Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii na ni mara yangu ya kwanza kuongea kutoka back bench. Naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutoa mchango wangu ndani ya Bunge hili na naahidi kushirikiana na wengi ili tuweze kutoa mchango wa Bunge kama unavyotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuwashukuru kwa dhati wananchi wa Wilaya na Jimbo la Hanang walionipa kura nyingi kurudi hapa Bungeni. Kulikuwa na changamoto na hujuma nyingi lakini hawakutetereka. Naomba waendelee kusimama na msimamo huu wa kujenga Wilaya yetu. Wale wabinafsi wakae kule wenyewe na sisi tuendelee kuliendeleza Jimbo letu la Hanang. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda sana kuwashukuru wananchi wa Hanang kwa kumpa Rais John Pombe Joseph Magufuli kura nyingi na CCM ikapita. Nashukuru sana na nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu amedhihirisha kutoka CCM wananchi wa Tanzania wanaweza wakapata mabadiliko ya kweli na ya uhakika. Kwa sababu wengi walifikiri mabadiliko yanaletwa na vyama vya upinzani lakini Mheshimiwa Rais ameonesha kwamba mabadiliko yaliyo dhahiri na ya uhakika yataanzia kutokana na Mpango huu wa pili na wa kwanza wa miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye Mpango ambao uko mbele yetu. Msingi wa Mpango huu ni ujenzi wa uchumi wa viwanda. Ujenzi wa uchumi wa viwanda utaleta maendeleo ya watu na si maendeleo ya vitu kama utaunganishwa na maendeleo ya kilimo, mifugo na uvuvi, shughuli ambazo zinahusu Watanzania walio wengi. Mimi kama Mbunge wa Hanang nashukuru sana kwa sababu Wilaya yangu kwa kiasi kikubwa ni ya mifugo, ni ya ukulima na kutokana na Ziwa Basotu kuna wavuvi vilevile. Kwa hiyo, viwanda vikijielekeza kwenye kuendeleza tija ya kilimo maendeleo ya watu yatapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tutambue kwamba kilimo kimekuwa ni shughuli ya watu wengi lakini na inaonesha kwamba maendeleo ya kilimo yanasuasua. Jambo moja ambalo ni dhahiri ni kwamba lazima tuunganishe mnyororo wa thamani ya mazao ya kilimo jambo ambalo liliharibika wakati wa ukoloni lakini hatujawahi kulirudisha mpaka leo. Viwanda hivi vitasaidia kwa sababu kwanza kutokana na viwanda teknolojia inayotakiwa kwenye kilimo itapatikana, zana bora zinazotakiwa kwenye kilimo na mifugo zitapatikana pia. Badala ya kuuza mazao yetu nje bila ya kuongeza thamani viwanda hivi vitasaidia kuunganisha mnyororo ule. Kwa hiyo, naomba sana viwanda ambavyo tutavianzisha viwe na uhusiano wa karibu sana na kilimo, mifugo na uvuvi bila ya kusahau utekelezaji wa Liganga na Mchuchuma ambavyo ni viwanda mama vitakavyojenga viwanda vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni uhai, maji ni maendeleo na maji ni siasa. Ukiangalia katika kampeni ambazo tumezimaliza juzi wananchi wa Tanzania walio wengi walikuwa wanadai maji. Maji ni kazi ya akina mama ambapo wanaacha watoto nyumbani wanaanguka au wanaungua na moto kwa sababu ya kutafuta maji kwa umbali mrefu. Bila maji itakuwa ni vigumu sana viwanda kuendelezwa. Kwa hiyo, naomba sana, kabla sijafika kwenye maji, kuna misingi ambayo tunapaswa kuitekeleza katika Mpango huu. Kwa mujibu wa makubaliano hata ya kimataifa, sekta ya kilimo inapaswa kupewa si chini ya asilimia kumi ya bajeti kila mwaka ndipo ambapo tutaona maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango huu, mkiunganisha na maji, suala la kujenga mabwawa ya kumwagilia ambayo yatatoa maji kwa mifugo na kusaidia maji hata kwa wananchi litakuwa ni suala muhimu. Maji ni muhimu kwa ajili ya uhai lakini yatasaidia vilevile kuongeza tija kwenye kilimo. Kwa hiyo, naomba suala la mabwawa tulitilie mkazo katika Mpango huu na mimi narudia kusema tena kuhusu suala la Wilaya ya Hanang ya kuomba maji ya Mlima Hanang yakusanywe kwenye Bwawa la Gidahababieg ili watu waweze kupata maji ya uhakika, ili watu waweze kufanya kilimo cha umwagiliaji na ili mifugo mingi ya Hanang nayo iweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka kwenye wilaya ya wafugaji, watu wanaohamahama. Naomba nikazie elimu kwani ndiyo itakayobadilisha mindset ya wafugaji wanaohamahama. Ili tuweze kuhakikisha watoto wa wafugaji wanapata elimu ya uhakika, naomba Mheshimiwa Waziri wa Elimu na wale wote wanaohusika na TAMISEMI waone suala la mabweni na hosteli kwenye Wilaya za wafugaji linatiliwa mkazo kwa sababu hawataacha kuhama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kengele ya kwanza imelia, naomba niseme kwamba jamani nzi anakwenda pale ambapo kuna mzoga haendi kwenye marashi. Kwa hiyo, tukitaka mambo ya polisi na FFU kutokuingia humu ndani, naomba Wabunge tuwe waungwana wakati tunatoa michango yetu. Humu ndani sisi ni Wabunge, sisi ndiyo dira ya wananchi, ni wawakilishi wa wananchi, tukileta fujo humu ndani, tunaashiria kwamba kule nje napo wafanye fujo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana tuwe watulivu, tuwe waungwana, tuheshimiane humu ndani na tuliweke Taifa letu mbele ili tuongee mambo yanayohusu maendeleo ya watu wa Tanzania badala ya kuongelea mambo ambayo kila mmoja anataka ajiinue ili aonekane. Tukiwa waungwana, tukitumia muda wetu vizuri, wananchi wa Tanzania watatuona zaidi kuliko tunavyopiga kelele humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda ni mdogo, naomba niishie hapa na mimi nitasaidiana na Waziri wa Mipango kwa sababu nilikuwa naye kabla nikiwa Waziri wa Mipango …
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Katika kuleta mambo ambayo yatasaidia Mpango huu. Ahsante sana. (Makofi)