Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nichangie Wizara hii muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuonesha masikitiko yangu kwa Mheshimiwa Waziri. Nimeona kwenye kile kitabu cha migogoro ya ardhi, Wilaya ya Karatu haipo. Nilimkabidhi mmoja wa wahudumu wa hapa ndani orodha ile na nikamsindikiza kwa macho yangu, Mheshimiwa Waziri alikuwa amekaa pale, alimkabidhi na aliisoma. Simlaumu, nimemwandalia orodha nyingine hii hapa ambayo ni more comprehensive. Nitampatia baadaye, ikibidi nipige picha ili nipate ushahidi kwamba nimemkabidhi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri imeainisha mamlaka tatu ambazo zinashughulikia masuala ya ardhi. Ziko mamlaka za Halmashauri za Vijiji, iko mamlaka za Halmashauri ya Wilaya na Mji na iko pia Wizara yake. Namwomba Mheshimiwa Waziri asiogope, asihofu. Akiona tunakuja kwake iwe ni kiashiria tosha kwamba wale walioko kule chini wameshindwa. Pia ionekane kwamba inawezekana wale walioko kule chini pia wanachangia katika matatizo yaliyopo. Kwa hiyo, tunakuja kwake kwa kuwa tumeshakata tamaa na wale ambao walipaswa kutusaidia kule chini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo migogoro mingi ya ardhi na migogoro hii mingine imesababishwa na sera. Tunayo ile sera iliyokuja mwaka 1975 ya Operesheni Vijiji, imeleta mkorogano mkubwa sana. Pia migogoro mingine imesababishwa na sisi viongozi wa kisiasa. Pia iko migogoro mingine na ndiyo mingi zaidi, imesababishwa na baadhi ya Watendaji katika ngazi mbalimbali za utendaji wao; Mabwana Ardhi wa Wilaya na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, akiona tunakuja kwake awe na amani kabisa. Tuna nia njema, amejaribu, nami naamini hatabadilika, aendelee na kasi hiyo. Tuna imani kiasi fulani kwamba amejaribu na ataendelea na kasi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo migogoro mingi sana ya ardhi. Wamesema Wabunge wengine, shida kubwa ya ardhi ya nchi hii, haijapimwa. Kuna shida gani kupima ardhi ya nchi hii na kuwamilikisha wale ambao wanayo? Kitabu cha Waziri kimesema ni asilimia 15 ya ardhi ya Tanzania ndiyo imepangwa na imepimwa, nami naamini hii ni ardhi iliyoko mijini, ardhi kubwa iliyoko vijijini inaonekana haina mwenyewe, lakini ile ardhi ina mwenyewe, yuko yule ambaye ameikalia hadi sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba na naishauri Serikali, kama kweli tuna nia ya dhati ya kumaliza migogoro hii au kuipunguza kwa kiwango kikubwa, Serikali ije na mpango madhubuti wa kupanga, kupima na kumilikisha ardhi kisheria. Bila kufanya hivyo, migogoro ya ardhi, leo utatatua, kesho utazaliwa mwingine. Kwa hiyo, kila kukicha utaendelea kupata migogoro hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ana mpango mzuri anaoufanya kule Ulanga na Kilombero; program ya upimaji wa ardhi katika zile Wilaya tatu, ni mpango mzuri, lakini atamaliza Tanzania baada ya miaka mingapi? Kama kwa miaka mitatu anafanya mpango wa majaribio katika Wilaya tatu. Anahitaji zaidi ya miaka 50 kupima ardhi ya nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri na ameandika pale, amesema mpango ule ukifanikiwa utasambaa katika nchi nzima. Majibu anayo, mpango ule lazima ufanikiwe, ikibidi akahamie kule yeye mwenyewe asimamie ile kazi ili ule mpango ufanikiwe ili ardhi ya wananchi ipimwe na wamilikishwe kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye eneo la mashamba ya wawekezaji, nchi hii inawaabudu sana hawa watu wanaoitwa wawekezaji. Nimeangalia kwenye kile kitabu iko jumla ya karibu ekari milioni 5.6 ambazo hawa waheshimiwa wamezikalia. Sisi kule Karatu tunayo mashamba 40 ambayo yana jumla ya ekari 45,000 hainingii kwenye akili kwanza kwa nini hawa watu walipewa mashamba haya? Kwa sababu, mashamba mengi wamepewa kwa ajili ya kulima na kufuga, wengi wa hawa ni watu waliotoka nje, hivi tulikuwa tunahitaji mtu atoke Ulaya kuja kufuga hapa Tanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wafugaji wazalendo ambao sasa hivi maisha yao ni kutangatanga na kuhamahama kutafuta malisho kwa sababu, ardhi kubwa imechukuliwa na hawa waheshimiwa. Hawa wawekezaji wamepewa maeneo ambayo ni very prime, yana maji, yana rutuba na yana mvua za uhakika. Wananchi wetu wamesukumwa wamekaa maeneo ambayo mvua ni kidogo sana na nimeona mashamba mengine karibu muda ule wa miaka 99 au 71 unakaribia kwisha, naomba hiyo miaka ikiisha mtushirikishe sisi watu wa maeneo hayo wasipewe tena maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri hebu atusaidie hivi hawa wawekezaji wanailipa Serikali shilingi ngapi kwa kuwa na maeneo hayo? Kwa sababu, baadhi ya wawekezaji hao badala ya kufanya yale ambayo wamekubaliana kufanya, leo wameyapangisha au kukodisha mashamba hayo kwa watu wengine na wana-charge hela nzuri tu! Kule kwetu Karatu eka moja ya shamba hilo lililoko kwenye maeneo mazuri unalikodisha kwa sh. 200,000/= kwa mwaka mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikipiga mahesabu ya harakaharaka kwa eka 45,000, ungeweza kupata shilingi bilioni tisa kutoka Karatu tu. Mheshimiwa Waziri mashamba yale 40 ya Karatu yanakuletea shilingi ngapi? Nadhani watakuwa wanaletea kidogo sana. Kwa hiyo, niombe na wengi wa hawa wawekezaji wanakaa nje ya nchi, yaani wanakuja tu kupumzikia kule wakati wa baridi kwenye nchi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye mashamba mawili ambayo yamekuwa ni tatizo katika Wilaya ya Karatu; liko shamba la mwekezaji anayeitwa Acacia Hill au Ndamakai Estate. Mheshimiwa Waziri nina uhakika anayo taarifa ya shamba hili, Mkuu wa Mkoa anazo taarifa, Mkuu wa Wilaya anazo taarifa na hata Mheshimiwa Waziri alipopita Karatu kwa muda mfupi aliambiwa habari ya shamba hili. Huyu bwana ni mbabe, ni katili, ni mkorofi na hata haijui Serikali. Ni mtu wa ajabu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu bwana anamiliki zaidi ya eka 3,840 lakini robo tatu ya eneo hilo halijaendelezwa, limekuwa ni mapori bubu ya kufugia wanyama tembo na wale wengine. Sasa siku hizi ni lazima asubuhi wototo wa shule wasindikizwe ili wasikutane na wanyama hao. Sasa mtu ana eka 3,840 ameendeleza tu robo, tena ameendeleza kwa kahawa ambayo imekwishazeeka, maeneo mengine yote ni pori! Mheshimiwa Waziri lile shamba ni size yake naomba aje autengue umiliki wa yule bwana! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini huyu bwana pia, kwa ukorofi niliousema amediriki kuwanyima wananchi barabara. Barabara ya mita sita kwa kilometa tano ukifanya mahesabu ya eneo ni karibu eka sita. Barabara ambayo inaokoa muda na gharama ya kwenda kijiji cha jirani ambacho ingebidi utumie karibu muda wa masaa mawili kwa umbali wa kilometa karibu 50, yaani kwa kukatiza pale unahitaji dakika 20, lakini huyu bwana kwa ukorofi wake amewanyima wananchi eneo hilo. Kwa hiyo, inabidi wazunguke kutoka Kijiji cha Mang‟ola Juu kwenda Kijiji cha Makumba, mtu anaingia gharama ya kwenda kilometa 40 kwa sababu ya ubabe na ukatili wa bwana huyu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba huyu bwana ashughulikiwe kabla wananchi hawajachukua hatua, kwa sababu yeye anapotaka kwenda mjini anapita kwenye maeneo ya wananchi. Tutamfungia kule kwenye kisiwa na ataishia kule! Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri achukue hatua za haraka kumnusuru huyu bwana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko shamba lingine jirani na hapo Mang‟ola Juu linaitwa Tembotembo, lina matatizo hayo hayo ni mashamba ambayo yameendelezwa kwa kiwango kidogo sana. Kwa bahati mbaya taarifa ambayo halmashauri imeandaa na taarifa ambayo iko kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri zinakinzana, lakini naamini tutashirikiana, ili kupata taarifa ambazo ni sahihi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri haya mashamba mawili naomba ayachukulie hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la uhakiki wa mipaka ya Ngorongoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.