Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyenzi Mungu, kwa kunijaalia uzima na afya njema na leo naomba kuchangia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa maandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi ya Mtwara Mjini hayapapimwa. Katika kikao cha kwanza Bunge lako hili la Kumi na Moja nimeuliza maswali juu ya upimaji na urasimishaji wa ardhi Mtwara Mjini ambalo mpaka sasa halijajibiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri atakapokuja kujumuisha hoja yake aje na majibu stahiki, ni lini maeneo mengi ya Mtwara Mjini yatapimwa na kurasimishwa? Swali hili ni muhimu sana kwa kuwa mtu akimiliki kipande chake cha ardhi kisheria anaweza kukopa benki kwa kutumia dhamana ile na kuweza kumsaidia kujikwamua kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara Mjini kuna migogoro ya ardhi mingi sana. Nashangaa Mheshimiwa Waziri ameweka/ametaja mgogoro mmoja tu ambao ni wa Libya. Siyo kweli kwamba Mtwara Mjini kuna mgogoro huu tu. Ipo mingi sana ambayo Serikali inakwepa kwa makusudi kabisa kupitia Maafisa wake wa Ardhi Mtwara Mjini wakiongozwa na Afisa Mipango Miji. Kuna eneo la Mji Mwema na Tangla, maeneo ambayo yalikuwa ya wananchi Serikali, imechukua tangu mwaka 2013 mpaka leo Serikali haijalipa fidia kwa wananchi wale. Wananchi hawana sehemu ya kulima na wengine wamebomolewa makazi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tathmini iliyofanyika kila squire meter moja walilipia shilingi 250 tu. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri kwa nini Serikali hii inawadhulumu na kuwanyanyasa wananchi wa Mtwara?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua kwa kuwa ni miaka mitatu sasa tangu wananchi wamenyang‟anywa maeneo yao na hawajapewa fidia, je, Serikali ipo tayari kulipa fidia ya miaka mitatu ili ilingane na thamani ya ardhi ya sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wameibiwa katika tathmini iliyofanywa na watendaji wa Halmashauri na kupewa shilingi 250 - 450 kwa square meter moja, Serikali ipo tayari hivi sasa kufuta bei hii na kufanya tathmini upya kwa maeneo hayo ya Mji Mwema na Libya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mgogoro huu ni mkubwa sana Mtwara Mjini na wananchi wamemwelezea mpaka Waziri Mkuu na kuahidi kuutatua, Mheshimiwa Waziri Lukuvi lini atakuja Mtwara Mjini ajionee mwenyewe kuliko kutegemea taarifa za uongo za Maafisa Ardhi ambao ndio wahusika wakuu wa utapeli huu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Plot Na. 99 ya Mzee Mayunga ekari 15 ambazo amenunua tangu miaka ya 1980 na amekuwa akilipia kila mwaka, leo Maafisa Ardhi wameshirikiana kuficha file la huyu mzee na wamemwambia kiwanja hicho hakitambuliki ili wauze eneo hilo kwa mtu mwingine. Plot hii Na. 99 anayonyang‟anywa ili wauze na wamethubutu mpaka kuficha file la mzee huyu ambalo lilikuwa Halmashauri, hii ni dhuluma ya hali ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri Lukuvi ahakikishe anamrudishia mzee huyu plot yake Na. 99 ambayo wameitisha watendaji wa Halmashauri na Mkoa wa Mtwara. Watendaji wa Ardhi Mtwara Mjini ni majipu makubwa yaliyoiva, tafadhali uje Mtwara kuyatumbua au mnasubiri mpaka watu waandamane na Mheshimiwa Rais aje kutumbua?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna msemo unaosemwa sana Mtwara kuwa kutokana na sakata la gesi Mtwara, viongozi wengi wamenunua viwanja kupitia hawa Maafisa wa Ardhi. Naomba sana msipokuja kuwatumbua watu hawa, usemi huu tutauamini sana kwamba mnawalinda kwa kuwa mnawatumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba zinazoitwa za bei nafuu siyo kweli kwani bei yake ni ya juu sana. Mwalimu mwenye mshahara wa shilingi 100,000 kwa mwezi kama basic salary hawezi kununua nyumba hizi kwa shilingi milioni 40, shilingi milioni 50 na kuendelea, mnasema ni za bei nafuu? Hapana, hizi ni nyumba za wale wale wenye fedha nyingi ambazo sitaki kutumia jina maarufu sana lililopita mtaani kuwa ni nyumba za mafisadi. NHC iwezeshwe kujenga nyumba za bei nafuu.