofia kwamba eti mkipandisha hapa wananchi watapata matatizo, siyo sawa. Nawaomba sana mshughulikie suala hili kwani kero ya maji ndiyo changamoto ya kwanza. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.