Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhuhanah Wataala kwa kunipa afya njema nikawa miongoni mwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nitakuwa mchoyo wa fadhila na shukrani zangu za dhati kabisa kama nitashindwa kuwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Tandahimba ambao wamenichagua kwa asilimia 57 nikawa Mbunge wa kwanza Tanzania kutangazwa, nawashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye Mapendekezo ya Mpango, ukienda ukurasa ule wa kumi yamezunguzwa sana mambo ya maji. Jambo la ajabu kwangu mie Tandahimba kunakozungumzwa maji ambapo kuna vyanzo vya maji vya kutosha, Serikali kama ingekuwa makini tusingeendelea kuimba wimbo wa maji leo hapa. Maana kwenye Jimbo langu sisi tupo mpakani mwa Msumbiji na Tanzania na tuna mpaka wa Tanzania na Msumbiji ni Mto Ruvuma. Jambo ambalo kama Serikali ingekuwa makini tusingekaa hapa watu wa Mtwara tukazungumza habari ya maji. Niiombe Serikali kupitia suala hili la bajeti, waone kabisa kuna kila sababu ya kuona Mkoa wa Mtwara hatuwezi kurudi tena tukazungumza suala la maji na maji yamejaa kule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndugu zangu wamezungumza suala la kuboresha kilimo. Tunapozungumza kuboresha suala la kilimo tunazungumza na suala la barabara pia. Tumezungumza 2014 ukitoa dhahabu ni korosho ambayo imeingiza Taifa bilioni 647.9. Ukitoka Mtwara kwenda Tandaimba, Newala, Nanyamba ambapo ndiyo wazalishaji wakubwa wa korosho hizi hawana lami kwa miaka 54 ya CCM bado mnasema mna mipango mizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Wizara ya Fedha niombe Mawaziri wenye dhamana wawafikirie wakulima hawa wa korosho ambao wanaleta pato kubwa la Taifa lakini bado ukasafiri kwa masaa sita, saba kwenda sehemu yenye umbali wa kilometa 95 kama Jimboni kwangu Tandahimba kutoka Mtwara Mjini kwenda Tandahimba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu waliotangulia wamezungumza sana suala la bandari. Nimeona mipango ya kuandaa bandari mpya ya Mbegani sijui wapi huko, nyingine ya Tanga, lakini bandari yenye kina kirefu Tanzania na Afrika Mashariki ni bandari ya Mtwara. Umezungumzwa mpango wa kujenga magati manne, lakini kwenye ule mpango limezungumzwa gati moja tu lenye urefu wa mita 300, lakini halijaelezwa lini lile gati litajegwa. Niiombe Serikali watakapokuja na mpango sasa wawaambie wana Mtwara gati hilo la mita 300 litajengwa lini na litakwisha lini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema Mtwara tuna fursa kubwa kama Serikali itakuwa inaona umuhimu huu. Leo unakwenda Uchina unakwenda nchi za Ulaya ukitafuta bandari, bandari ya Mtwara yenye kina kirefu haipo kwenye ramani. Sasa Serikali hii ya CCM bado mnajivuna, mnazungumza suala la viwanda na gesi tunayo Mtwara mtajengaje viwanda vya korosho Tandahimba ambapo umeme wenyewe haupo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo REA phase II iliyozungumziwa mpaka leo ukija sehemu zenye uzalishaji umeme bado haupo. Napata shida sana, tunapozungumza suala la viwanda wakati sehemu yenye umeme bado wananchi wake hawana umeme, lakini mnazungumza kupeleka viwanda, unapelekaje viwanda sehemu ambayo haina umeme? Sasa niombe muwe makini sana mnapoleta mipango hii, na mara zote CCM mmekuwa wazuri sana wa ku-plan, ni wazuri sana wa ku-plan, implementation ndiyo shida. Sasa ninaiomba Serikali ya CCM kama ina nia njema, yale mliyoyaweka kwenye mpango myatekeleze. Vinginevyo sisi tuna take off 2020, tunachukua nchi hii kabisa. Haya wala siyo masihara mimi kwangu kule nimeshawapiga, Madiwani nimeshachukua kila kitu nimezoa zoa pale. Tunajiandaa kuisafisha CCM 2020, Mtwara kama hamkuleta mambo mazuri kule, kabisa! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuzungumza suala la umeme, ambalo nimekuja kuzungumza hapa, tulipata shida, sisi ndiyo tulipigana, tulipigwa tukakaa jela wakati tunaitetea gesi, lakini watu wa Mtwara hawakuwa na shida ya Serikali kutoa gesi Mtwara kwenda Dar es Salaam, watu wa Mtwara walikuwa wanatetea maslahi ya watu wa Mtwara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama leo bomba limekwenda Dar es Saalam kilometa 542 ,lakini Mkoa wa Mtwara kuna watu hawana umeme. Wakilalamika mnataka wasilalamike, wakilalamika mnawapiga, sasa Serikali imekuwa ni ya kupiga piga tu hovyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmezungumza suala la elimu hapa, wakati mnazungumza suala la elimu tumepongeza Mpango wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Magufuli, suala la elimu bure, lakini vitu vya ajabu, kama Rais amesema elimu bure iweje leo mtoto anakwenda hospitali kupima anaambiwa atoe pesa na ndiyo kauli ya Rais. Kama Rais amesema bure vyombo vyake vingine kama ni suala la kupima mwanafunzi aende apimwe bure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, joining instruction nayo ni shida wakienda Mahakamani wanatakiwa watoe pesa sasa hata kwa vitu vidogo hivi! Hata kwa vitu vidogo hivi! Hebu msaidieni Rais Magufuli huyu aonekane alichokisema kina maana ya bure kweli. Tusikae hapa kuzungumza bure watoto wanaenda hospitali tu wanaambia elfu tano ya vipimo, mwanafunzi anakwenda Mahakamani anaambiwa shilingi elfu tano ili aandikiwe sijui kitu gani sijui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe Serikali hii kama ina dhamira njema kama ilivyozungumza tuone haya mambo mnaweza kuyarekebisha, lakini mlizungumza vitu vizito, wenzangu wakazungumza suala la airport ya Mtwara. Ukisoma hotuba ya Rais kuna maeneo yanaonekana airport ya Mtwara, uwanja umekarabatiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Waziri mwenye dhamana kama utapata fursa njoo Mtwara, ile airport tunayozungumza kwamba imekarabatiwa ndege ikitua ni balaa. Utafikiri unatua kwenye maporomoko, sijaona uwanja wa ndege wa namna hiyo wa ovyo. Mataa hakuna sasa akina Dangote watakuja asubuhi tukiwa na mambo ya dharura ya usiku inakuwaje! Ndiyo maana hata Mawaziri hamji Mtwara usiku kwa sababu hakuna facility airport pale, taa hakuna mmezibeba taa zile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nione kama mna dhamira njema ya kuleta viwanda mnavyosema, kuboresha miundombinu mnayosema. Hebu wafakirieni watu wa Mtwara kwa namna nyingine sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu limezungumzwa suala la elimu kwa maana ya VETA nataka niizungumzie VETA kidogo, kwa maana ya viwanda mnavyosema, viwanda na Vyuo Vikuu. Kwangu pale kuna kata moja ya Mahuta, kuna majengo pale yaliyoachwa na Umoja wa Wazazi Tanzania. Kuna majengo yanayotosha Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi kama una shida ya majengo ya VETA njoo tukukabidhi Mahuta pale ili watu wa Tandahimba wapate fursa ya kuwa na VETA ili iwasaidie watu wa Newala, Masasi, Nanyamba watapata fursa kwa sababu majengo tayari tunayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, mchango wangu ulikuwa huu. Ahsante sana. (Makofi)