Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Ardhi. Awali ya yote niseme kwamba Bunge hili liliunda Kamati Teule kwa ajili ya kuchunguza migogoro ya ardhi na kwa bahati nzuri, nilikuwa miongoni mwa Wabunge walioteuliwa na Mheshimiwa Spika wa Bunge la Kumi kuingia kwenye Kamati hiyo kwa ajili ya kazi mahususi ambayo Bunge liliagiza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kumpongeza Waziri Lukuvi pamoja na wasaidizi wake, kwa sababu kadri ninavyofuatilia utendaji wao ni kwamba yale mapendekezo ya ile Kamati Teule yanaendelea kutekelezwa hatua kwa hatua. Moja kati mapendekezo tuliyotoa ni kwamba Wizara ijaribu kuzi-coordinate Wizara zinazoshughulika na masuala ya ardhi; Wizara ya Mifugo, Wizara ya Maji, ili kuweza kuratibu vizuri matumizi ya ardhi yetu maana yake tuligundua kila Wizara inafanya mambo yake kuhusu masuala haya ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiona ni kwamba, hili linafanyika na mambo yanakwenda vizuri. Vilevile tulitoa pendekezo kwamba, lazima watumishi wa Wizara hii wapewe nafasi ya kwenda kujifunza, kwa sababu migogoro ya ardhi haipo Tanzania peke yake, iko nchi nyingi. Nchi zetu za Afrika Mashariki na Kati, migogoro hii ni mingi sana na wenzetu kwa mfano, Ethiopia wamejaribu kuitatua kwa namna ambavyo imeleta muafaka kati ya wakulima na wafugaji. Kwa hiyo, tulipendekeza watumishi hawa wapewe nafasi ya kwenda kujifunza namna wenzao walivyotatua migogoro hii na kuleta amani katika maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo lingine ambalo tulitoa ni hili ambalo linazungumzwa sasa hivi kuhusu upimaji wa ardhi. Migogoro haiko kwa wakulima na wafugaji peke yake au kwa wakulima na hifadhi peke yake au na wawekezaji peke yake, lakini hebu tazameni; ukitoka Dar es Salaam kuja Dodoma, sasa miji hii inaungana, maana yake kuna ujenzi holela wa ovyo ovyo tu. Dar es Salaam imeshaungana na Chalinze; Chalinze imeshaungana na Morogoro; Arusha imeungana na Bomang‟ombe; Bomang‟ombe imeungana na Moshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiachia hali hii iendelee, maana yake ni kwamba huko tuendako Taifa hili litakosa ardhi ya kilimo, kwa sababu kila anayefikiria kuweka jengo lake analiweka mahali popote anapotaka. Ni matumaini yangu kwamba Mheshimiwa Lukuvi hili atalizingatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na upimaji, Wizara ilikuwa na mfuko maalum ambao ulikuwa unazisaidia Halmashauri kukopa ili kuweza kufanya upimaji katika Halmashauri zao. Ulikuwa unaitwa Plot Development Revolving Fund.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasi watu wa Rombo tulipeleka maombi yetu Wizarani kwa ajili ya kukopa fedha hizi ili tuweze kufanya upimaji, mpaka leo hatujajibiwa na nadhani pengine Mfuko umekufa. Nadhani hiki kilikuwa kitu kizuri. Wizara iangalie namna ya kuboresha huu Mfuko ili Halmashauri ziweze kukopa fedha kwa ajili ya kusaidia kupima katika maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, ni hiki kilio cha kila Halmashauri kirejeshewe mapema ile retention wanapokusanya kodi ya ardhi. Mara nyingi inachelewa, sasa matokeo yake ni kwamba zile Ofisi za Ardhi katika Halmashauri zinakuwa kama zimefungwa miguu na mikono, hazina nyenzo, hazina fedha, kwa sababu hiyo upimaji unakuwa ni mgumu sana na utekelezaji wa majukumu yao pia unakuwa ni mgumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, nizungumze kidogo kuhusu Jimbo langu. Katika Jimbo langu kuna eneo la Ziwa Chala. Hili ni ziwa pekee katika Afrika kama siyo dunia. Ni ziwa pekee ambalo maji yake hayajachafuliwa kwa asilimia 85. Sasa hivi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinafanya utafiti wa namna tabianchi ilivyobadilika kwa miaka 500,000 iliyopita kwa kutumia lile ziwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sijui Halmashauri au Wizara, ilikwenda ikakabidhi watu iliyowaita wawekezaji eneo la lile ziwa na kuwamilikisha. Pamoja na hayo, ardhi inayozunguka lile ziwa ni ardhi ambayo wananchi wa Kata ya Holili, Chala, Mamsera, Ngoyoni na Mengwe walikuwa wamemilikishwa zamani na iliyokuwa inaitwa Land Board. Sasa wananchi wa Kata hizi wanazuiwa kwenda kwenye maeneo yao, wanapigwa, wanadhalilishwa na wenzao wawili matajiri ambao ni Warombo kule kule waliokwenda kumleta Mzungu wakamweka pale kwa kigezo kwamba ile ardhi ni mali yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Wizara kwa sababu waliopewa hiyo ardhi walikuwa viongozi katika Serikali ya Chama cha Mapinduzi, mwone kwamba jambo kama hili linawachafua. Kata nilizotaja ni karibu tano, wazee wanapigwa, akinamama wanapigwa na watu wachache waliopewa ardhi yao wanadai kwamba ni mali yao. Naamini Mheshimiwa Lukuvi kwa kasi aliyoonesha na kwa usikivu alioonesha, nami niseme ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, siyo dhambi kumpa pongezi Mheshimiwa Lukuvi. Siyo dhambi hata kidogo, kwa sababu hata mimi binafsi niseme tu kwamba, kuna mambo aliyonitendea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilidhulumiwa kiwanja Tegeta tangu mwaka 1994. Nimekwenda kwenye haya mnayoita Mabaraza za Ardhi, nimehangaika sikupata haki yangu; lakini Mheshimiwa Lukuvi ameingia, haki yangu nimepata. Sasa ndiyo maana nasema siyo dhambi kama jambo zuri likifanyika lisemwe. Nami ningesema na wengine waige mfano wa Mheshimiwa Lukuvi wa kutatua mambo kwa haraka. Kwa hiyo, ni imani yangu kwamba hata hili la Ziwa Chala Mheshimiwa Lukuvi atalifuatilia na alitatue kwa masilahi ya watu wangu wa Rombo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, pale Tarakea kuna kiwanja cha vijana cha kucheza mpira, watu wamefanya siasa tu, wakampa mfanyabiashara mmoja anaitwa Maulidi, kajenga hapo jengo lake. Sasa kwa uhaba wa ardhi tuliyonao Rombo, vijana wetu hawana mahali pa kuchezea, lakini tajiri kaweka jengo pale, liko limesimama naye anatumika kwa ajili ya kukisaidia Chama chenu kwenye kampeni, anatoa pesa za kampeni. Matokeo yake kwa kuwa anatoa pesa za kampeni, hakuna mtu anayemgusa. Ni imani yangu kwa kasi hiyo hiyo pia Mheshimiwa Waziri atakwenda pale aangalie jambo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kata ya Mengwe, hili nililisema kwenye Wizara ya Ujenzi, tuna kiwanja pia cha watoto cha kucheza mpira. Wameweka hapo matingatinga tangu mwaka gani sijui, yako pale, vijana hawana mahali pa kuchezea, hebu Mheshimiwa Lukuvi aangalie namna ya kutusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niseme tu, Mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla tuna matatizo makubwa sana ya ardhi. Wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro nao ni Watanzania, nimesikia tukizungumza hapa kuhusu mashamba ambayo Serikali inayarejesha kwa wananchi. Naomba kama unaweza ukawekwa utaratibu hata wananchi wa maeneo ambayo ni highly populated kama Rombo, vijana wana moyo wa kufanya kazi ya kilimo, lakini hawana maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wapo tayari kwenda kwenye maeneo mengine ya nchi ambayo wakipewa ardhi kwa utaratibu fulani wanaweza wakaendeleza kilimo. Nami niko tayari kuwaorodhesha vijana kama hao na kuwapeleka ofisini kwa Mheshimiwa Waziri ili kama kuna shamba fulani la Serikali watalitoa, basi na wale vijana wanufaike kwa sababu nao ni Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kujua, huu utaratibu wa kupima ardhi ambazo tunapata hati zile za kimila, sijui namna gani, kwa mashamba ya kimila kama ya Kilimanjaro, vile vihamba ambavyo vina makaburi, tunaambiwa hatuwezi kukopa kwa sababu mashamba yetu yana makaburi, upimaji wake unafanyika namna gani. Sisi tutakosa hiyo haki kwa sababu siyo dhambi sisi kuzika kule kwenye vihamba vyetu, ni kwa sababu ya ukosefu wa ardhi. Mheshimiwa Waziri aangalie namna ya kutusaidia ili wale wananchi waweze kupata manufaa ya ardhi yao.