Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba ya Bajeti iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naipongeza Serikali yote kwa jinsi ambavyo imeleta mpango na bajeti ya kuthubutu, tusiogope kuthubutu, changamoto zitakazojitokeza huko mbele ya safari tutazitatua, lakini naipongeza sana Serikali pamoja na Waziri kwa uwasilisho mzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishukuru sana Serikali kwa kuamua kujenga reli kwa standard gauge, kwetu sisi tunaotoka Tabora, Kigoma na Mwanza ni ukombozi mkubwa. Natunaomba mpango uanze mara moja mwaka huu wa fedha ili tusaidie kupunguza bei kutokana na usafiri wa reli utakaopunguza bei ya bidhaa zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napongeza Serikali kwa kuja na mpango wa maji, ombi langu mimi ni kwamba ili akina mama watokane na ubebaji wa maji kwenye vichwa, badala ya shilingi 50 kama walivyopendekeza Kamati ya Bajeti tuongeze zifike shilingi 100 ili akina mama vijijini wapate maji wajikomboe na wafanye kazi zingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika mimi ningeanza na upandewa mtu ni afya. Bila afya hakuna chochote kinachowezekana. Ningejikita zaidi kwa upande wa mama na mtoto. Ndugu zangu tuwapongeze wakinamama na nafasi ingeniruhusu ningewaomba akina mama na akina baba wote tusimame tuwape heshima akina mama wanaofariki kwa njia ya uzazi, wanafanya kazi kubwa na wanafariki katika kutimiza wajibu wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona zimetengwa asilimia tisa ya bajeti nzima kwa ajili ya afya. Naiomba Serikali ifikishe asilimia 15 kama walivyokubaliana katika Azimio la Abuja. Lakini pia mimi ningependa katika kujumuisha tupate majibu mpango wa MMAM uliishia wapi? Kwa sababu mpango wa MMAM ulikuwa na lengo la kuongeza zahanati ili wakinamama wafike haraka kwenye zahanati ili wasipoteze maisha yao. Tunataka tathmini ya mpango wa MMAM. Zahanati nyingi hazijajengwa, lakini pia zina upungufu mkubwa wa watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwapeni mfano wa Urambo tuna zahanati 20 ni zahanati tano tu zenye Maafisa Tatibu. Ni haki mama mjamzito mwenye complication kweli akapewe prescription ya dawa na muuguzi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali katika mwaka huu wa fedha iangalie; na ndiyo maana nasema iongezewe bajeti ili kuwe na wafanyakazi wengi wa kutosha wa hospitali na zahanati. Urambo ina uhaba wa wafanyakazi 150, na nimeshatoa mfano kwamba zahanati tano tu ndizo zina Maafisa Tabibu ambao siyo haki hata kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kulikuwa na mradi huu wa ADB. Mimi naiomba Serikali iangalie jinsi gani ya kukamilisha zile theaters zilizokuwepo, najua hii bajeti katikati huko italeta tu mabadiliko ya kuomba nyongeza ya fedha, kwa sababu Serikali hii inathubutu. Tuna theater Urambo na sisi tulikuwa tunafikiri kwamba njia mojawapo ya kupunguza vifo vya kina mama na watoto ni kuwa na theater katika vituo vya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha ajabu ni kwamba Urambo nzima yenye kata 18 tuna kituo cha afya kimoja tu halafu hakina theater ni haki hii? Halafu theater iliyokuwa inajengwa imeishia kwenye linter kwa mpango wa ADB.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Urambo jamani tunahudumia mpaka Uvinza na ile miji ya karibu ya Mkoa wa Kigoma kutokana na umbali, lakini cha ajabu theater iliyokuwa inajengwa Urambo imeishia kwenye linter. Ndugu zangu nipeni pole mimi Mbunge wa huko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa kuthamini afya ya mama na mtoto mpango wa ADB ulikuwa unajenga clinic ya mama na mtoto, jamani imeachwa imechimbwa msingi mpaka leo. Lakini pia kulikuwa na kliniki ya mama na mtoto katika sehemu ya Isongwa imeachwa katika hatua ya msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, na ninasikitika, nina barua hapa kutoka Wizarani inayotutaka sisi wenyewe tumalize, Halmashauri inaweza kupata shilingi milioni 500 za kumaliza theatres? Na hayo ni majengo tu hayahusiani na vifaa. Nina barua hapa ya kusikitisha sana ya kutuambia sisi kama Halmashauri tumalize miradi ya ADB, kwa nini walileta mradi ya ADB kama walikuwa wanajua sisi tuna uwezo? Mimi ningeomba suala hili la theatres zilizoachwa bila kumalizwa zote pamoja na majengo ya kliniki yamaliziwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia sisi Kanda ya Magharibi hatuna Hospitali ya Rufaa, je, Serikali inafikiriaje kuhusu Kanda ya Magharibi nayo kupata Hospitali ya Rufaa?
Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye kilimo. Mimi naipongeza hii Serikali kwa kushughulikia sana suala la viwanda ili kuinua hali ya wananchi. Tunaomba badala ya tumbaku kutoka Tabora kupelekwa Morogoro tuwe na kiwanda, na sisi tuna hitaji viwanda kwa sababu vitatupa pia ajira kwa watu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ukurasa wa 45 nimesoma, Serikali imeandika hapa kwamba inafahamu vizuri sana changamoto za wakulima. Nimeona hapa nikafarijika nikasema ahaa kumbe Serikali inajua. Ukurasa wa 35 inasema kwamba hata hivyo bado sekta hii ya kilimo inakabiliwa na changamoto kadhaa zikiwemo za kodi na tozo za mazao zisizo na tija. Tumbaku ina kodi zaidi ya 12, halafu wanasema tena uhaba wa pembejeo ambazo pia zina kodi nyingi, vifaa duni, masoko na uhaba wa Maafisa Ugani, kumbe Serikali inajua? Je, Serikali inachukua hatua gani katika kutimiza haya kutatua changamoto hizo? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la zao la tumbaku, tumbaku ni jani, mwezi wa pili tu jani linaiva, jani likishaiva masoko yanatakiwa yaanze mara moja mwezi wa tatu, lakini utaona cha ajabu masoko yanasuasua hadi leo hii. Bodi ya Tumbaku haina fedha nimeongea nao hawana fedha, wakulima watafanyaje?
Mheshimiwa Naibu Spika, tumbaku ndugu zangu inavyokaa inapoteza ubora na inapoteza uzito. Inapofika Morogoro imepoteza uzito, je, ni haki hii?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nawashukuru, Naibu Waziri wa Kilimo amesema na mimi naomba nirudie sijui kama itakuwa ni vibaya, kwamba anakuja Tabora, pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu waone shida zinazowakabili wakulima wa tumbaku waongee nao, vyama vya msingi vinakufa watafanyaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, makato kwenye pembejeo ni mengi, makato kwenye zao lenyewe mengi, kuna uhaba wa wanunuzi. Naomba mtuambie; kwa kuwa mnatambua; kwenye ukurasa wa 35; Serikali inachukua hatua gani ya kupata masoko zaidi ili kuwe na ushindani wa masoko? Haya makampuni matatu hayatoshi, yana ukiritimba, tunataka masoko mengine kutoka nje, nchi za Japan pamoja na China, Serikali inasema nini kuhusu hili?
Lakini pia wenzetu, kwa mfano wa Uganda wajanja wale wame-market kahawa yao wameiuza ndiyo maana unaona watu wa Kagera wanapeleka kahawa kuuzia Uganda. Kwa nini na sisi tusishirikishe Wizara ya Mambo ya Nje ili tumbaku yetu iuzwe? Kwa sababu ladha na harufu iliyo kwenye tumbaku tunayolima sisi watu wa Tabora ndiyo inayofunika duniani kote waulizeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa nini na sisi tusiitangaze kwa kutumia pia Wizara ya Mambo ya Nje, Mabalozi, nchi majirani ili tumbaku yetu na sisi ivutie tupate wanunuzi wengi zaidi. Mimi ninachoshukuru ni kwamba Mheshimiwa atakuja ajionee mwenyewe. Lakini naomba sana Bodi ya Tumbaku iwezeshwe ili iweze kufanya kazi, na pia nimesema kiwanda cha tumbaku kijengwe Mjini Tabora.
Mheshimiwa Naibu Spika, itakuwa kwa kweli siyo haki kama nikimaliza bila kusemea mtoto wa kike. Nimeona mipango mingi ya Wizara ya Elimu, mimi naomba kujua elimu bure inayotolewa itamsaidiaje mtoto wa kike hapa katikati pasiwe na tatizo lolote la kumfanya atoke nje ya darasa ili amalize kuanzia kidato cha kwanza hadi mwisho? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba Wizara itakapokuja kumalizia ituambie kutokana na wingi wa taasisi za elimu zilizo nchini ni lini Mamlaka ya Ukaguzi itaundwa ili ukaguzi kweli ufanyike kikamilifu?
Mheshimiwa Naibu Spika, ni mengi ambayo ningeongea lakini bado nawakumbuka walimu wangu, tunaomba chombo kile kinachoundwa kwa ajili ya walimu kifanye kazi ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hiyo.