Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii adhimu ya kuweza kuchangia katika hotuba hii. Ningependa kuendelea kupongeza jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali. Pia ningependa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mwakilishi wa vijana sisi vijana tunatambua kazi kubwa ambayo inafanywa na Shirika la Nyumba la Taifa yaani NHC, lakini tungependa kuiomba Serikali kwa kuzingatia kwamba takwimu zinaonesha uwiano wa jumla ya idadi ya watu, vijana ndio wanaochukua asilimia kubwa; lakini pia kwa kuzingatia asilimia 59 ya nguvu kazi ya Taifa ni vijana. Basi vijana waweze kutengenezewa utaratibu wa kipaumbele wa kupata nyumba hizi za NHC lakini za bei rahisi. Kwa wale vijana ambao wanaanza kufanya kazi, wanaoajiriwa, wanakuwa na kazi basi na wenyewe watengenezewe utaratibu wapate hizi nyumba za bei nafuu. Hiyo bei nafuu iwe kweli bei nafuu na isiwe bei nafuu kwa kiwango fulani ambacho vijana watashindwa kuzimudu bei zake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kuishauri Serikali yangu sikivu juu ya umiliki wa ardhi. Sheria namba nne ya ardhi na sheria namba tano ya ardhi zinaeleza kwamba mmiliki wa ardhi ya Tanzania atakuwa ni Mtanzania na sio mgeni na kama mgeni akitaka kumiliki ardhi atamiliki ardhi kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC) na kuna utaratibu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria namba nne kifungu cha 20(4) kinaeleza bayana kwamba kampuni inayokuwa na shareholders wa kigeni yaani share nyingi kwa mtu ambaye ni mgeni, kampuni hiyo inakuwa ni kampuni ya kigeni na kampuni ya kigeni kwa sheria za Tanzania hairuhusiwi kumiliki ardhi ila pasipokuwa tu kwa kupitia TIC yaani kwa maana ya uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna utaratibu ambao wageni wanautumia; wageni wanakuja wanashirikiana na wazawa wanasajili kampuni lakini katika share structure ya hiyo kampuni inaonesha kwamba wazawa ndio wana-share nyingi zaidi lakini baadaye, baada ya kumiliki ardhi wanakuja wanabadilisha ile share structure na share structure inaonesha kwamba yule mgeni anakuwa ana share nyingi zaidi, yaani ni majority shareholder. Kwa hiyo, inaifanya ile kampuni inakuwa ni foreign company, yaani kampuni ya kigeni lakini inakuwa bado imemiliki ile ardhi. Kwa hiyo, inakinzana na hii sheria ambayo inasema mgeni na kampuni la kigeni haliruhusiwi kumiliki ardhi Tanzania pasipokuwa kwa utaratibu maalum ambao umewekwa chini ya Kituo cha Uwekezaji (TIC).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali itengeneze utaratibu yaani Msajili wa Makampuni BRELA pamoja na Kamishna wa Ardhi kuwe kuna mawasiliano ili kuweza kubaini mabadiliko haya ya share structure ili kuhakikisha kwamba makampuni ya kigeni au wageni wasitumie makampuni haya kwa kuchezesha hizi share structure kutumia kumiliki ardhi ya Kitanzania tofauti na utaratibu na sheria za nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa sana kuishauri Serikali yangu kuhusiana na sheria yetu hii kwa mfano Sheria ya Ardhi namba tano, kifungu cha 18 kinaeleza bayana kwamba, ardhi au haki yaani customary right of occupancy ina hadhi sawa na granted right of occupancy yaani haki miliki ya kimila ina hadhi sawa na hati miliki ya kupewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii ipo kisheria, iko pia kama yaani sera au kama sheria, lakini kiuhalisia hizi hati za kimila hazina haki sawa na hizi hati miliki ya kupewa. Kwa sababu mtu ambaye ana hii customary right of occupancy ambayo ni hati miliki ya kimila hawezi kwenda benki akataka kuikopea au kupata mkopo ku-mortgage kwa sababu atapata kipingamizi, itaonekana haifai, haitoshi, haina kiwango sawa pamoja na hii hati miliki ya kupewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tunajua vijana wetu wengi waliopo hata huko vijijini wana hizi ardhi na wangependa kutumia hii ardhi waliyoletewa na Mwenyezi Mungu katika Taifa hili kwa ajili ya manufaa yao wao wenyewe na kuboresha uchumi wa Taifa. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kuangalia kwamba hii section 18 ya Village Land Act iweze kuwa na uhalisia kwa sababu ipo tu academically lakini kiuhalisia hati miliki ya kimila haina hadhi sawa na hati miliki ya kupewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kushauri kuhusu Mabaraza ya Ardhi; Mabaraza ya Ardhi yalianzishwa ili kusaidia kupunguza migogoro ya ardhi, lakini kuharakisha hii migogoro ya ardhi iweze kwisha kwa wakati. Tofauti na matarajio kimsingi haya Mabaraza ya Ardhi yanaonekana yameelemewa; kesi zimekuwa nyingi, zinachukua muda mrefu hadi miaka mitano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu kwa Serikali, kabla sijakwenda nataka nisome Katiba ya Jamhuri ya Muungano na kabla sijaenda huko nilikuwa napenda ifahamike Mabaraza haya ya Ardhi ya Kata yanasimamiwa na Wizara ya TAMISEMI; lakini Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya yanasimamiwa na Wizara hii ya Ardhi, lakini ukija kwenye mahakama unakuta mahakama inasimamiwa na Wizara ya Katiba na Sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, unakuta kwamba kuna Wizara tatu tofauti ambazo zimepewa mamlaka ya kusimamia jambo ambalo ni moja. Ukisoma Katiba, Ibara ya 107(a) utakuta imetamka bayana kwamba mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano itakuwa ni mahakama. Sasa haya Mabaraza ya Ardhi yanafanya kazi ya kutoa haki ambacho ni kinyume na Katiba nadiriki kusema. Kwa sababu mahakama ndiyo chombo cha mwisho cha kutoa haki na sisi tunajua haya Mabaraza yanachukua muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama yameshindwa hii kazi na naweza kudiriki kusema naona yameelemewa, basi hii kazi ya kutoa haki irudishwe katika mfumo wa mahakama, kuanzia Mahakama za Mwanzo mpaka kufika mwisho katika mfumo wa mahakama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizingatia Ibara ya 113 ambayo imeelezea majukumu ya Tume ya Utumishi wa Mahakama, inasema, jukumu mojawapo la Tume ya Mahakama ni kuajiri Mahakimu na kusimamia nidhamu yao. Kwa hiyo, katika mfumo wa mahakama hawa Mahakimu wanasimamiwa na sheria na nidhamu zao zinasimamiwa kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, wana mamlaka ya kuwawajibisha lakini hawa viongozi wanaokaa katika Mabaraza ya Kata, ya Wilaya hamna mamlaka ya kushughulikia nidhamu zao. Hakuna bodi ambayo ina-deal na ethics zao, hivyo, ningeomba sana Serikali iweze kuleta Muswada kwa ajili ya kurekebisha hizi sheria zilizoanzisha haya Mabaraza ya Ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba mahakama ina uwezo mkubwa sana wa kuendelea kutekeleza au ku-solve haya matatizo na changamoto za ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba pia Waziri wakati anahitimisha aweze kutoa kauli juu ya uhalali wa kukopesheka kwa hati hizi za kimila kwa sababu vijana sisi tunajua wengi wetu tunazo hizi hati; tunataka ziweze kutumika kwa ajili ya manufaa yetu, sheria inatamka kwamba zina haki sawa pamoja na hizi hati za Kiserikali. Kwa hiyo, tunaomba Waziri atamke ili ifahamike na ziweze kutambulika kwamba zina hadhi sawa katika mabenki ili tuweze kukopa kwa kuzitumia hizi hati za kimila. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.