Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuchukua fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii ya Waziri wa Fedha.
Kwanza, niwashukuru sana wapiga kura wa Jimbo la Lulindi ambapo katika uchaguzi uliopita nilishinda Ubunge kwa asilimia 87. Siri kubwa ya ushindi katika uwakilishi kwa wananchi ni kupunguza maneno na kufanya kazi na kuondoa kero kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa hatua zote anazoanza katika kuhakikisha Taifa hili linaelekea kwenye uchumi wa kati, nampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuwapa pole sana wapiga kura wangu kwa maafa waliyopata kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika vijiji vya Matogoro kule Msanga, Mkangaula, Lupaso na maeneo mengine ambayo sikuyataja, nawapa pole sana na nataka kuwahakikishia kwamba nipo pamoja nao katika mkasa huu uliowapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda moja kwa moja katika hoja, nianze kuzungumzia kuhusu mapato. Kwanza, nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Naibu wake na timu nzima ya Wizara ya Fedha kwa jinsi ambavyo imejipanga kuhakikisha kwamba tunakusanya mapato ya kutosha ili tuweze kwenda kuondoa kero za wananchi ambapo kwa muda mrefu wamekuwa wakisubiri huduma kutoka Serikalini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niishauri Wizara ya Fedha na watendaji, baadhi ya watendaji wengi hapa nchini wanashindwa kuwa wabunifu wa vyanzo ni kwa sababu wenyewe wanaendelea kupata riziki yao kwa maana ya mshahara na wanaendelea kupata pensheni baada ya kustaafu, wako tofauti kabisa na taasisi za binafsi ambapo wenzetu wamekuwa wabunifu sana. Mimi naomba sana tuhakikishe tunakuwa wabunifu na kupata vyanzo vipya vya mapato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunacho chanzo kikubwa sana cha mapato ambacho hatukitumii cha property tax. Mheshimiwa Mnyika atakubali kule Dar es Salaam tunazo nyumba nyingi sana kama zingeweza kulipa property tax vizuri na tukawaweka katika makundi mawili, wale ambao tunaweza kutathmini nyumba zao lakini wale ambao tunaweza kuwaweka katika kundi la ukadiriaji na tukakadiria katika kiwango ambacho mwananchi anaweza akalipa, ni chanzo kikubwa sana cha mapato. Naomba Wizara na Halmashauri ziweze kuona ni jinsi gani tunaweza tukakusanya mapato kutoka kwenye chanzo hiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuziwezesha halmashauri zetu kuweza kukusanya mapato ni jambo lingine. Kwa mfano, Halmashauri yangu ya Wilaya ya Masasi, tarehe 23 Januari, 2013 nilipata janga kubwa sana la watu waliovamia Halmashauri na kuchoma magari 11 lakini pia kuchoma ofisi tano. Serikali ilituahidi kwamba halmashauri yetu ingeweza kupata fidia ya shilingi 1,337,000,000/= lakini tangu mwaka 2013 hadi sasa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Masasi imekuwa ikifanya kazi katika mazingira magumu sana. Kwa hiyo, hata viwango tunavyopangiwa kukusanya tunapata ugumu mkubwa sana. Namwomba Waziri wa Fedha, namuona Naibu yupo, hebu chukueni jambo hili ili kuhakikisha kwamba Halmashauri hii inapata fidia ili tuweze kununua magari, tuweze kutengeneza majengo yale ili ifanye kazi yake inavyostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye suala zima la barabara. Barabara ni jambo muhimu sana na sisi wote tunajua. Kwa mikoa ya Kusini sisi ni wazalishaji wakubwa wa zao la korosho na moja ya barabara ambayo ni ya kiuchumi ni ile inayotoka Mtwara – Newala - Tandahimba - Masasi kupitia Lulindi. Barabara hii imeahidiwa na Mheshimiwa Rais na ipo kwenye Ilani na tayari kuna dalili za kuanza kujenga barabara hii.
Naiomba sana Wizara ya Fedha na Wizara ya Miundombinu kuhakikisha katika miaka mitano barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingine ni barabara ya Ulinzi. Katika miaka mitano iliyopita tumezungumza sana juu ya barabara ya Ulinzi ambayo inapita kwenye zaidi ya Majimbo manne. Jimbo Mtwara Vijijini kwa Mheshimiwa Hawa Ghasia, kwa Mheshimiwa Mkuchika, kwa Mheshimiwa Katani kule Tandahimbi, kwangu kwenye Jimbo la Lulindi na kwa Mheshimiwa Dua kule kwenye Jimbo la Nanyumbu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ilikuwa na madhumuni makubwa mawili, kwanza ilikuwa ni barabara ya ulinzi. Wakati ule tunapigana na Mreno kule Msumbiji barabara hii ndiyo ilitumika vizuri sana kuhakikisha kwamba tunapambana naye. Pia tulianzisha vijiji vya ulinzi katika barabara yote hii lakini vijiji vile vyote havipati huduma ya barabara kwa sababu tuliiombea iingizwe kwenye TANROADS lakini hadi sasa Wizara haijakubali. Namuomba sana Waziri anayeshughulika na Wizara hii ya Miundombinu tuhakikishe kwamba barabara ile tunaiweka TANROADS ili iweze kutengenezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilitaka nilieleze ni suala zima la umeme. Nimshukuru sana Mheshimiwa Profesa Muhongo, tulikuwa wote kwenye Kamati ya Nishati na Madini, kwa kweli kazi yake kila mmoja wetu hapa tunakiri ni kazi iliyotukuka, hongera sana Mheshimiwa Profesa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa ameeleza hapa kwamba wanatagemea kwenda Mtera kufanya tathmini ya REA I na REA II, yako mambo ambayo ningeomba mkayazungumzie. Kwanza, ni kwamba kwenye REA I na REA II idadi ya wananchi wanaotakiwa kupewa umeme kwa bei ya shilingi 27,000/= ni ndogo sana ukilinganisha na mahitaji. Kwa hiyo, jambo hili ni muhimu sana mkalizungumzie ili kuhakikisha kwamba idadi ile inaongezeka kulingana na hali halisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ambalo limejitokeza ni kwamba wakati vijiji vinavyowekwa kwenye mradi wale wanaokwenda kufanya survey wanaacha vijiji vya katikati bila kuviingiza kwenye mpango, jambo ambalo linatusumbua sana wakati mpango ukiendelea. Ningeomba sana Profesa hili mkalishughulike kwa nguvu zenu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tayari kengele ya kwanza imeshagongwa, nichukue fursa hii kuzungumzia suala la viwanda. Kule Kusini zao letu la korosho linahitaji kuongezewa value lakini itategemea na jinsi ambavyo tutaanzisha viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Waziri mwenye dhamana afanye juhudi katika miaka mitano hii kuhakikisha kwamba viwanda vya korosho vinafufuliwa katika Mikoa ya Kusini ili korosho ipewe thamani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuokoa muda, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, ahsante sana. (Makofi)