Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsate kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo hotuba ya Waziri wa Fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa siku hii ya leo. Lakini kubwa nimpongeze Waziri wa Fedha na timu zake zote kwa kazi nzuri waliyoifanya. Kwa kweli hotuba nzuri na mwelekeo wa bajeti hii ni mzuri, angalau unaweza ukapunguza makali ya umaskini wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Hotuba ya Waziri wa Fedha nimeona kuna asilimia tano ya mapato ya Halmashauri zetu nchini ambao huwa wanatenga asilimia 10 vijana asilimia tano na wanawake asilimia tano.
Mheshimiwa Waziri wa Fedha, mimi nikuombe, chonde chonde asilimia hii tano ni ya miaka dahari na dahari iko pale pale tunaondoaje umaskini na tunapunguzaje umaskini? Lakini kama tuna nia ya dhati ya kupunguza umaskini; katika hotuba yako umesema ongezeko la makusanyo ya mapato yetu limeongezeka kwa kutokana na haya yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza mianya ya rushwa imezuiliwa, wafanyakazi hewa mshahara wake upo umeingia kwenye mapato, wakwepaji kodi ambao walikuwa wanakwepa mpaka kuingiza makontena hela yake ipo, mapato ya gesi na cement viwanda vyake vipo. Mimi nikuombe Mheshimiwa kwa heshima na taadhima kubwa hebu muangalie sekta hii ya waakina mama na vijana ajira haipo, lakini tunapobana tu asilimia tano umekuwa wimbo wa Taifa na Halmashauri hizo asilimia kubwa hawakidhi viwango vya kupeleke hii asilimia 10. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri, yeye kwa huruma yake atusaidie kwa hilo ili angalau sasa aongeze kwa njia moja au nyingine anavyoona yeye inafaa kwa mapato haya mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie shilingi milioni 50. Kuna Mbunge mwenzangu hapa amezungumzia; kwa sababu tukiipeleka kwenye SACCOS moja kwa moja yatarudi yale ya Mfuko wa Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete, kwa sababu wajanja wote ndio wenye SACCOS, vijijini kule hawana SACCOS, sasa inakuwa ni masharti makubwa kiasi ambacho watanuafaika watu wachache. Mimi nadhani Serikali ina wataalamu wazuri wa maendeleo ifanye utaratibu isifanye haraka ya kusambaza hela kupitia SACCOS. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Wenyeviti wa Mitaa, tuna Makatibu tarafa Wakuu wa Wilaya ndio wanaohodhi eneo la kijiji chote. Mimi ningeomba kabla hamjafanya maamuzi ya kupeleka kwenye SACCOS mimi naomba pesa hizi ziende kwa utaratibu wa vijiji, pia kila Jimbo wapewe maana ndiyo tupo shuleni sasa, ya kwanza ilipita free, sasa hii maadamu tunaipigia sasa; na kwa kuwa Rais hakutoa ahadi mijini, amepita kwenye kampeni yake vijijini kote pamoja na Mheshimiwa Makamu wa Rais; isiwe kwa kuwa wale wa mjini kwa sababu ndio wenye SACCOS nyingi wapate, vijijini ambapo hakuna wakose. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba hilo liangaliwe sana kwa sababu tuna mengi ya kuongea, lakini niombe hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine afya. Mheshimiwa Waziri wa Fedha mimi niombe katika fedha za mwaka huu Wizara ya Afya tuna miradi mingi ambayo haijakamilika, tuna zahanati nyingi zimejengwa na zina hospitali ambazo zimejengwa hazina theatre, kuna wafadhili wamekuja wameweka vifaa vyao hivi mnawaambiaje? kwa sababu kila mwaka watafuatilia pesa zao ziko pale lakini mnasema daktari wa usingizi hayupo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kama Zahanati ya Bukene Mawaziri wote wamepita pale wameiona waakina mama wanakufa, hivi unapunguzaje vifo wakati ipo tayari vifaa vya kisasa ambavyo hata Muhimbili hawana, Bungando hawana vipo pale kwa ajili ya kuokoa maisha ya mama na mtoto. Kwa hiyo, mimi niombe kipaumbele Wizara ya Afya iangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nimeangalia kitabu hiki katika kupunguza kodi, kuondoa misamaha bado hujatoa misamaha kwa nguo za akina mama, kwa lugha nyingine mataulo yao bado sijaiona. Kuna wanafunzi wanashindwa hata kununua pedi, leo hakuna uondoaji wa kodi. Mimi ningeomba Serikali hata hii inapata kigugumizi gani kutoa iondoe kodi ili angalau viweze kuingia kwa urahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nizungumzia tozo nyingi za tumbaku. Hivi unaweka tozo nyingi za tumbaku halafu unasema unamsaidia mkulima? Mheshimiwa Waziri wa Kilimo liangalieni hili mnapokaa kwenye Baraza la Mawaziri, tozo ni nyingi hazifai, wakulima wanazidi kuwa maskini, kilimo chenyewe cha mkono lakini hawapati msaada wowote kutoka Serikalini. Mimi naomba Serikali iangalie sana suala zima la tumbaku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia pamoja na hayo sekta hii imetengwa haisaidiwi na Serikali, hawa wanunuaji wa tumbaku wanajipangia wenyewe bei, wanaamua juu ya soko wanavyotaka wenyewe. Waziri wa Fedha utapataje ongezeko la pesa ikiwa wakulima wa tumbaku wananyanyaswa ambao asilimia 60 ya tumbaku wanayolima inasaidia mapato ya Serikali? Kwa hiyo, hilo nalo ningeomba Serikali muangalie tuna hali ngumu sana huku wakulima wa chini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee habari ya maji. Ukigusa umegusa wanawake, akina baba wote humu mnafuliwa nguo na akina mama, mnapikiwa na akina mama, lakini wao ndiyo wanahangaika na maji. Leo hakuna bajeti inayoeleweka ikaambiwa kwamba hii ni bajeti ya maji. Mheshimiwa Waziri, mimi nimesikia sana hotuba zako, umesifia wanawake, umewaonea huruma wanawake, sasa huu Mfuko wa Maji Vijijini toka kwenye 50, weka kwenye 100 hili suala usisumbuke...
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.