Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi, na kwa kweli hii ni nafasi ambayo nilikuwa naisubiri kwa hamu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie mambo mawili ambayo yanaendelea katika Jimbo langu. Mwaka 2011 nilisimama katika Bunge hili nikasema Jimbo la Rombo halina hifadhi ya wanyama, nilisema hivyo kwa sababu tembo kutoka Kenya, Mbuga ya Tsavo pamoja na Amboseli walileta maafa makubwa sana katika Jimbo langu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, karibu vijiji 20, Kata ya Holili, kijiji cha Kidondoni Kata ya Chana, kijiji cha Ngoyoni, kijiji cha Ngareni, Shimbi Kati, Kiraeni, Msaranga, Mahorosha, Leto, Urauri na Rongai, mazao ya wananchi yaliliwa na tembo, wananchi waliuawa na wengine wakapata vilema vya kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi ya fidia yalipelekwa Wizarani kuanzia mwaka 2012 hadi leo hakuna majibu, hakuna chochote. Ninaiomba sana Wizara ishughulikie jambo hili kwa sababu ni kero na wananchi wamejenga chuki kubwa kati yao na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iliahidi kutujengea vituo vya kudhibiti wanyama pori. Iliahidi kutujengea vituo vitatu, kimoja Ngoyoni, kituo cha pili Mahorosha na kituo cha tatu Kikelelwa, hadi sasa ni kituo kimoja tu kimejengwa. Naomba Wizara ifanye jitihada za kuhakikisha kwamba vituo vingine viwili vimekamilishwa na ninapenda nimsikie Waziri wakati anafanya majumuisho ili kero hii iishe moja kwa moja kwa wananchi wa Rombo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kero nyingine ambayo ningependa kuizungumza ni uvamizi wa nyani kutoka mlima Kilimanjaro. Kijiografia, Mlima Kilimanjaro wote uko katika Jimbo la Rombo, pamoja na kwamba mlima huu unahudumiwa na Halmashauri zote ambazo zinazunguka ule mlima. Mlima Kilimanjaro ukiungua ni wananchi wa Rombo wanaswagwa kwenda kuzima moto mlimani. Wapo waliovunjika, wapo waliokuwa vilema kwa sababu ya kwenda kuzima moto, wanachoambulia ni nusu mkate kwa kila anaekwenda kuzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lucy Owenya amezungumza hapa imefika wakati Mheshimiwa Maghembe, wananchi wa Rombo na Halmashauri zinazozunguka Mlima Kilimanjaro tunataka mrabaha kama wenzetu wa madini wanavyopata. Vinginevyo tumedhamiria safari hii mlima ukiungua hatuzimi, mje mzime wenyewe. Kwa sababu mlima unaingizia TANAPA zaidi ya shilingi bilioni 60 kwa mwaka, lakini hakuna ambacho Halmashauri hizi hususan watu wangu wa Rombo wanakipata zaidi ya vilema ambavyo vinatokana na maporomoko wakati wanaenda kuzima moto mlimani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kama vile haitoshi mlikuwa mmetupa half mile kwa ajili ya akina mama kwenda kukata kuni pamoja na majani mkijua kabisa kwamba Jimbo la Rombo ardhi yetu ni ndogo na kwa sababu hiyo hatuna maeneo ya kuswaga wanyama wetu, wanyama wetu tunawaweka ndani.
Kwa hiyo, eneo lile mlitupa, tulikuwa tunapata majani pamoja na kuni, sasa taabu tunayoipata ni kwamba wananchi ambao wanaishi karibu na eneo hili, vijiji vya Masho, Maharo, Mokara, Ubaa, Mashuba, Kirwa, Katangara, Lesoroma wanapata shida mbili; shida ya kwanza ni kwamba kila wanapolima nyani wanatoka mlimani wanakula mahindi yao yote na mwaka huu wameshindwa kulima kwasababu ya shida ya nyani, KINAPA hawataki kutuwezesha ili kupambana na wale nyani. Shida ya pili ni akina mama ambao wanakwenda kwenye ile half mile kwa ajili ya majani na kuni kinachowapata ni kwamba wanatandikwa viboko, wengine wanabakwa, wengine wananyang‟anywa vifaa vyao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme mwaka jana askari wa KINAPA waliwakamata akina mama wafuatao, Ndugu Selfina Mtengesi Luka wa Kitongoji cha Mori, Ndugu Fabiola Joseph, Ndugu Rose Luka, Ndugu Witness John, Ndugu Rafia Makongoro wa Kitongoji cha Kimongoni, wakawalaza chini na kuwatandika viboko. Ninaiambia Serikali tabia hii ya askari wenu kupiga wananchi hovyo hovyo, mnawakomaza na mnaleta matatizo katika nchi kwa sababu itafika mahali watasema hapana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba wakati wa kufanya mjumuisho aibu hii ambayo imetokea Rombo ya akina mama ambao hawajawahi hata kupigwa na waume zao wanaambiwa walale chini, watandikwe viboko vya makalio katika Serikali hii ambayo tunasema ni Serikali yenye amani na utulivu, uniambie ni hatua gani zitakazochukuliwa, kwa sababu ikiendelea hivi itafika mahali sisi tutasema hapana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiondoka kwenye masuala yanyohusu Jimbo langu, ni kwamba tunazungumza habari ya utalii lakini kuna mambo mengi sana katika nchi yetu ambayo tungeweza tukayatumia yakatuletea uchumi mzuri tu. Kamati ya Bajeti chini ya Mheshimiwa Chenge mwaka jana nakumbuka tulienda Dubai kwa ajili ya semina wakatucheka, wakatuambia mnahangaika na vitu chungu nzima, utalii peke yake ungefanya Tanzania ikawa kitu cha ajabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza habari ya Serengeti, habari ya Mlima Kilimanjaro na kadhalika, mbona kuna vitu vingi vinapotea? Mimi nashangaa watu wanakuja kutalii Bungeni hapa, nashangaa. Kila Halmashauri TANAPA ingeweza ikaamua kujenga makumbusho katika kila Halmashauri watu wakaenda kujifunza habari ya vita ya Maji Maji, watu wakaenda kujifunza kwa mfano pale Kilwa pana handaki linakwenda mpaka Mombasa, linafukiwa tu. Pale Rombo kuna Kata inaitwa Keni, kuna handaki Machifu walichimba zamani linatoka Keni linaenda mpaka Wilayani, yanafukiwa tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa walivyotumia wazee wetu akina Mirambo, akina Mkwawa, akina Mangi Mareale, vinapotea mnaona tu, hakuna mtu anayejali ajenge makumbusho avihifadhi viweze…
MWENYEKITI: Ahsante.