Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri.
Naomba niende moja kwa moja kwenye masuala machache, sasa hivi Wizara inafanya mapito makubwa ya sera ya ardhi na tunaona huko mikoani inaendelea. Naomba kwa hatua hii Wizara isifanye makosa waliyofanya mwanzoni pale. Baada ya sera ya mwaka 1995 waliandaa sheria halafu baadae ndiyo wakaja kuandaa mkakati wa kutekeleza sheria. Kilichokuwa kinatakiwa ni kwamba baada ya sera unaandaa mkakati wa Taifa ambao unakwenda sambamba na programu ya Kitaifa ya kutekeleza sera, halafu ndiyo unakuja unamalizia na sheria. Kwa hiyo, naomba safari hii wazingatie huo mfuatano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye utekelezaji wa sera tunahitaji mambo mawili makubwa, kwanza awareness ya wadau wote waielewe sera, lakini pili tunahitaji rasilimali, rasilimali watu hiyo ni ya kwanza kabisa na rasilimali fedha. Kwa miaka mingi fedha ambayo imekuwa ikitengwa au inaombwa na Wizara hii imekuwa ni kidogo mno. Ndiyo maana Wizara hii ina upungufu mkubwa wa Maafisa Ardhi, Maafisa Mipango Miji, Wapima, Wathamini, Wachora Ramani, Wakadiriaji Majengo na kadhalika. Kwa kifupi ina nguvukazi kidogo sana, sidhani kama hiyo nguvukazi inaweza kutekeleza sera kama wanavyotaka. Vilevile rasilimali fedha imekuwa inapangwa kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ukiangalia taarifa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri viwanja vilivyopimwa mwaka huu 2015/2016 ni 112,000 tu angalau wangepima 400,000 ingekuwa ni afadhali kwa nchi yetu. Kati ya hivyo viwanja 112,000 viwanja 38,700 vyote vimepimwa Dar es Salaam na Pwani ambayo ni asilimia 35, huu ni upungufu mkubwa sana. Hati miliki zilizosajiliwa 25,000 tu angalau wangekuwa na uwezo wa kusajili hati 100,000 kwa mwaka ingetusaidia kama nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama trend ni hii ina maana kwamba hata hii mipango kabambe ya majiji, manispaa na miji yetu inayoandaliwa haitaweza kutekelezeka kwa sababu ya ufinyu wa rasilimali fedha na upungufu wa rasilimali watu. Naomba sana Wizara ijipange ili kwenye mwaka mwingine unaokuja baada ya mwaka ujao (2017/2018), waje na mkakati wa maombi ya fedha za kutosha ili utekelezaji ufanyike vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna upungufu wa nguvu kazi au upungufu wa uwezo wa kutumia fedha. Katika mwaka huu wa fedha walipanga kutumia shilingi bilioni 3.45 kwa ajili ya miradi ya maendeleo wamepata shilingi bilioni 3.43 ambayo ni sawasawa na asilimia 99, lakini hotuba ya Waziri inatuambia wametumia milioni 745 tu ambayo ni asilimia 21. Ina maana hata kama tukiwapa pesa kumbe uwezo wa kutumia fedha yaani ile absorption capacity inavyoelekea kwa Wizara hii ni ndogo sana, sasa sijui watajipangaje. Mheshimiwa Waziri atakaposimama atueleze vizuri wamejipangaje, hivi uwezo wa kutumia fedha tufanyaje, sisi Wabunge tumsaidie vipi ili Wizara hii iwe na uwezo wa kutumia fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mwingine ni Shirika la Nyumba la Taifa, utekelezaji wake nao ni mdogo sana. Mahitaji ya nyumba kwa nchi yetu ni 200,000 kwa mwaka, lakini wao wamepanga kujenga nyumba 5,000 tu kwa mwaka ukilinganisha na nyumba 200,000 yaani ni upungufu mkubwa sana. Mahitaji ya jumla ya nchi yetu sisi tunahitaji nyumba 3,000,000, tutafikia lini malengo haya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.