Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Vicky Paschal Kamata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. VICKY P. KAMATA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana. Nami nianze kwa kuunga hoja mkono na kumpongeza sana Waziri na Naibu Waziri kwa hotuba yao nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hifadhi zetu kuna madini mengi sana na ili Mtanzania aweze kuyachimba lazima apate kibali kutoka kwa Wakala wa Misitu. Akishakipata kile kibali anatakiwa kulipia ada milioni moja kwa mwaka na kama ana hekta kumi ina maana atalipa milioni kumi. Vilevile anatakiwa kulipia leseni 800,000 kila mwaka. Wakati huo huo anatakiwa kulipa asilimia nne kama loyality.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni maombi ya wachimbaji wadogo wa Geita wamenituma nimweleze Waziri kwamba wanaomba sana kwamba hili haliwasaidii wachimbaji wadogo wadogo kwa sababu ada ile ni kubwa, lakini pia wanachangia maendeleo siyo kitu kibaya, kwa kuwa wanachangia maendeleo basi wafikiriwe kupunguziwa. Hilo ni ombi maalum kutoka kwa wachimbaji wadogo wa Geita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumzie kidogo hili jambo ambalo limezungumziwa sana na Wabunge wenzangu linalohusu wafugaji. Mimi pia ni mfugaji na nimetoka sehemu ya wafugaji. Naungana mkono na wale wenzangu wanaosema kweli kuna umuhimu wa kuwashawishi wafugaji wetu kuona kama inawezekana wakapunguza hii mifugo ambayo pengine imekuwa mingi kama ambavyo mnasema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini natofautiana na wenzangu kwa namna wanayosema mifugo hii ipinguzwe. Isipunguzwe kwa kuwaumiza hawa wafugaji lakini ipunguzwe kwa kuwanufaisha, huo upunguzaji uwe na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kaka yangu Dotto aliongea na mimi nilipata uchungu sana. Inaumiza kuona mfugaji anauliwa mifugo yake ng‟ombe sitini, ishirini, thelathini, yaani hiyo ni torturing ya aina gani? Yaani jiweke tu kwenye viatu vya huyo mfugaji maumivu aliyoyapata, achilia mbali hasara kwamsababu mtu anapofuga kitu tayari anammapenzi nacho. Mimi ni mfugaji nina mbwa kama wanne nyumbani kwangu. Hivi juzi kuna mbwa mmoja, amekufa katika mazingira ambayo mimi sikuyaelewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hao mbwa nilikuwa nampenda sana yule mbwa, amekufa sikuelewa amekufaje, mpaka hivi ninavyozungumza ameniuma na ni mbwa tu mmoja, hebu fikiria hawa ng‟ombe sitini ana maumivu kiasi gani? Yapo mengi ya kuwasaidia wafugaji wetu wakafuga katika hali nzuri na wakanufaika na mifugo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimshauri Mheshimiwa Waziri akae vizuri na Waziri wa Mifugo, wakae vizuri na Waziri wa Ardhi, wakae vizuri pia na Waziri wa Viwanda waje na Mkakati Maalum wa kuwasaidia hawa wafugaji ili wasije wakajiona kwamba kumbe kufuga katika nchi hii ya Tanzania ni mateso.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa Serikali ikishirikiana na hawa wafugaji ambao wana mifugo mingi na wana pesa nyingi, wanaweza wakawasaidia hata wakaenda kujifunza kwa wenzetu Netherland wanafugaje! Ufugaji wao utakuwa ufugaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nilikuwa najaribu ku-google kidogo asubuhi, nijaribu kuona wenzetu walifanyaje. Netherland wanafuga na ufugaji wao una tija, sitaki kujilinganisha nao kwa sababu wenzetu wako mbali sana, lakini bado tunaweza tukajifunza kutoka kwao. Serikali ikawasaidia hawa wafugaji, ikachukua labda kila mkoa ambao una wafugaji wengi wakachukuliwa kumi au kumi na tano ama ishirini wakaenda kule Netherland wakaenda kujifunza, kuna teknolojia nzuri kabisa ambayo wakirudi nayo hawa wafugaji watakubali wenyewe kwa kusema kwamba tunapunguza mifugo na sisi tunafuga kisasa na ufugaji wetu uweze kuwa na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanayo teknolojia nzuri sana ambayo siwezi kuizungumza hapa, nimejifunza mimi leo hii, lakini naamini Mheshimiwa Waziri akiifanyia kazi, akashirikiana na hawa wafugaji; kwanza wana pesa wanaweza hata wao wenyewe wakajilipia ndege na hoteli kule wakaenda kujifunza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile vijana wetu wanaosoma vyuo vikuu, wanaosomea mambo ya kilimo, tuwapeleke nje wakasome. Hili jambo hatuwezi tukaliondoa haraka sana bali taratibu, kama kweli tunataka ufugaji upungue, watu wasifuge ng‟ombe elfu thelathini, wasifuge ng‟ombe wengi kiasi hicho, tusiwakatili ghafla sasa kwamba mnaanza kufuga ng‟ombe watano, mwisho kumi, hapana. Taratibu, taratibu kwa kuanza na mind set zao, tuwaelimishe kwanza kwa kuwapa hiyo exposure, waende wakajifunze, warudi na vijana wetu wanaosoma pia watatusaidia kuhakikisha kwamba ufugaji wetu unakuwa na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilivyosema Mheshimiwa Waziri akae na Wizara hizo kwa maana ya Wizara ya Ardhi, Wizara ya Viwanda bado naona kuna umuhimu wa kutengewa maeneo. Watengewe maeneo maalum ili waweze kulisha mifugo yao wakati tukiendelea huko kwenye teknolojia ya kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo kuhusu suala la utalii, nilipokuwa naangalia hiki kitabu ukurasa wa 15 nimeona jinsi ambavyo, (sintasoma) lakini nimeona jinsi ambavyo utalii umeweza kuchangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa, nawapongeza sana. Ninaamini bado kuna vitu vya ziada vya kufanya ili utalii huu uweze kutuletea pato kubwa sana kwenye Taifa letu na kukuza uchumi wa nchi yetu. Kwa mfano, tukiamua kumleta Jay Z na familia yake hapa, tukamleta David Beckham na Victoria Beckham hapa, tukakubaliana nao kabisa kwamba hiyo tour yao iwe broadcasted na vyombo vyote vikubwa vikaimulika Tanzania kwa siku zote watakazo kaa hapa, Serikali mkakubali kabisa kuwa-host, wakawa kila mahali wanapoenda vyombo vyote viimulike Tanzania, ninaamini watajua Mlima Kilimanjaro uko Tanzania maana sasa hivi tunalalmika tu, ooh, Kenya wanasema Mlima Kilimanjaro uko kwao, ili tuioneshe dunia kwamba mlima Kilimanjaro uko Tanzania tukubali kuingia gharama kama hizo, tuwalete watu maarufu duniani, watembelee Mlima Kilimanjaro, vyombo vyote vikubwa vya habari vimulike nchi yetu, kila mahali wanakoenda wamulikwe, itaonekana kumbe Mlima Kilimanjaro uko Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unyayo ambao yule binti wa Kenya alikurupuka akasema sijui Olduvai Gorge iko Kenya tutawa-prove wrong kwamba kumbe haiko Kenya iko Tanzania kwa kuwaleta watu mashuhuri wakatembelea hayo maeneo. Waende Rubondo, Rubondo - Geita kuna hifadhi zetu nzuri sana pale, lakini haijulikani. Wakija watu kama hao wakatembelea hata hivi vivutio vyetu ambavyo havijulikani itakuwa mojawapo ya kuvitangaza na watalii wengi watakuja na mwisho wa siku tutapata pesa nzuri sana. (MakofI)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema Tanzania hii ndiyo nchi pekee tunatoa Tanzanite, ninasikitika sana kuona kwamba hatujitangazi kwamba hata hii Tanzanite inatoka kwetu. Hao hao akina Jay Z wakija hapa wakaenda kwenye duka moja hapo Arusha itajulikana kumbe Tanzanite inatoka Tanzania. Camilla alikuja hapa na Prince Charles wakenda pale Cultural Heritage wakanunua Tanzanite nyingi, lakini hakuna mtu aliyejua kwamba wamekuja lakini kama tungekuwa tuliongea nao, tukafanya utaratibu, wakaonekana wakiwa kwenye lile duka walilonunua zile Tanzanite tayari tungekuwa tumeonesha dunia kwamba Tanzanite iko kwetu na tayari tungevutia watu wengi kuja kutalii hapa nchini kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa utalii unaweza ukawa chanzo kikubwa sana cha mapato kuliko hapa huu ukurasa wa 15 unavyosema. Naamini tunaweza kufanya vizuri zaidi na zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nimpongeze Waziri na nimtakie kila la kheri nikiamini kwamba atayazingatia hayo.