Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niwe miongoni mwa wachangiaji kwenye hotuba ya bajeti. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Wanafanya kazi ya kuwasaidia Watanzania hasa wale wenye kipato cha chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwenye eneo la mfumo wa bandari. Kwenye eneo la bandari yapo makubaliano ambayo yamekubaliana kati ya nchi yetu na nchi ya Kongo, Zambia na Malawi. Mfumo huu wa single customs territory ni mfumo ambao unadidimiza mapato ya nchi yetu. Ukusanyaji wa mapato unakuwa kidogo kwa sababu wale wafanyabiashara ambao walikuwa wanatumia bandari yetu wameihama, wamekimbilia kwenye bandari nyingine za nchi jirani. Bandari hizo ni bandari za Durban, Bandari ya Mombasa, Bandari ya Msumbiji ambazo ziko jirani, wanakwepa masharti ambayo kimsingi makubaliano yale hayainufaishi nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba Serikali iangalie mfumo huu, iurekebishe mapema ili tuweze kutoa wigo mkubwa sana wa ukusanyaji wa mapato kwa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo kodi nyingize ambazo zinawafanya wafanya biashara waweze kukimbia. Mfano nchi ya Zambia mizigo inayoletwa nchini wanatozwa gharama kubwa sana kiasi kwamba wale watu ambao wanatumia bandari yetu wanakimbia. Ni vyema Serikali ikaangalia ni sababu zipi zinazofanya mizigo ya kutoka Zambia iwe na gharama kubwa kuliko maeneo mengine ya watumiaji wa bandari hii?
Naomba Serikali iangalie kwa makini sana, tukiboresha kwenye maeneo haya, tutaisaidia nchi yetu iweze kupata mapato makubwa sana kwa sababu watumiaji wa bandari hii watakuwa wengi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasisitiza hili kwa sababu siasa za sasa hivi ni uchumi. Wenzetu ambao wametuzunguka, wanatumia udhaifu tunaokuwa tumejiwekea sisi wenyewe. Mnakubaliana kwenye makubaliano halisi, lakini kwenye utekelezaji wao ndio wa kwanza kuvunja yale makubaliano, sisi tunabaki tumeng’ang’ania vitu ambavyo havitusaidii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika eneo la pili ni eneo la ukusanyaji wa mapato ambao Serikali imekuja na mpango wa kuongeza VAT juu ya utalii. Kwa hesabu za haraka haraka tu, tukitekeleza hili ambalo limeletwa na Serikali, watalii wanaokuja nchini watapungua kwa kiwango kikubwa sana na hii intatoa fursa kwa nchi jirani ya Kenya iweze kutumia udhaifu wa kwetu sisi kama nchi uweze kuwanufaisha wao Wakenya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali iangalie na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana aone umuhimu wa hili jambo kwamba halitawasaidia Watanzania, linawasaidia jirani zetu ambao wanapakana na sisi na watumia udhaifu wetu, wanajua kabisa kwamba hiki kitu hakiwezi kuwasaidia Watanzania. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iangalie kwenye maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni mapato ya Halmashauri kukusanywa na TRA. Serikali imekuja na nia njema kutaka kusaidia mazingira ya uboreshaji wa ukusanyaji wa mapato, lakini tunapata shaka sana; kama Serikali kipindi chote imekuwa ikikusanya mapato na kurudisha fedha kule kwenye Halmashauri, fedha hazifiki. Leo hii tunawapa jukumu la kukusanya wao, hata kile ambacho kimekuwa kikiwasaidia kitatoweka kabisa. Tunaangalia miaka hii mitatu, upelekaji wa fedha wa Serikali kwenda kwa walengwa ulikuwa hafifu sana, unakuta asilimia 40 mpaka asilimia 45. Sasa leo hii fedha zote zibaki zinamilikiwa na Serikali Kuu, tutakua tunaziua Halmashauri zetu. Naomba na hili mliangalie. Ni vyema tukatizama vitu ambavyo vitawasaidia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kila kitu kama kitakusanywa na Serikali Kuu, huku chini mimi sina imani kwamba hizi fedha zitawafikia walengwa. Kwenye eneo la Halmashauri za Wilaya ndiko ambako kuna utekelezaji mkubwa wa fedha zinazopelekwa kule, kunakuwa na utekelezaji wa shughuli za maendeleo. Tunahitaji tupate huduma za maji, tunahitaji tuboreshe barabara vijijini na tunahitaji tupate huduma za afya zilizo bora. Kama Serikali haitakuwa imepeleka mazingira mazuri ya kuangalia fedha hizi, nawaambia tutakuja kulaumiana na Serikali itajuta kwa sababu sina imani itaweza kukusanya kadri wanavyokusanya sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali, kuna maeneo kwenye suala la uwiano wa fedha za miradi. Pamoja na kwamba Serikali ina nia njema ya kupeleka huduma zilizo sawa kwa wananchi, bahati mbaya sana Wizara husika ya Fedha bado haitumii uwiano ulio sawa wa kupeleka fedha kwenye Mikoa mbalimbali. Fedha nyingi zimekuwa zikipelekwa maeneo ambayo baadhi na sehemu nyingine hawapati kabisa hizo fedha. Naomba Serikali kwa sasa ibadili mfumo na iangalie uhalisia wa kusaidia hasa ile Mikoa ambayo ilisahaulika, ambayo iko nyuma kimaendeleo, wapelekewe fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, ipo Mikoa mipya, Wilaya mpya ambazo zina changamoto nyingi mno. Tunaomba Serikali ipeleke fedha zikasaidie kutekeleza miradi ya shughuli za maendeleo kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, zipo Wilaya nyingi sana ambazo ni mpya ikiwemo Wilaya mpya ya Tanganyika kule Jimboni kwangu Mkoa wa Katavi; lakini zipo Wilaya ambazo zinahitaji kusaidiwa kama Buhigwe, Chemba na Mlele. Zile Wilaya zinahitaji sana kupata fedha ambazo zitainua shughuli za maendeleo kwenye maeneo yao na kuna changamoto kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie eneo la kuziunganisha taasisi hizi za Kampuni ya TRL, RAHCO; TPA na Marine Service. Naomba Mheshimiwa Waziri, hizi kampuni ziunganisheni ziwe kitu kimoja ili ziweze kutoa huduma kwa wananchi. Kuongeza haya makampuni kila sehemu inafanya kazi zake, hakuna ufanisi wa aina yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, tumeangalia eneo hili kuna shida kubwa sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri muangalie sheria ile ambayo ilifanya kuwe na mgawanyo ije mwilete hapa Bungeni tuirekebeshe ili haya makampuni yaunganishwe na yafanywe kitu kimoja ambacho kitawasaidia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nami naungana na wenzangu kwenye suala la gratuity. Ni vyema Mheshimiwa Waziri ukatafakari, ukaangalia na ukaona umuhimu mkubwa kwamba Waheshimiwa Wabunge wanafanya kazi kubwa sana. Hawana pensheni; hiyo wanayopewa ni kama Honoraria tu, kwa sababu ndiyo malipo yao ya mwisho kwa kazi ambazo walizifanya. Nawaomba Mheshimiwa Waziri uangalie changamoto ambazo wanazifanya Waheshimiwa Wabunge. Naamini ungelikuwa umeshaonja nawe ukawa Mbunge wa Jimbo, ungeona adha yake ilivyo. Karibu misiba yote ni ya Mbunge, mahafali yote ni ya Mbunge, harusi zote za Mbunge, kila kitu kilichopo kwenye jamii kinamwandama Mbunge. Naomba katika hili uliangalie, siyo kwa Waheshimiwa Wabunge tu, lazima tuone kwenye maeneo yote yanayohusiana na mapendekeza yako.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, isije kengele ikanililia. Naunga mkono hoja. Ahsante.