Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwapongeza Wizara ya Ardhi ikiongozwa na Waziri Mheshimiwa William Lukuvi kwa kuonyesha nia ya kutatua migogoro ya ardhi kwa kushirikisha wadau wa ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumshukuru Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri wa Ardhi na Waziri wa Maliasili kwa kuonyesha uongozi na nia ya kumaliza mgogoro wa ardhi katika msitu wa Kazimzumbwi uliopo katika Kata za Chanika, Zingizwa, Buyuni na sehemu ya Pugu ambao umedumu tangu mwaka 1994 kutokana na kupunguza mipaka mwaka 1954.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu kumaliza mgogoro wa Bonde Msimbazi hasa maeneo ya Kinondoni, Segerea na Ukonga ambapo nyumba za wananchi zimewekwa alama ya “X” na zingine kubomolewa, huko ni kuwarudisha nyuma wananchi wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu Mheshimiwa Waziri kumaliza mgogoro wa Kipawa Kipunguni, eneo la Uwanja wa Ndege. Pia mgogoro wa ardhi kati ya watu wa kutoka Kipawa na Kipunguni waliopelekwa Kinyerezi Pugu na Buyuni katika Jimbo la Ukonga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kulinda maeneo ya umma kama vile shule, zahanati, masoko na polisi; ni muhimu upimaji na kulinda maeneo ya huduma za jamii liwe shirikishi kwa viongozi wa mtaa, kata, Wabunge na wananchi ili kuondoa mianya ya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za upimaji ni kubwa sana kiasi kwamba wananchi wengi wanashindwa hivyo kuishi bila kupima maeneo yao. Ni vema Wizara ikaangalia namna ya kupunguza kero hizo ili wananchi walio wengi au wote wapime ardhi yao ili kujipatia manufaa ikiwemo uwezekano wa kukopesheka katika vyombo vya fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Ardhi iongeze kasi ya kuondoa migogoro ya ardhi na hasa maeneo ya maliasili ili watu wetu waishi kwa amani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwapongeza Wizara ya Ardhi walau kwa kuweka mipango shirikishi na kuanza kumaliza baadhi ya migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.