Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa binafsi nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa bajeti ya Wizara yake pamoja na hotuba yake nzuri iliyojaa mazuri na mambo ambayo yametoa kiu za wananchi. Pamoja na style yake ya kutoa mabegi yaliyojaa mambo yote yanayohusu Wabunge na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kumpongeza Mheshimiwa Waziri sina budi kumshukuru kwa kunipatia Baraza la Ardhi katika Wilaya ya Lushoto ambalo lipo kwenye Jimbo langu kwani mchakato huu niliufuatilia wakati tupo kwenye Kamati yako ya Ardhi. Hivyo hujasita kuondoa kiu yangu na ya wananchi wa Lushoto kwa kiujumla na kuahidi kuja kufungua Baraza hilo mwezi wa saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya ardhi, Mheshimiwa Waziri migogoro ya ardhi ipo katika nchi nzima lakini ndani ya Jimbo la Lushoto kuna migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na wakulima hasa maeneo ya Bwei, Kilole na Mlola, yote haya yanasababishwa na eneo dogo lililopo katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mwekezaji wa kiwanda cha mbao kinachoitwa Mombo Saw Mill. Kiwanda hiki kilikufa takribani miaka 20 iliyopita, lakini Mheshimiwa Waziri eneo hili linapakana na shule ya sekondari ya St. Mary’s - Mazinde Juu na shule hii ni ya boarding kwa ajili ya wasichana. Mheshimiwa Waziri eneo hili limekuwa ni kichochoro cha watu kuingia katika eneo la shule ukizingatia eneo hilo linapakana na shule hiyo na upande lilipo ndiyo mabweni ya wanafunzi. Father amemfuata mwenye eneo lakini hakuonesha ushirikiano kwa sababu mwenye eneo hili anashirikiana na watu wabaya ambao hawana nia nzuri ya shule hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninakuomba Mheshimiwa Waziri kwa heshima na taadhima na kwa unyenyekevu mkubwa, suala hili uliingilie kati, eneo hili liweze kurudi ili liungane na eneo la shule. Ninashauri hivyo kwa ajili ya kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza, sambamba na hilo eneo hili halijalipiwa kwa muda mrefu sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ningeomba Mheshimiwa Waziri Mungu akikujalia kufika Lushoto kufungua Baraza la Ardhi, utembelee eneo hilo la Magamba na shule ya sekondari Mazinde Juu kwa ajili ya kupata maelezo ya kina kwenye uongozi wa shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Lushoto kuna muingiliano mkubwa wa watumishi wa ardhi, hii imepelekea ujenzi holela na urasimu wa kupata hati ni tatizo kubwa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimtakie Mheshimiwa Waziri utumishi uliotukuka huku wananchi wa Lushoto wakiendelea kukuombea kwani wana imani kubwa sana na wewe.