Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nitoe mchango wangu katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa letu. Nichukue nafasi hii kuwashukuru Wananchi wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki kwa dhamana kubwa waliyonipa kuwawakilisha ndani ya Jimbo hili. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia afya na uhai wa kufika siku hii ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nijielekeze katika suala la miradi mikubwa ile, hasa suala lile la miradi mkubwa wa Village City ambao uko Mkulazi unapatikana katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki ndani ya Morogoro Vijijini katika Jimbo ninalotoka mimi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema nijielekeze hapa kwa sababu huu siyo mradi wa kwanza kupewa ndani ya Jimbo hili lakini utekelezaji wake unachukua muda mrefu. Kwa mfano, tuna mradi wa bwawa la Kidunda mpaka sasa hivi unaenda una suasua. Hata hivyo, tunaishukuru sana Serikali kwa kutupa mradi huu, lakini naomba nisisitize katika utekelezaji ufanyike haraka iwezekanavyo; hasa katika kuandaa miundombinu rafiki kwa ajili ya uwekezaji. Kwa mfano, sasa hivi Mkulazi vijiji vyake vyote vinne ambavyo ni Usungura, Chanyumbu, Mkulazi yenyewe na Kidunda vyote havina mawasiliano, vyote barabara haipitiki mwaka mzima, lakini pia hata maji yenyewe ndiyo hayo ya kubahatisha pia havina umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeiomba Serikali ingekuja na mpango kabla ya kuwekeza huo mradi mkubwa kuandaa hayo mazingira ili kuwavutia wawekezaji, hata wale watu wenye nia ya kuja kuwekeza ndani ya Morogoro vijijini, ndani ya Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki wawe na moyo kwamba mazingira yanaruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusu suala la viwanda, Morogoro ambayo ndiyo Mji wa mwanzo kabisa baada ya uhuru Serikali iliamua kabisa kuitenga mahsusi kwa ajili ya viwanda. Tunashukuru kwa hilo na kulikuwa na viwanda vingi tu ambavyo viikuwa vinasaidia ajira ndani ya Morogoro vijijini, Morogoro Mjini na Taifa kwa ujumla, lakini viwanda vile vingi havifanyi kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kabla ya kuja na Mpango wa Pili wa viwanda wangekaa na hawa ambao waliobinafsishiwa ili kujua changamoto gani ambazo zimewakabili mpaka sasa haviwezi kuzalisha vile viwanda na kutoa ajira kwa Watanzania. Tulikuwa na viwanda vya Moro Shoes, Viwanda vya Ngozi, Viwanda vya Mafuta, Viwanda vya Nguo vyote hivyo vimekufa vimebaki vya Tumbaku na vile vya Sukari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwauliza wale wa wawekezaji wanatuambia jambo moja tu, wanasema kwamba viwanda tukizalisha hapa havilipi, kwa hiyo, ndiyo maana rai yangu Serikali ni vizuri mkakaa na hawa mliowabinafsishia mkajua changamoto zao, hata kama mnataka tuvichukue tena lakini itatusaidia kubaini changamoto mapema ambazo zitatusaidia katika Mipango mipya kwa hapo kuanza kwenda mbele zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie kuhusu viwanda hivyo hivyo, suala la Viwanda vya Tumbaku kuwa Morogoro. Morogoro kwanza watu tusisahahu kwamba na sisi ni wazalishaji wa tumbaku, lakini pia unapoanzisha kiwanda mahali popote, wote humu Wabunge tungetamani kila Jimbo kuwe na kiwanda. Hata hivyo, kiwanda unaanzisha kwa kutugemea cost benefit, unatazama wapi nikiweke hiki kiwanda ambacho kitanilipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya makampuni Morogoro ilijaliwa kwa Mwenyezi Mungu mwenyewe katika kuwa pale, kwa sababu ndiyo mikoa michache ambayo ilikuwa na rasilimali nzuri tangu wakati huo, lakini pia ndiyo sehemu iliyokuwa na maji ya uhakika, kulikuwa na umeme wa uhakika, lakini pia Morogoro ndiyo karibu na Dar es Salam ambako ndiyo kuna bandari kuu ya kusafirisha mazao. Kwa ushahidi huu ndiyo maana hata sasa hivi wafanyabiashara binafsi bado wanaitamani kuwekeza Morogoro kwa sababu ya jiografia na hali ya hewa iliyokuwepo Morogoro. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nichukue nafasi hii Serikali muendelee kutupa nafasi kubwa zaidi Morogoro kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda kwa sababu mazingira ni rafiki ambayo yanavutia na yana gharama nafuu sana ya uendeshaji. Nitoe mfano tu, hiyo tumbaku inazalishwa songea, Morogoro, Iringa na Tabora na mikoa mingine. Siyo rahisi kwa mwekezaji kuweka kila kiwanda katika kila mkoa ni kwa sababu inategemea na wingi wa raw material. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nizungumzie kuhusu wajasiriamali. Mpango huu umekuja lakini umeweka nje wajasiriamali, kwa sababu tukizingatia hivi maendeleo ya viwanda ambao ndiyo Mpango wa muda wa Pili huu unakuja utategemea sana maendeleo ya kilimo. Hata hivyo, wajasiriamali wa nchi hii, hususani wanaojishughulisha katika mazao ya kilimo wamewekwa kando ya mfumo wa soko letu hapa Tanzania. Leo hii mfanyabiashara au kijana aliyemaliza elimu ya Chuo Kikuu au elimu ya sekondari ambaye anataka kujiajiri mwenyewe hususani katika shughuli za kilimo hana fursa hiyo kwa mfumo wa soko uliokuwepo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kijana aneyesifiwa mfanyabiashara mzuri ni yule anayefanya importation, akienda nje ya nchi akinunua mazao kitu chochote bidhaa amuuzie mkulima huyo anaruhusiwa na atapewa vigelegele, lakini yule ambaye anakwenda kununua mazao kwa mkulima afanye exportation ataambiwa mwizi, kibaraka, mnyonyaji, kibaraka wa Wahindi na majina yote ya ajabu ajabu atapewa huyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali waje na Mpango mzuri jinsi ya kuliboresha soko letu ili sekta hii ya sehemu hii wafanyabiashara wadogo, wakati na wakubwa waweze kushiriki kikamilifu katika ununuzi wa mazao ya biashara kutoka kwa wakulima moja kwa moja. Kwa sababu sasa hivi mfumo uliopo umewatenganisha kati ya mnunuzi na muuzaji. Leo hii mnunuzi hajui mzalishaji anahitaji nini na mzalishaji hajui mnunuzi anahitaji nini kwa viwango ambavyo wanavitaka. Matokeo yake baadaye biashara zetu zinakosa masoko baada ya uzalishaji na hatimaye wakulima wetu wanakuwa watu wa kuhangaika, leo wanazalisha zao hili, kesho zao lile, hakuna zao moja ambalo ana uhakika nalo la kumuinua kimaisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nizungumzie mgogoro wa wafugaji na wakulima. Sisi Morogoro kiasili ni wakulima lakini sasa hivi tumevamiwa kwa kiasi kikubwa na wafugaji wasiofuata sheria, taratibu hata na kanuni zile za kufuga. Baada ya kuchunguza muda mrefu nimeona wanahama kwa sababu wanakosa malisho maji huko wanakotoka. Niiombe Serikali ije na mpango mkakati wakuboresha miundombinu ya wafugaji huko wanakotoka na kuwapa elimu ya kufuga kisasa ili waendele kubaki huko ili janga ambalo mnatuletea Morogoro limeshakuwa kubwa linatuzidi uwezo wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kwa mfano jana tu, wakulima wangu kule Kata ya Tununguo na Vijiji vyake wamepigwa na wafugaji. Mfugaji anakuja anaingia ndani ya shamba anamwambia mkulima kwamba, mifugo ni muhimu kuliko chakula wanageuza mazao ya wakulima ndiyo chakula cha mifugo. Wanawatandika bakora hata wakienda sehemu yoyote hawasikilizwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali ije na Mpango mkakati wa kumaliza tatizo hili la wafugaji nchini, hasa kujenga miundombinu ya wafugaji sehemu za wafugaji na kupima ardhi yote ili tuweze kujua eneo la wafugaji lipi na wakulima? lakini hasa kuimarisha hiyo miundombinu ya kifugaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho haina maana kwa umuhimu, kuhusu suala hapo hapo suala la kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo na najua maendeleo ya viwanda vinakuja baada ya maendeleo ya kilimo kuwa endelevu. Serikali kwenye Mpango wenu mmesema kabisa haijafanya vizuri kwenye kilimo, bila kuimarisha kilimo hata hivi viwanda tunavyotaka kuviweka vitakuja kukosa raw material baadaye italazimika tu-import raw material kwa ajili ya viwanda hivyo. Niishauri Serikali ije na Mpango Mkakati thabiti wa kuimarisha kilimo, kuongeza uzalishaji, kuwavutia masoko ili ku-adress matatizo ya wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu. (Makofi)