Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hii Wizara asubuhi ya leo. Wizara ya Maliasili na Utalii ni miongoni mwa Wizara mtambuka inapokuja mahusiano yake na wakulima, inapofika mahusiano yake na wafugaji. Nchi yetu ina ukubwa wa takribani kilomita za mraba 947,300. Kati ya hizo ardhi ambayo tunaweza kutumia kwa ajili ya kufuga, kulima, kujenga na shughuli nyingine za miundombinu ya kijamii ni takribani kilomita za mraba 885,800.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilomita za mraba 61,500 ni kwa ajili ya water bodies, kwa ajili ya bahari, mito na maziwa. Kwa maneno mengine shughuli zote tunazozitumia kwa ajili ya ustawi wa maisha yetu, tunategemea kilomita za mraba 885,800 ambazo wakulima wanazihitaji hizo hizo, wafugaji wanazihitaji hizo na hifadhi wanahitaji hizo hizo. Ukifuatilia hotuba ya Mheshimiwa Waziri unakuja kugundua asilimia 33 ya hizo kilomita za mraba nilizozitaja ndiyo mbuga na hifadhi za misitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tunaendelea kuongezeka kwa idadi kila siku na ng‟ombe wanazidi kuzaliana na kuongezeka kila siku. Katika hiyo 885,800 kilomita za mraba, kuna ukame unaikuta hilo hilo eneo, kuna mafuriko, lakini kuna shughuli nyingine za volcano kwa mfano kule Oldoinyo Lengai ikipiga volcano pale huwezi kulima, huwezi kufuga. Kwa hiyo, ardhi bado inaendelea kupungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana hapa watu wamesema wafugaji wanahitaji malisho na hizi sababu nilizozitaja ndizo zinazowafanya wahamehame. Tumesahau kwamba na wakulima nao wanahamahama kutafuta chakula, kutafuta sehemu nzuri ya kulima kwa hoja hizo hizo kama za wafugaji. Tukisema leo tuangalie tu mgogoro kati ya wakulima na wafugaji kwenye sehemu ya malisho ya wanyama, tukienda kutazama mgogoro kati ya hifadhi na wakulima kwenye yale maeneo ya buffer zone kama maeneo ya Mto Kilombero, eneo lina rutuba nzuri wakulima wanakuja eneo la hifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ukienda upande wa selous kule wakulima wamekata miti wanaingia eneo la hifadhi. Ukija Kilosa, Mikumi the same, kila sehemu utakuta mkulima anaongezeka kutafuta maeneo ya kilimo kwa sababu eneo analolima kwanza rutuba nayo inapungua, ikipungua rutuba aina yetu ya kilimo kwa sababu siyo kilimo cha kisasa tunakutana na matatizo mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye upande wa mifugo, takwimu zinatuonesha tuna zaidi ya ng‟ombe milioni 25 na hawa ng‟ombe wanazaliana kila mwaka kwa zaidi ya milioni moja. Baada ya miaka 10 tutakuwa na ng‟ombe milioni 35. Nashangaa humu ndani tunasema tuna wafugaji, mniwie radhi humu ndani tuna wachungaji hatuna wafugaji. Huwezi ukajiita mfugaji unahama pori moja unakwenda pori lingine na huwezi ukajiita mkulima, hatuna wakulima, tuna wabangaizaji wanaotafua maeneo kwa ajili ya kulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri kitu kimoja, juzi nilisema hizi Wizara nne, tano zikae pamoja kwa ajili ya kupanga vizuri, tukisema leo tutenge maeneo kwa ajili ya ufugaji, ng‟ombe wanazidi kuongezeka, ardhi bado ni ndogo na aina yetu ya ufugaji tunaona kabisa hatuwezi kuja ku-solve hili tatizo. Baada ya miaka10 tuna ng‟ombe milioni 35 tutawatengea maeneo gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewaondoa kule Ihefu tumewapeleka Lindi, yale maeneo Lindi yaliyopangwa kwa ajili ya wafugaji leo watu wanalima ufuta. Kwa tatizo lile lile wakulima wana matatizo, wafugaji wana matatizo. Sasa hili haliwezi likajibiwa kwa Waziri kuja kutuambia hili tatizo atalimaliza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tujadiliane hivi, lakini baada ya bajeti mimi niiombe Serikali, ikae Wizara ya Ardhi, Wizara ya Kilimo, Maliasili na Utalii na Wizara ya Mazingira. Lazima haya tuangalie, tunakwenda tunamsahau wa mazingira huyo, ukame ukija, tunamsahau wa mazingira huyu, mafuriko yakija na haya maeneo yanayotengwa yanatengwa kwa hoja za ikolojia. Tukisema tulime kote, tufuge kote, mwisho wa siku mvua tutakosa, nchi nzima itakuwa jangwa. Kwa hiyo, hoja siyo hoja ya hisia, siyo hoja ya kusema mimi ni mkulima nataka wakulima wangu wakae vizuri, mimi ni mfugaji nataka ng‟ombe wangu akue.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku tutalima wote, tutafuga wote, tutashindwa sehemu ya kufuga, ardhi itageuka jangwa na hata tunaohama hama wakulima kutafuta maeneo mazuri ya hifadhi yenye udongo wa rutuba kwa ajili ya kupata mahindi mazuri, kwa ajili ya kupata maharage mazuri, ufuta, itafika muda haya maeneo mvua haitafika, na hiyo mito tunayotegemea kumwagilia nayo mvua haitakuwepo, maji hayatakuwepo, samaki hawatakuwepo. Kwa hiyo, sekta moja ikikorofisha itapelekea sekta nyingine kuharibikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kwa nia njema kabisa, tutajadili kila kona kuhusu Maliasili na Utalii kwenye eneo la migogoro ya wafugaji, kwenye maeneo ya matumizi bora ya ardhi, lakini hatutafika mwishoni kama hakutakuwa na mpango mkakati wenye sura mbili. Kwanza mpango wa dharura, uitwe transformation strategy, kuwatoa wakulima wanaohama hama wawe centralized katika kilimo cha kisasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuwaondoa wachungaji wanaohama kuchunga chunga wawe centralized, wafuge ng‟ombe wao vizuri wazaliane na wawe na tija. tukienda hapo tutafika mbele kwa haraka na ardhi yetu tutaitunza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna kosa moja tunalifanya, tunapoongelea vyanzo vya mapato na nguvu kazi ya Taifa letu tunatazama wakulima, tunatazama wafanyakazi tunasahau kuwatazama wafugaji kama sekta rasmi ambayo ipangiwe mipango kama tunavyopanga mipango kwenye maeneo ya kilimo. Tunamwangalia mkulima, yaani mfugaji anakwenda kwenda tu, ndiyo kwa maana leo yuko Lindi, keshokutwa anatoka, hatuwezi kwenda kwa staili hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali, wafugaji sasa kwa sababu sio wafugaji, tuwa-transform kwenda kuwa wafugaji, wawekwe kwenye utaratibu mzuri, tija tutaipata. Hatuwezi leo kusema tuna ng‟ombe milioni 25, halafu pato hatulioni. Baada ya miaka 10 tutakuwa milioni 35 halafu wao wanazunguka tu nchini, haiwezekani hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kwa nia njema kabisa hizi Wizara nne zikae pamoja, zije na mkakati mkubwa, hii migogoro haitakuwepo na wala tusitoe hapa maneno ya kuwafurahisha wakulima, kuwafurahisha wafanyakazi ili migogoro itulie, haitatulia. Ardhi ni ndogo sana, msijidanganye mnatoka hapa mpaka Dumila mnaona yale si mapori, yale ndiyo kwa ajili ya kuleta vertilization ni AC ile ya kuleta hali ya hewa nzuri. Sasa siku mki-clear ile miti, cha moto mtakiona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.