Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia kwenye bajeti yetu ya kwanza kabisa ya Serikali ya Awamu hii ya Tano. Nakushukuru sana kwa sababu nafasi hizi ni adimu na Wabunge ni wengi na tuna hamu sana ya kuishauri Serikali. Niiambie tu Serikali kuanzia kwa Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango, fungueni masikio msikie Waheshimiwa Wabunge wanasema nini, msizibe masikio. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la ku-withdraw benefits. Mimi niseme nimefanya kazi mining, najua shida za waajiri wa aina ile na makampuni yanayofanana nayo. Naishangaa sana Serikali kukazia hapo, kutaka watu wakae mpaka miaka 55, wakati Serikali hii inayaruhusu makampuni mbalimbali kuingia mikataba ya mwaka mmoja mmoja. Sasa kama mtu anafanya kazi mwaka mmoja anaingia mkataba mwingine na mwingine, stability ya ajira yake haipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nashauri hebu watu hawa waachwe; mtu akimaliza kazi yake achukue chake. Hakuna haja ya kuwazuia. Labda kwa sababu Serikali inakopakopa hizi fedha za wafanyakazi, kwa hiyo, naona ili kuzifanya ziwepo, ni kuwazuia watu kuchukua. Kazi za sasa huwezi kuwapata watu wenye umri zaidi ya miaka 50, kama akina Mheshimiwa Kadutu. Vijana wengi wako chini ya miaka 20, 28 au 30, anafanya kazi mwaka mmoja, mwaka wa pili kaenda kwingine; lakini kuna uwezekano wa kukosa kazi kwa miaka hata sita.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, aendelee kusubiri miaka 55? Nadhani siyo jambo jema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, migodini kule ziko kampuni ambazo zina mikataba na makampuni mama kwa maana ya yanayoendesha migodi, lakini zile kampuni kwenye Mikataba ya Wafanyakazi zimeweka sharti kwamba pindi mkataba wa kampuni mama na kampuni hiyo nyingine ndogo utakapokwisha au utakapositishwa, automatic na wewe mfanyakazi mkataba umekwisha. Sasa mtu huyu unataka abaki aje kuwa mzee, ni nani atakayekubali kufanya kazi katika mazingira hayo?
Kwa hiyo, nilikuwa nadhani muda umefika, itatamkwe tu; Serikali itamke, mtu akiachana na mwajiri wake, kwa nini iwe kikwazo? Kwanza siku hizi mmetoa ruhusa ya kuchangia mfuko wowote unaotaka, kwa nini iwe kikwazo mtu kuchukua amana zako? Hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni hili ambalo kila Mbunge analisema, nami nadhani Dkt. Mpango utakuwa umesikia vizuri. Kila Mbunge anaposimama anasema hapana. Basi hapana hii iwe maana yake hapana. Hivi unataka kutoza kodi kwa Mbunge; nawaambieni Waheshimiwa Wabunge sisi tuko tofauti na wafanyakazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wako Wabunge hapa wanachangia maendeleo ya majimbo yao kwa shilingi milioni 500 mpaka shilingi bilioni moja. Je, na sisi tuanze kuandika invoice kuidai Serikali? Yako maeneo yamepangiwa pesa hayakupelekewa pesa hata senti tano, lakini shughuli za maendeleo zinakwenda. Sasa je, na sisi tuanze kuidai Serikali? Kwa sababu wajibu wa kufanya kazi hiyo ni wa Serikali. Kwa nini Serikali inataka kutugombanisha? Baadaye mtatuona sisi wakorofi, haiwezekani. Lazima mtambue shida ambazo tunazitatua kwa Majimbo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Doctor labda niseme, kama watu hawakwambii, watu wanasema labda kwa sababu Dkt. Mpango hana Jimbo. Watu wandahani hivyo. Iko shida Jimboni ambayo Mbunge anatumia pesa hizi hizi kupata nguvu ya kuendesha shughuli za Majimbo, lakini hili tuko wenyewe. Tunapunguziana nguvu za mwisho za kupambana kwenye uchaguzi. Ukikata shilingi milioni sitini au ngapi, maana yake umedhoofisha Mbunge huyu anayetaka kurudi tena kuwatumikia wananchi, hana nguvu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Uchaguzi umekuwa ghali, sasa na nyie mnataka kunyofoa shilingi milioni 60, 70, za nini? Serikali ina wasomi wengi, tafuteni mbadala. Tafuteni njia nyingine za kutoza kodi, kwani lazima mwangalie tu mafao ya Mbunge? Sasa mkikata zetu, Madiwani je? Maana mtafanya siasa iwe kazi. Kuna siku mtatutoza fedha kuingia hapa. Badala ya ku-punch finger print, tutakuwa tunalipia hapa, kwa sababu hamtaki kutafuta kodi nyingine. Jamani tafuteni kodi nyingine. Hivi imefika wakati mtukamue sisi mpaka damu? Haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili mpaka mwisho mimi sikubali. Kama ni hivi, hii kazi ya Ubunge ni kazi ya hasara. Tutashindwa kuwahudumia wananchi kwa sababu kila kukicha kale kadogo alikopewa Mbunge mnataka kukachukua.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali isikie vizuri, kelele zote hizi haziwezi kuwa kama jogoo. Kule Unyamwezini tunasema jogoo anaweza akapiga kelele usiku mmelala ili muamke; lakini yeye hawezi kujifungulia mlango. Sasa tusipige kelele kama vile jogoo. Sisi mlango tunao, wenyewe ndio tunasema hii bajeti sawa au haipo. Sasa isije kuwa mambo yamekwama mkimbilie caucus. Tumalizane tu humu jamani, mtusikilize na sisi.
Kuhusu pesa za maendeleo kwenye Halmashauri, hazipelekwi kwa wakati katika Halmashauri zetu. Hazipelekwi! Mwaka uliopita 30% tu kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kaliuwa ilipelekwa, 70% yote haikupelekwa. Unategemea nini sasa? Maana yake kazi haziendi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tusichomeke. Nami naishauri Serikali, kama ina mambo yoyote muhimu, sijui madawati, maabara, itakuja na nyingine sijui itatengeneza jina gani, yaleteni mapema kwenye bajeti, siyo kuyachomeka wakati hayana mafungu. Matokeo yake Halmashauri zinaparaganyika. Zinakusanya, haziwezi kutumia kwa sababu tayari kuna maagizo. Tafuteni pesa kokote mlipo, eeh, maabara, eeh sijui madawati. Kazi ya Serikali, leteni mpango kama sasa, badala ya kuchomeka chomeka. Kwa nini tuchomeke wakati ninyi wataalam mpo na bajeti mnatengeneza? Naiomba sana Serikali isitengeneze utaratibu wa kuchomeka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, madeni ya wazabuni. Mheshimiwa Waziri hebu tujaribu kuyaondoa madeni, ni aibu. Tunakazana, lakini huko madeni ni mengi, wazabuni walio-supply shuleni, kwenye hospitali, Halmashauri, Magereza, watu wanaidai Serikali, ni aibu! Tudaiwe basi na mashirika makubwa na nchi nyingine, lakini humu humu ndani mtu deni lake halali, anadai hata shilingi milioni mbili; hivi kuhakiki shilingi milioni mbili mnataka tena mtafute wataalam kutoka nje waje wahakiki deni? Haiko vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, CAG report kule kwenye Halmashauri Mheshimiwa Waziri tafuteni mzungumze na TAMISEMI. CAG report ni serious report, haiwezi kuwa inajadiliwa haraka haraka halafu inafunikwa tunaondoka. CAG report inaonesha kama kuna madudu, kama kuna mafanikio, lakini eti kwa kubana matumizi, tunaziambia Halmashauri zijadili siku moja au masaa, haiwezekani. Mbona wenyewe CAG report anakuwa amekagua karibu mwezi mzima amepiga kambi; lakini kujadiliwa na Madiwani, inajadiliwa kwa nusu saa au kwa masaa mawili. Mheshimiwa Waziri tengenezeni utaratibu CAG report ipate muda mzuri wa kujadiliwa kama ambavyo tunaweza kujadili hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imechangiwa kwa utaalam na Waheshimiwa Wabunge wengi, nisingependa kusubiri kengele, lakini mtusikie, kodi kwa Waheshimiwa Wabunge, achaneni na mpango huo, tafuteni mbadala. Withdraw benefit, waacheni watu wachukue mali zao kama ambavyo na sisi Wabunge tunachukua mali zetu. Kwa nini muwakabe? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.