Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye mawasilisho ya bajeti iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze kwa kuipongeza sana Kamati ya Bajeti, imefanya kazi kubwa, na naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tusome sana hotuba ya Kamati ya Bajeti, wamekuwa wazalendo kweli kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niungane nao kuzungumzia masikitiko yangu kwamba kama kweli Bunge hili linataka kutumika kama rubber stamp Wabunge tukatae kwa nguvu zetu zote. Tulifanya kazi kubwa ya kuja na Budget Act, tukasema ni sheria inayokuja kututoa kwenye kufanya mambo kama business as usual. Ninyi leo mnataka kuturudisha kule?
Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Kamati inalalamika kwamba haikuzingatia maoni ya Kamati, Wabunge tusikubali asilani. Serikali hii ni sikivu, sikieni haya yanayosemwa na Kamati ya Bajeti, sikieni haya yanayosemwa na Wabunge. Nchi hii yetu sote, tukifika mahali kikundi fulani kikajiona chenyewe kinajua zaidi ya Wabunge tuna tatizo kama nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma mpango, Ripoti ya Hali ya Uchumi inatuambia sekta ya ujenzi imeongoza kwa kuchangia kwa asilimia 16.8, sekta ya habari na mawasiliano asilimia 12, sekta ya fedha na bima asilimia 11, sekta ya madini asilimia 9.1; lakini sekta zote hizi zinashughulisha watu wachache. Sekta inayoajiri asilimia 70 ukuaji umeshuka. Sekta ya kilimo ukuaji umeshuka kutoka asilimia 3.4 sasa ni asilimia 2.3 and yet we are happy, hii haikubaliki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nataka nijielekeze kwenye eneo moja, sekta ya uvuvi hivi tunataka tuambiweje ili tuelewe?
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma ripoti ya mwaka 2014 ya state of the fisheries ya Shirika la Chakula Duniani inasema kwamba uzalishaji wa samaki kupitia ufugaji (aquaculture) ulikuwa ni tani milioni 100 ulimwenguni; pasipo kuzungumzia uvuvi bali ufugaji wa samaki; zenye thamani ya bilioni 144.4. Hivi watanzania hatutaki kushiriki kwenye uchumi mkubwa kiasi hiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika uzalishaji huo Asia imezalisha asilimia 88 ya hizi, Amerika asilimia 4.7, Europe asilimia 4.3, Afrika asilimia 2.2, kwa maana kwamba imezalisha tani milioni 1.4. Lakini angalia kichekesho chake katika tani milioni 1.4. Lakini angalia kichekesho chake, katika tani milioni 1.4 Misri peke yake imezalisha tani milioni 1, nchi nyingine za Afrika ndio tunanyanganyia 0.4. Lakini Misri hii ufugaji huu wa samaki inategemea maji kutoka Mto Nile, Tanzania ikiwa sehemu ya uchangiaji wa maji ya Mto Nile. Sisi tuna ziwa Victoria, Tanganyika, tuna bahari, tuna Ziwa Nyasa tumelala usingizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, uchumi mkubwa kama China wanaona umuhimu wa kushiriki kwenye uchumi huu, wanazalisha nusu ya samaki wanaofugwa ulimwenguni. Sisi Watanzania tunaona sekta hii ya kipuuzi, tubadilike. Ni kwa kupuuza vitu kama hivi ndiyo maana leo hii mchango wa sekta ya uvuvi umeshuka, na umekuwa ukishuka tangu mwaka 2007. Mchango wa sekta hii ilikuwa asilimia 1.7, tumeporomoka mpaka asilimia 1.2 mwaka jana, lazima tubadilike. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Kamati kwa kuzungumzia suala la mfuko wa maji, safari hii msitufanyie kiini macho. Mwaka wa jana tulisema fedha zile ziende vijijini mkazipeleka mijini safari hii pelekeni fedha zile vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Bajeti imesema tuweke tozo kwenye mafuta mbona Wakenya wameweka bajeti yao ya juzi? Tuweke tozo kwenye mafuta, twende tukajenge zahanati. Hii ni aibu kwamba tangu mwaka 2000 tunaweka kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kwamba tutapeleka zahanati kwenye kila kijiji tumekwenda kwa asilimia 20 tu. Tutenge bajeti twende tukajenge zahanati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuongeze fedha za maji, wananchi wetu wanataabika vijijini. Pale Mkinga kuna one stop border post, tumeambiwa kimekamilika; kituo kile hakina maji. Mheshimiwa Mpango watu wako watakuwa kwenye ofisi ile haina maji; yatakuwa yanachukuliwa kutoka Kenya. Tuna mradi wa bilioni sita tupeni fedha tukafanye mambo pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja ahsante.